Timu za Afrika zimefanyaje hadi sasa Kombe la Dunia 2026?
Timu za Afrika zimekuwa na matokeo yanayochanganya katika hatua za awali za Kombe la Dunia 2026, huku baadhi zikionyesha uwezo mkubwa dhidi ya vigogo wa soka duniani.
Morocco imekuwa miongoni mwa timu zilizovutia zaidi baada ya kutoka sare ya 1-1 dhidi ya Brazil kabla ya kuifunga Scotland 1-0 katika Kundi C. Simba wa Atlas sasa wanasalia na mchezo mmoja dhidi ya Haiti huku wakionekana kuwa katika nafasi nzuri ya kusonga mbele.
Kundi L, Ghana ilianza kampeni yake kwa ushindi wa 1-0 dhidi ya Panama na sasa inajiandaa kwa mtihani mkubwa dhidi ya England Jumanne. Nayo DR Congo iliandika matokeo ya kuvutia baada ya kuilazimisha Ureno sare ya 1-1, wakati Misri ilitoka sare ya 1-1 dhidi ya Ubelgiji katika Kundi G.
Cape Verde nayo imeendelea kuonyesha kuwa si timu ya kubezwa baada ya kutoka sare ya 0-0 dhidi ya Hispania, moja ya timu zinazopewa nafasi kubwa kwenye michuano hiyo.
Hata hivyo, si timu zote za Afrika zimeanza vizuri. Senegal ilipoteza 3-1 dhidi ya Ufaransa, Afrika Kusini ilifungwa 2-0 na Mexico kabla ya kutoka sare ya 1-1 na Jamhuri ya Czech, huku Tunisia ikipokea kichapo kizito cha mabao 5-1 kutoka Sweden katika Kundi F.

