Matokeo ya Uchaguzi Kenya 2022: Mbivu na mbichi kujulikana

Iliyochapishwa

Matokeo ya muda yanaonesha ushindani mkali wa kura za urais nchini Kenya kati ya Naibu Rais William Ruto na waziri mkuu wa zamani Raila Odinga.

Huku ikiwa zaidi ya asilimia 90% ya matokeo yametumwa kutoka mashinani, hesabu za ndani za data zinaonesha kwamba wawili hao wamekabana koo.

Hata hivyo inaweza kuchukua siku kadhaa kabla ya matokeo rasmi kutagazwa.

Uchaguzi huu unajiri baada ya kipindi cha kampeni kali iliyotawaliwa na mijadala kuhusu gharama za maisha, ukosefu wa ajira na ufisadi.

Waliojitokeza kupiga kura wanakadiriwa kuwa karibu 60%, ikiwa ni idadi ndogo ikilinganishwa na asilimia 80% katika uchaguzi uliopita miaka mitano iliyopita.

Siku ya uchaguzi iliokuwa na amani kwa kiasi kikubwa ilikumbwa na ucheleweshaji wa vifaa na kushindwa kwa kifaa cha kielektroniki kutambua baadhi ya wapiga kura katika maeneo kadhaa nchini.

Baba dhidi dhidi ya 'Hustler'

Wapinzani wawili katika kinyang'anyiro cha urais ni wanasiasa wenye uzoefu.

Bw Odinga, 77, - kiongozi wa upinzani wa muda mrefu, anayeitwa Baba ("baba") , anawania urais kwa mara ya tano. Bw Ruto, 55, ambaye amejaribu kusisitiza uhusiano wake na Wakenya wa kawaida kwa kujiita "hustler", anawania wadhfa huo kwa mara ya kwanza.

Wagombea wengine wawili - David Mwaure na George Wajackoya - pia wako kwenye kinyang'anyiro hicho.

Rais anayeondoka Uhuru Kenyatta anaunga mkono Bw Odinga, mpinzani wake aliyegeuka kuwa mshirika wake, kumrithi, baada ya kutofautiana na Bw Ruto.

Ili kushinda kinyang'anyiro cha urais katika awamu ya kwanza, mgombea anahitaji:

  • Zaidi ya nusu ya kura zote zilizopigwa kote nchini
  • angalau 25% ya kura zilizopigwa katika angalau kaunti 24.

Baada ya kuhesabu kura, viongozi wa eneo hilo huchukua picha ya karatasi ya mwisho ya kujumlisha na kutuma picha hiyo kwa maeneo bunge na vituo vya kitaifa vya kujumlisha kura.

Vyombo vya habari, vyama vya kisiasa na mashirika ya kiraia yamekuwa yakikusanya hesabu zao kwa kutumia matokeo haya ya mwisho yaliyotangazwa katika vituo zaidi ya 40,000 vya kupigia kura.

Lakini tume ya uchaguzi pekee ndiyo inayoweza kutangaza mshindi wa uchaguzi wa urais baada ya kuthibitisha fomu halisi na za kidijitali zinazotumwa kwa kituo cha kitaifa cha kuhesabia kura.

IEBC ina siku saba kutangaza matokeo.