Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Obama ampigia simu Trump kumpongeza

Mgombea wa Republican Donald Trump amemshinda Hillary Clinton wa Democratic katika uchaguzi wa urais uliokuwa na ushindani mkali.

Moja kwa moja

  1. Habari za hivi punde, Trump: Asanteni sana

    Trump amepanda jukwaani Manhattan, New York. Amewashukuru wafuasi wake na kusema amepigiwa simu na Hillary Clinton "kuwapongeza".

    Aidha, amesema mwenyewe amempongeza Bi Clinton.

      "Hillary amefanya kazi kwa bidii sana na kwa muda mrefu sana na twafaa kumshukuru kwa alivyoitumikia nchi yetu," Bw Trump amesema.

    "Sasa ni wakati wa Marekani kuponya vidonda vya mgawanyiko."

  2. Habari za hivi punde, Mike Pence, makamu wa rais mteule jukwaani

      Mike Pence, mgombea mwenza wa Donald Trump, na mkewe Karen, wamejitokeza na kupanda jukwaani mkutano wa Trump wa kusherehekea ushindi jimbo la Manhattan.  

  3. Shangwe kambi ya Trump

    Shangwe, nderemo na vifijo zimetanda miongoni mwa wafuasi wa Donald Trump.

  4. Habari za hivi punde, Clinton akubali kushindwa

      CNN na NBC wameripoti kwamba mgombea wa chama cha Democratic Hillary Clinton amempigia simu Donald Trump na kukubali kushindwa.

  5. Habari za hivi punde, Maafisa wa Clinton wasema ni mapema mno

    Mwenyekiti wa kampeni wa Hillary Clinton John Podesta amesema bado ni mapema mno na maafisa wa kampeni wa Clinton hawawezi kusema lolote kwa sasa.

    "Bado wanahesabu kura na kila kura ina umuhimu ... majimbo kadha kura zimekaribiana sana kwa hivyo hatutasema mengine zaidi leo.

    "Kila mtu anafaa kwenda nyumbani, alale. Tutasema mengi kesho."

  6. Habari za hivi punde, Trump na Clinton wagawana kura Maine

    ABC News wanakadiria kwamba kura tatu za wajumbe kati ya nne jimbo la Maine zitamwendea Bi Clinton.

    Moja itachukuliwa na Trump.

    Jimbo hilo limekuwa likiunga mkono Democratic. Mwaka 2008, Obama alikuwa mbele kwa asilimia 17. Maine na Nebraska ndiyo majimbo pekee ambapo wagombea wanaweza kugawana kura za wajumbe.

  7. Majonzi kambi ya Clinton, shangwe kwa Trump

    Wafuasi wa wagombea wakuu wa urais nchini Marekani Hillary Clinton na Donald Trump wamepokea matokeo yanayoendelea kutangazwa kwa hisia tofauti mjini New York.  

  8. Habari za hivi punde, Masikitiko yakumba kambi ya Clinton

    Timu ya Trump ilitaraji kwamba mgombea wao angeshinda uchaguzi kama jana lakini matokeo ya uchaguzi yamewakosoa. 

     Mwandishi wa BBC Chris Gibson amekuwa akizungumza na wafuasi wa Clinton katika mkutano wake huko New York,akiwemo mfuasi mmoja ambaye alidhani kwamba matokeo hayo yangemfanya 'atapike'.

  9. Kufuatilia matokeo ya uchaguzi wa Marekani, Nairobi

    Maafisa wa ubalozi wa Marekani, raia wa Marekani pamoja na wanahabari kadha walioalikwa, wamekuwa wakifuatilia matokeo ya uchaguzi ubalozi wa Marekani jijini Nairobi.

    Hivi ndivyo hali ilivyo:

  10. Mashabiki wa Trump wafurahia matokeo

    "Umekuwa usiku mwema kwa mashabiki wa Donald Trump ,usiku mwema kwa raia wa Marekani na usiku mwema zaidi kwa walimwengu,Curtis Ellis mshauri mwandamizi wa timu ya kampeni za Trump .

