Maandamano, Uhaba, hofu na Ukimya - Upi mustakabali wa Tanzania
Ni siku ya tano sasa tangu huduma za intaneti nchini Tanzania zikatwe, hatua iliyoathiri upatikanaji wa taarifa sahihi kuhusu hali ya kiusalama kufuatia maandamano makubwa yaliyoshuhudiwa kati ya Jumatano na Ijumaa wiki iliyopita.
Chanzo cha kidiplomasia kimeiambia BBC kuwa kuna ushahidi wa kuaminika unaoonyesha kuwa angalau watu 500 wameuawa katika ghasia hizo.
Hata hivyo, Waziri wa Mambo ya Nje, Balozi Thabit Kombo, ameeleza kuwa serikali haiwezi kuthibitisha idadi hiyo rasmi. Wengine wanasemekana kukamatwa au hawajulikani walipo, huku mashuhuda walioko Dar es Salaam wakieleza kusikia milio ya risasi katika siku mbili za mwanzo za maandamano.
Hali hiyo imekuja sambamba na amri ya kutotoka nje katika baadhi ya maeneo, huku Mkuu wa Majeshi jenerali Nkunda akionya kuwa JWTZ halitasita kuchukua hatua kali dhidi ya yeyote atakayevunja amani.
Wakati huo huo, Tume Huru ya Uchaguzi INEC imemtangaza Samia Suluhu Hassan kuwa Rais mteule wa Tanzania na kumkabidhi cheti cha ushindi — hatua iliyozua maoni mseto katika mitandao ya kijamii kabla ya mitandao hiyo kufungwa.
Hali ya maisha kwa raia wengi imezorota. Mafuta yamepanda bei mara nne kwenye soko la magendo, vituo vya mafuta vimefungwa, na usafiri wa umma umesimama. Ni bodaboda wachache pekee wanaoendelea kufanya kazi, wakitoza bei kubwa. Ukosefu wa mafuta na usafiri unakwamisha usafirishaji wa bidhaa muhimu kama chakula.
Maduka mengi yamefungwa, mengine yakiishiwa bidhaa. Wakati huo huo, huduma za benki na malipo ya kidijitali zimevurugwa kutokana na kukosekana kwa intaneti. Uingereza imetoa onyo kwa raia wake, ikitaja uhaba wa chakula, mafuta, fedha taslimu na intaneti, na kuwataka wasafiri kuepuka safari zisizo za lazima.
Kwa sasa, kukosekana kwa intaneti kumezidisha ukosefu wa taarifa zilizothibitishwa. Mitandao ya kijamii kama X, Instagram, TikTok na Telegram nchini Kenya imefurika video na madai kuhusu kinachoendelea Tanzania, lakini wachambuzi wanasema si zote ni za ukweli. Mfano mmoja ni video iliyosambaa ikionyesha watu wakikimbia katika Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere — tukio lilihusiana na mapokezi ya mwili wa hayati Rais John Magufuli mwaka 2021.
Wataalamu wa usalama wa kidijitali wanatahadharisha kwamba kufungwa kwa mitandao kunazidisha uwezekano wa upotoshaji wa habari. Mtaalamu George Musalama ameiambia BBC: “kukosekana kwa intaneti kunazidisha taharuki na kutoa nafasi kwa propaganda kuenea bila uthibitisho wowote.”
Kuhusu intaneti WaziriKombo alisema kuwa serikali ilichukua hatua ya kuminya mitandao ili kukomesha mawasiliano kati ya, kwa maneno yake, “vijana wahuni waliokuwa wanaitumia kupanga vitendo vya uvunjifu wa amani.”











