Mwanamke afariki baada ya gari la Tesla kutoka barabarani na kugonga nyumba
Maafisa wa usalama wa usafiri nchini Marekani wanafanya uchunguzi kuhusu ajali mbaya iliyohusisha gari la Tesla lililotoka barabarani na kugonga nyumba.
National Highway Traffic Safety Administration ilitangaza Jumatatu kuwa imefungua uchunguzi rasmi kuhusu ajali hiyo iliyotokea tarehe 19 Juni katika jimbo la Texas, ambapo gari la Tesla lilitoka nje ya barabara na kugonga nyumba ya makazi.
Kwa mujibu wa polisi wa eneo hilo, mwanamke aliyekuwa ndani ya nyumba hiyo alipata majeraha mabaya na baadaye alifariki kutokana na ajali hiyo.
Polisi walisema kuwa dereva hakuwa chini ya ushawishi wa pombe au dawa za kulevya. Dereva huyo aliwaambia wachunguzi kwamba gari lilikuwa likitumia mfumo wa usaidizi wa uendeshaji wa kiotomatiki wakati ajali ilipotokea.
Msemaji wa NHTSA alisema:
“Wakala umeanzisha uchunguzi maalumu kuhusu ajali hii.”
Kwa upande mwingine, mwakilishi wa Tesla, kampuni inayomilikiwa na bilionea wa Marekani Elon Musk, hakujibu maombi ya kutoa maoni kuhusu tukio hilo au uchunguzi unaoendelea.
Ajali hiyo ilitokea takribani saa 2:00 usiku kwa saa za eneo hilo siku ya Ijumaa.
Ripoti ya polisi inaeleza kuwa dereva wa gari aina ya Tesla Model 3 “alishindwa kudhibiti gari akiwa katika njia ya kupita magari mengine, akatoka nje ya barabara na kugonga nyumba ya makazi.”
Uchunguzi huo unalenga kubaini sababu halisi ya ajali hiyo na iwapo mfumo wa usaidizi wa uendeshaji wa gari ulikuwa na mchango wowote katika tukio hilo.
Unaweza kusoma;