  11. Obama: "Jua lazima litachomoza asubuhi"

    Kwenye ujumbe wa video, Ras Obama amesifu demokrasia bila kujali nani atashinda usiku huu (Marekani bado ni usiku).

    Amesema bila kujali kitakachotokea, "Jua lazima litachomoza asubuhi."

    Ameandika kwenye Twitter na kuwashauri wapiga kura "kutazamana sio tu kama wafuasi wa Democratic au Republican bali kama Wamarekani".

  12. Trump yuko wapi kwa sasa?

    Donald Trump ameondoka Trump na kuelekea hoteli ya Hilton Midtown ambapo anatarajiwa kuandaa mkutano wa ushindi

    Jeff DeWitt, mkuu wa fedha jimbo la Arizona, amekuwa na Bw Trump wakifuatilia matokeo ya uchaguzi.

    Amepakia picha ya Trump akimfunga tai mwanawe, na nyingine ya Trump na mgombea mwenza wake Mike Pence wakifuatilia matokeo.

    Tazama:

  13. Wamarekani walivyopokea ushindi wa Trump Florida

    Hivi ndivyo Wamarekani walivyopokea matokeo ya uchaguzi mjini Florida

  14. Habari za hivi punde, Clinton ashinda jimbo la Nevada

    Hillary Clinton ameshinda uchaguzi wa urais jimbo la Nevada, ambapo amejizolea kura 6 za wajumbe. Sasa ana kura 215 naye Trump 244. Mshindi anahitaji kura 270.

  15. Mambo yalivyobadilika kwa Trump na Clinton

    Wengi wameanza kujadili uwezekano wa Trump kuibuka mshindi. New York Time, gazeti lililokuwa linamuunga mkono Hillary Clinton, limechapisha mchoro wa jinsi matarajio ya mshindi wa urais yalivyobadilika.

    Nate Silver, anayeandika blogu ya FiveThirtyEight (538 ni idadi ya kura za wajumbe) amesema pia kuna uwezekano wa Donald Trump kushinda urais.

    Silver anafahamika kwa kuweza kutabiri matokeo katika majimbo yote 50 mwaka  2012.

    Tazama mchoro hapa chini:

  16. Itakuwaje wagombea wakitoshana nguvu?

    Iwapo wagombea wote wawili watatoshana nguvu kwa kura za wajumbe, kila mmoja apate kura 270, basi Bunge la Wawakilishi ndilo litakaloamua nani atakuwa rais.

  17. Habari za hivi punde, Clinton ana 'njia moja pekee ya kushinda'

    Hillary Clinton sasa atahitajika kushinda majimbo ya Pennsylvania, Michigan na Wisconsin iwapo atashinda urais kulingana na Norm Ornstein.

     "Ana njia moja ya kupata ushindi huku Trump akiwa na njia nyingi''.

    Mwandishi wa BBC wa Amerika Kaskazini Anthony Zurcher pia anakubaliana na Ornstein kuhusu umuhimu wa Michigan na Wisconsin.

  18. Habari za hivi punde, Trump ajipatia kura 16 kutoka Georgia

    Donald Trump ameshinda jimbo la Georgia kwa mujibu wa makadirio ya ABC News. Jimbo hilo lina kura 16 za wajumbe. Sasa Trump ana kura 244 naye Clinton 209. Mshindi anahitaji kura 270 za wajumbe.

  19. Habari za hivi punde, Trump ashinda jimbo la Iowa

    Donald Trump ameshinda jimbo la Iowa, kwa mujibu wa makadirio ya ABC News. Amejishindia kura 6 za wajumbe. Sasa ana 228 naye Clinton 209. Mshindi anahitaji kura 270.

  20. Habari za hivi punde, Clinton ashinda jimbo la Washington

    Hillary Clinton ameshinda jimbo la Washington kwa mujibu wa makadirio ya ABC News. Jimbo hilo lina kura 12 za wajumbe. Sasa Trump ana kura 222 za wajumbe na Clinton 209 za wajumbe. Mshindi anahitaji kura 270.