Uchaguzi kenya 2022: Wakenya wahimili baridi kali alfajiri kupiga kura

Wapiga kura kenya
Maelezo ya picha, Wapiga kura kenya
    • Author, Abdalla Seif Dzungu
    • Nafasi, BBC Swahili
  • Iliyochapishwa
  • Muda wa kusoma: Dakika 4

Mamilioni ya Wakenya hii leo wamejitokeza katika vituo tofauti nchini kushiriki katika shughuli ya upigaji kura ambapo wanawachagua viongozi wao ikwemo rais mpya.

Wakenya hushiriki katika shughuli hiyo kila baada ya miaka mitano kama ilivyo katika katiba.

Na hii leo Wakenya walirauka alfajiri na mapema kupiga foleni wakiwa na lengo la kuwachagua viongozi wao baada ya kipindi kirefu cha kampeni .

Baadhi ya masuala yaliojadiliwa katika kipindi hicho cha kampeni ni pamoja na Ukosefu wa ajira, gharama ya juu ya maisha na ufisadi.

Zaidi ya Wakenya milioni 22 wamesajiliwa kushiriki katika shughuli hiyo katika zaidi ya vituo 40,000.

Wakati huohuo rais anayeondoka madarakani Uhuru Kenyatta amekuwa akimuunga mkono kiongozi wa upinzani Raila Odinga dhidi ya naibu wake William Ruto.

Huku Raila Odinga akitafuta uungwaji mkono kwa kushinikiza vita dhidi ya ufisadi katika kampeni yake, naibu wake William Ruto amekuwa akijihusisha zaidi na raia wa tabaka la chini akiwahakikishia kuinua hali yao ya maisha.

Ajuza akipiga kura kumchagua kiongozi wake
Maelezo ya picha, Ajuza akisaidiwa kumpigia kura kiongozi wake

Vituo vya Kupiga kura katika maeneo mengi ya nchi vilifunguliwa mwendo wa saa kumi na mbili kamili huku Wakenya wakihimili baridi kali kupiga foleni.

Baadhi ya raia wanadaiwa kulała vituoni ili kuwa katika mstari wa mbele katika shughuli hiyo.

Idara ya hali ya hewa nchini Kenya imesema kuwa sehemu kubwa ya nchi huenda ikawa kavu wiki hii hatua inayotoa fursa nzuri kwa Wakenya zaidi kushiriki katika shughuli hiyo.

Nani yuko kwenye kinyang'anyiro cha kuiongoza Kenya ?

Fahamu zaidi kuwahusu wagombea urais wa Kenya

Chagua mgombea ili kutazama wasifu wake

Raila Amollo Odinga

Muungano wa Azimio la Umoja

  • Mgombea huyo mwenye umri wa miaka 77 ni mhandisi aliyesomea Chuo Kikuu cha Ufundi cha Magdeburg (sasa kinajulikana kama Chuo Kikuu cha Otto-von-Guericke Magdeburg) nchini Ujerumani.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya Azimio la Umoja One Kenya Coalition Party.
  • Hili litakuwa jaribio lake la tano baada ya kugombea katika: 1997, 2007, 2013 na 2017.
  • Bw Odinga alikuwa mmoja wa wapiganiaji wa demokrasia ya vyama vingi nchini Kenya. Alikamatwa, akafungwa na wakati fulani akaenda uhamishoni kwa sababu ya kupigania haki hiyo
  • Aliwahi kuwa Waziri Mkuu, kuanzia 2008-2013.
  • Odinga alihusika kufanikisha miradi mikubwa iliyotekelezwa na serikali ya Kibaki, kama vile miradi ya umeme vijijini na barabara.
  • Kuafikia ukuaji wa uchumi wa tarakimu mbili kupitia uwekezaji katika biashara ndogo ndogo na sekta ya viwanda.
  • Utoaji wa huduma bora za afya kwa wote.
  • Utoaji wa vifaa vya michezo na burudani kwa ukuaji wa kimwili, kiakili, kijamii, kimaadili na maendeleo ya watu.
  • Kufuatia jaribio la mapinduzi ya Agosti 1, 1982, Raila Odinga alikamatwa na kukabiliwa na mashtaka kadhaa, yakiwemo ya uhaini ambayo alizuiliwa bila kufunguliwa mashtaka. Tume ya Ukweli ya Haki na Maridhiano iliambiwa mwaka 2011 kwamba Odinga alikuwa na mawasiliano na mpangaji mkuu wa mapinduzi hayo. Odinga amekana kuhusika kila mara. - Makavazi ya Kitaifa ya Kenya.

