Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Virusi vya Corona: Chanjo ya Urusi yaonesha dalili za kukabiliana na virusi
Wanasayansi wa Urusi wamechapisha taarifa ya kwanza juu ya chanjo yao ya virusi vya corona, wakisema kuwa vipimo vya awali vimeonesha ishara ya chanjo hiyo ya kuuwezesha mfumo wa kinga ya mwili kupambana na virusi.
Ripoti iliyochapishwa na jarida la kitabibu la The Lancet ilisema kuwa kila mshiriki aliyepewa chanjo hiyo aliweza kutengeneza sehemu ya protini ya damu inayoweza kuua virusi, bakteria na vimelea wengine hatari wanaoshambulia mwili wa binadamu(Antibodies) na haikuwa na athari mbaya.
Urusi iliidhinisha chanjo hiyo kutumiwa ndani ya nchi mwezi Agosti, ikiwa ni nchi ya kwanza duniani kufanya hivyo kabla ya kuchapishwa kwa data juu ya ufanisi wa chanjo.
Wataalamu wanasema majaribio yalikuwa ni madogo sana kuweza kuidhinisha ufanisi na usalama wa chanjo hiyo.
Lakini utawala wa Moscow umesifu matokeo ya chanjo yao na kuyataja kama jibu kwa wakosoaji.
Baadhi ya wataalamu wa nchi za magharibi wameelezea hofu zao juu ya kasi ya kazi ya Urusi, wakisema kwamba watafiti huenda walitumia njia fupi kutengeneza chanjo hiyo.
Mwezi uliopita Rais Vradimir Putin alisema kwamba chanjo hiyo imepita vigezo vyote vya uchunguzi na mmoja wa watoto wake wa kike alipewa chanjo hiyo.
Je ripoti inasema nini ?
Majaribio mawili ya chanjo, yanayofahamika kama Sputnik-V, yalifanyika Juni na Julai, Jarida la Lancet lilisema. Kila jaribio liliwahusisha watu 38 waliojitolea kupewa chanjo ambao walipewa dozi ya chanjo na baadae wakapewa kichocheo cha chanjo wiki tatu baadaye.
Washiriki -waliokuwa na umri wa kati ya miaka 18 na 60 -walifuatiliwa kwa siku 42 na wote miili yao ilitengeneza protini ya damu ya kinga dhidi ya virusi na bakteria katika kipindi cha wiki tatu. Miongoni mwa athari za kawaida za chanjo hiyo zilikuwa ni maumivu ya kichwa na maumivu ya viungo.
Majaribio hayo yalikuwa ya wazi kwa anayetaka na walishiriki hawakuchaguliwa bila mpangilio, ikimaanisha kuwa waliojitolea walikuwa wanatambua kuwa walikua wanapokea chanjo.
"Majaribio makubwa na ya muda mrefu huhusisha mbinu ya kulinganisha wale waliofahamu kabla na ambao hawakufahamu kuwa wanakwenda kuchanjwa chanjo na ufuatiiaji zaidi unahitajika ili kubaini usalama wa muda mrefu na ufanisi wa chanjo ili kuzuwia maambukizi ya Covid-19 ," ilisema ripoti.
Awamu ya tatu ya jaribio la chanjo hiyo itawahusisha watu 40,000 "wa umri tofauti na makundi yanayokabiliwa na hatari ya maambukizi ," kwa mujibu wa jarida la Lancet.
Chanjo ya Urusi hutumia kirusi cha adenovirus, ambacho kwa kawaida husababisha homa ya mafua ya kawaida kuchochea ufanisi wa kinga ya mwili.
Unaweza pia kusoma:
Je chanjo maoni juu ya chanjo hii ni yapi ?
Kirill Dmitriev, mkuu wa mfuko wa uwekezaji nchini Urusi ambao ulidhamini chanjo hiyo, alisema wakati wa kikao na waandishi wa habari kuwa ripoti ilikuwa "jibu la nguvu kwa wasio na imani na chanjo ambao wanakosoa bila sababu chanjo ya Urusi ".
Alisema kuwa watu 3,000 tayari wamepata mafunzo kwa ajili ya majaribio ya awamu ijayo.
Waziri wa afya wa Urusi Mikhail Murashko alisema kuwa nchi itaanza kutoa chanjo hiyo kwa watu kuanzaia mwezi Novemba au Disemba, walengwa wakuu wakiwa ni makundi yanayokabiliwa na hatari zaidi.
Wataalamu walionya kuwa itachukua muda mrefu kwa chanjo ya corona kupatikana sokoni.
Brendan Wen, Profesa wa vimelea wa bakteria katika taasisi ya-London School of Hygiene and Tropical Medicine, aliliambia shirika la habari la Reuters kwamba : "Ripoti ni suala la hadi sasa, mambo sasa ni mazuri '".
Kwa mujibu wa Shirika la afya duniani (WHO), kuna chanjo 176 zinazotengenezwa kwa sasa kote duniani . Kati ya chanjo hizo 34, zinafanyiwa majaribio kwa watu . Miongoni mwa hizo, nane ziko katika ngazi ya tatu, ambacho ndio kiwango cha juu zaidi kinachokaribia mchakato wa kuidhinishwa.