Matokeo ya uchaguzi Kenya 2022: Vigogo wa William Ruto walioshindwa katika maeneo yao

    • Author, Abdalla Seif Dzungu
    • Nafasi, BBC Swahili
  • Iliyochapishwa

Licha ya naibu wa rais William Ruto kuwa katika kinyang'anyiro kikali kati yake na kiongozi wa Muungano wa Azimio Raila Odinga katika uchaguzi wa urais , Kiongozi huyo hakuponea wimbi la chama cha mpinzani wake katika maeneo mbalimbali nchini.

Jijini Nairobi wakili Maarufu mjini na mgombea wa chama cha UDA katika eneo bunge la Westlands Nelson Havi alikuwa wa kwanza kukubali kushindwa na mgombea wa Muungano wa Azimio Tim Wanyonyi.

Harvey ambaye ni wakili maarufu alikiri kushindwa wakati ambapo matokeo bado yalikuwa yakitiririka kutoka vituo mbalimbali vya eneo bunge hilo.

Alimpongeza mpinzani wake Tim Wanyonyi kwa kutetea kiti chake.

Bwana Nelson Havi ni miongoni mwa mawakili wa Ruto waliowasilisha kesi ya pingamizi dhidi ya BBI.

Wakati huohuo aliyekuwa mbunge wa eneo la Lang'ata mjini Nairobi Nixon Korir alikiri kushindwa na mcheshi maarufu nchini Felix Odiwour Jalang'o katika kiti cha ubunge cha Langata.

Jalang'o aliyewania kiti hicho kwa tikiti ya chama cha ODM alimpatia kongole bwana Korir kwa kukubali kushindwa.

Vilevile Diwani wa wadi ya Sirikwa Alfred Mutai ametangazwa mshindi wa kiti cha eneo bunge la Kuresoi Kaskazini.

Afisa wa Uchaguzi wa eneo bunge hilo Lilian Akoth alimtangaza Bw Mutai kuwa mbunge mpya Alhamisi asubuhi baada ya kujizolea kura 25,365 dhidi ya wagombea wanne.

Bw Mutai ambaye alikuwa akiwania kwa tikiti ya UDA alikuwa kwenye kinyang'anyiro kikali na Moses Cheboi-naibu spika wa bunge la Kitaifa ambaye alikuwa anawania kama mgombea huru lakini katika mrengo wa naibu rais William Ruto.

Na hayo yakijiri mbunge wa Garisaa mjini Aden Duale alishindwa kuukabili umaarufu wa kiongozi wa Azimio Raila Odinga katika eneo bunge lake baada ya Odinga kujipatia kura nyingi ikilinganishwa na alizopata Naibu wa rais William Ruto. Duale ni mshirika wa karibu sana wa Ruto.

IEBC ina siku saba kutangaza matokeo.