William Samoei Ruto

Muungano wa Kenya Kwanza

  • Mgombea huyu mwenye umri wa miaka 55 ana Shahada ya Uzamifu/PhD katika Ikolojia ya Mimea na BSc katika Botany na Zoology kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya chama cha United Democratic Alliance ( chenye mafungamano na Kenya Kwanza).
  • Aliongoza Vuguvugu la vijana la Youth for Kanu '92 (YK'(92).
  • Wizara yake iliorodheshwa kama inayofanya bora zaidi serikalini alipokuwa Waziri wa Kilimo.
  • Alihudumu kama Naibu Rais wa kwanza wa Kenya chini ya katiba mpya ya 2010.
  • Alihudumu kama mbunge wa eneo bunge la Eldoret Kaskazini kuanzia 1997-2007.
  • Kutenga $424 milioni kila mwaka kwa biashara ndogo ndogo za kati.
  • Kuanzisha mfuko wa elimu wa kitaifa ili kukidhi gharama zisizo za masomo.
  • Tekeleza kikamilifu sheria ya usawa wa kijinsia ya thuluthi mbili katika uteuzi wa kisiasa na kutenga nusu ya baraza lake la mawaziri kwa wanawake.
  • Mnamo 2008, Mahakama Kuu ya Kenya iliamuru Naibu Rais William Ruto kusalimisha shamba la ekari 100 na kulipa $ 62,500 kwa Adrian Muteshi, mkulima ambaye alimshtaki kwa kuchukua mali hiyo baada ya uchaguzi wa 2007. - Kenya Law
  • Mnamo 2011, Bw Ruto alikabiliwa na kesi kwa makosa matatu dhidi ya binadamu: Mauaji, uhamisho wa watu kwa lazima na mateso ya watu katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu. Miaka mitano baadaye mahakama ilisitisha kesi hiyo kwa msingi kwamba - ushahidi wa upande wa mashtaka ulikuwa dhaifu. -ICC

George Wajackoyah

Chama cha Roots

  • Profesa huyo mwenye umri wa miaka 61 ana shahada ya uzamili katika sheria kuhusu maendeleo kutoka Chuo Kikuu cha Warwick na shahada ya uzamili , sheria (sheria za Marekani kutoka Chuo Kikuu cha Baltimore.
  • Bw Wajackoyah anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Roots Party.
  • Alihudumu kama Inspekta katika idara ya usalama ya Special branch wakati wa utawala wa marehemu Rais Daniel Moi kabla ya kulazimika kutorokea ng'ambo ili kuepuka kufunguliwa mashtaka na mamlaka.
  • Yeye ni mshirika katika kampuni ya mawakili aliyoianzisha mwaka wa 2018.
  • Alifunnza somo la sheria na uchumi katika vyuo vikuu vya Marekani, Uingereza na Kenya.
  • Kuhalalisha matumizi ya kiviwanda ya bangi
  • Badilisha siku za kazi hadi Jumatatu hadi Alhamisi.
  • Huduma ya afya ya bure na msaada kwa wazee, walio hatarini na wajawazito

David Mwaure Waihiga

Chama cha Agano

  • David Mwaure anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Agano.
  • Ni kiongozi wa Chama cha Agano.
  • Alihitimu na shahada ya sheria kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi na ana Shahada ya Uzamili katika masomo ya uongozi.
  • Yeye ni wakili mkuu na amehudumu kama mwanasheria kwa zaidi ya miongo mitatu.
  • Ana kampuni ya uwakili na amewania viti mbalimbali vya kisiasa.
  • Ilianzishwa chama cha Agano mwaka 2006.
  • Kupambana na ufisadi uliokithiri.
  • kuunda nafasi za ajira.
  • Kurejesha mali ya Kenya iliyofichwa nje ya nchi.

Pata maelezo zaidi kuhusu sera za wagombea urais hapa

Baadhi ya Vituo wanawake walionekana kubeba watoto wao wachanga ili kushiriki katika shughuli hiyo.

Katika Kituo cha Kibra jijini Nairobi , Mwandishi wa BBC Mercy Juma alisambaza picha ya mwanamke ambaye alikuwa amepanga foleni na mtoto wake wa miaka miwili kutoka saa kumi alfajiri saa za kenya, licha ya baridi kali ya asubuhi katika mji mkuu, Nairobi.

Alipoulizwa ni kwanini alikuwa amebeba mtoto wake mgongoni alijibu kwa kusema kwamba hakuwa na mtu wa kumwachia mtoto nyumbani.

Akina mama wajawazito na walio na watoto, wazee na walemavu kwa kawaida hupewa kipaumbele wakati wa kupiga kura.

