Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Odinga na Kenyatta: Mambo yalivyokuwa siku ya Uchaguzi Mkuu Kenya 2017 tarehe 8 Agosti

Muungano wa upinzani nchini Kenya umepinga matokeo ya urais ambayo yamekuwa yakitangazwa na tume ya taifa ya uchaguzi IEBC.

Moja kwa moja

  1. Wapiga kura kituo 'cha Bw Odinga'

    Wapiga kura katika kituo cha shule ya msingi ya Olympic katika mtaa wa Kibera, Nairobi walifika mapema.

    Abdinoor Aden ametutumia picha hizi za wapiga kura, baadhi wakitafuta majina yao katika orodha ya wapiga kura iliyowekwa ukutani. Baadhi wamekuwa wakitumia taa za simu zao kumulika.

    Mgombea urais wa muungano wa upinzani National Super Alliance Raila Odinga anatarajiwa kupiga kura yake katika kituo hicho baadaye leo mchana.

  2. Wakenya waliokesha vituo vya kupigia kura

    Baadhi ya Wakenya wamekesha katika vituo vya kupigia kura. Kwa nini? Msikilize mmoja wao.

  3. Mambo muhimu kuhusu uchaguzi wa urais Kenya 2017

    Uchaguzi wa mwaka huu una ushindani mkubwa kati ya Rais Kenyatta na Bw Odinga, rais huyo akipigania kuchaguliwa tena. Katika majimbo 47, uchaguzi unafanyika mara ya pili kuwachagua magavana baada ya kutekelezwa kwa mfumo wa ugatuzi mwaka 2013.

    BBC imekuandalia mambo muhimu unayofaa kuyafahamu kuhusu uchaguzi huo.

    Tazama:

  4. Waziri awahakikishia Wakenya usalama wakipiga kura

    Kumekuwa na wasiwasi kuhusu hali ya usalama nchini Kenya, hasa kutokana na ushindani mkali unaoshuhudiwa kati ya wagombea urais wawili wakuu.

    Wengi bado wanakumbuka ghasia zilizozuka baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2007, miaka kumi iliyopita.

    Aidha, majuzi meneja wa masuala ya teknolojia wa tume ya uchaguzi IEBC Chris Musando aliuawa na watu wasiojulikana.

    Kaimu waziri wa usalama wa ndani Dkt Fred Matiang'i amewahakikishia Wakenya kwamba usalama umeimarishwa na hawafai kuwa na wasiwasi wakipiga na hata baada ya kupiga kura.

    "Sisi wenyewe tumekomaa kisiasa kama nchi, mipango yetu ya kuandaa uchaguzi imeimarika zaidi na tume huru ya kusimamia uchaguzi imekuwa ikiimarika kila wakati. Sioni haja ya mtu yeyote kuhama kutoka sehemu moja hadi nyingine," Dkt Matiang'i aliambia BBC.

    Msikilize hapa:

  5. Familia za Kenyatta na Odinga

    Kwa mara nyingine tena, Uhuru Kenyatta na Raila Odinga, wanashindania uongozi wa taifa la Kenya baada ya kukabiliana tena Machi 2013.

    Rais Kenyatta ni mwana wa rais wa kwanza wa Kenya, Mzee Jomo Kenyatta naye Bw Odinga mwana wa makamu wa rais wa kwanza Jaramogi Oginga Odinga.

    Familia hizo zilianza kwa kuwa marafiki wa kufa kuzikana wakati wa Kenya kujipatia uhuru wake. Jaramogi alipewa fursa ya kuwa kiongozi wa kwanza wa Kenya na Waingereza lakini akaikataa fursa hiyo na kusema Kenya haiwezi kupokea uhuru kiongozi wake Mzee Kenyatta akiwa jela.

    Jomo Kenyatta aliachiliwa na akawa waziri mkuu na mwaka mmoja baadaye baada ya Kenya kuwa jamhuri akawa rais wa kwanza wa Kenya, na Jaramogi akawa makamu wake.

    Lakini uhasama ulizuka mwaka 1966 na Kenyatta akamfuta kazi Jaramogi na kuanzia hapo uhasama wa muda mrefu kati ya jamii ya Wakikuyu (Kenyatta) na Wajaluo (Odinga) ukaanza.

    Uhuru Kenyatta na Odinga walishindana katika uchaguzi wa urais mwaka 2013 na Bw Kenyatta akaibuka mshindi.

    Wakati huu, kivumbi tena ni kati ya wawili hao.

    Bw Odinga anagombea urais mara ya nne na ushindani kati ya wawili hao ni kama umefikia kilele.

  6. Wapiga kura waanza kufika vituoni

    Ingawa vituo vya kupigia kura vitafunguliwa rasmi saa kumi na mbili, wapiga kura wameanza kujitokeza vituoni.

    Katika baadhi ya vituo, watu walifika mapema mwendo wa saa tisa hizi.

    Tayari vituo vingi kuna foleni.

    Mwandishi wa BBC Dayo Yusuf alikutana na baadhi yao katika kituo kimoja Nairobi:

  7. Hujambo!

    Karibu kwa taarifa za moja kwa moja kuhusu uchaguzi mkuu wa Kenya. Wapiga kura 19 wanatarajiwa kufika vituoni kumchagua rais, , magavana wa kaunti, wabunge, maseneta, wawakilishi wa wanawake na wawakilishi wa wadi.