Kwengineko Wapiga kura katika kituo kimoja cha kupigia kura katika mji mkuu, Nairobi, walijawa na ghadhabu baada ya shughuli ya kupiga kura kukosa kuanza kwa wakati.

Baadhi ya wapiga kura walionya kuzua vurugu iwapo shughuli ya upigaji kura haitaanza. Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wetu Dickens Olewe ulibani kwamba nyenzo za uchaguzi zilichelewa kufika na upangaji ulikuwa ukiendelea.

Raia aliyepiga kura
Maelezo ya picha, Raia aliyepiga kura

Wagombea wakuu wapiga kura

Wakati huohuo baadhi ya viongozi wakiwemo wagombea wakuu wa uchaguzi huo Raila Odinga , William Ruto , Waihige Mwaura walitekeleza wajibu wao wa kupiga kura mapema leo.

Naibu rais William Ruto ambaye anagombea wadhfa wa urais kwa tiketi cha ya chama UDA alikuwa wa kwanza kupiga kura.

Ruto aliyeambatana na mkewe Rachael Ruto walikuwa wa kwanza kushiriki katika uchaguzi huo baada ya kupiga kura nyumbani kwake eneo la Sugoi lililopo jimbo la Bonde la Ufa.

'Tatizo kwa kawaida huja wakati, si wakati watu wanapiga kura, lakini wakati watu wanakataa matokeo ya uchaguzi.

Nadhani kwa mara ya kwanza katika historia ya demokrasia ya vyama vingi nchini Kenya, wagombea wote wamejitolea kwamba watakubali matokeo ya kura

Kwa hivyo nadhani hii itakuwa tofauti na itakuwa ya amani, na ndani ya muda mfupi iwezekanavyo. Tunapaswa kuleta nchi pamoja na kutekeleza ajenda ambayo watu wa Kenya watakuwa wamechagua."

Ruto akipiga kura
Maelezo ya picha, Naibu ya rais Wilkiam Ruto akipiga Kura

Wa pili Kushiriki katika zoezi hilo alikuwa mgombea mwenza wa Raila Odinga Martha Karua ambaye muda mchache tu baada ya Ruto kushiriki katika shughuli hiyo ya Kihistoria, alipiga kura katika eneo bunge la Gichugu , huko Kirinyaga.

Akizungumza muda mfupi baadaye Karua alisema kuwa Wakenya wana nafasi ya kubainisha mwelekeo ambao nchi itafuata.

Martha alitoa wito kwa raia kujitokeza kutekeleza haki yao ya kikatiba.

Naye mgombea mwenza wa William Ruto, Rigathi Gachagua pia naye alipata fursa ya kushiriki katika shughuli hiyo ya kikatiba alipopiga kura katika eneo bunge la Mathira.

Rigathi ambaye alipata mkosi katika kituo cha kupiga kura baada maelezo ya alama zake za vidole kukosekana katika kifaa cha kielektroniki cha kupigia Kura, KIEMS kabla ya jina lake kuidhinishwa kupitia sajili la daftari la wapiga kura ,alisema kwamba ni wakati muhimu na kutoa wito kwa Wakenya kushiriki kwa wingi katika shughuli hiyo.

Mgombea wa chama cha Azimio Raila Odinga aliyeambatana na mkewe Ida Odinga alipiga kura mwendo wa saa nne huku idadi kubwa ya wafuasi wake wakiwasili naye katika kituo cha kupigia kura cha Kibra.Aliambatana na mkewe Ida Odinga aliyesema-

'Wapiga kura wametekeleza jukumu lao,kilichosalia ni IEBC kuhakikisha inatoa matokeo yanayoelezea matakwa yao halisi'

Ruka X ujumbe
Ruhusu maudhui? (Mitandao ya kijamii)

Mkala hii imebeba madhui yaliyotoka kwenye mitandao ya kijamii. Tunaomba ruhusa yako kabla kitu chochote hakija pakiwa, sababu wanaweza wakawa wanatumia Cookies na tekinolojia nyingine. Unaweza ukasoma sera sera ya kutumia cookies katika mitandao ya kijamii kabla ya kukubali. Kutazama maudhui haya chagua accept and continue

Onyo: Imetoka kwingine na inaweza kuwa na matangazo

Mwisho wa X ujumbe

Naye mgombea wa Urais wa Chama cha Roots Prof. Wajakoya amepata hitilafu za kielektroniki za kifaa cha kupigia kura cha KIEMS katika kituo cha kupigia kura cha Shule ya Msingi ya Indangalasia. Amerejea nyumbani kwake na atapiga kura maafisa wa IEBC watakapotatua suala hilo.

.

Uchaguzi Kenya 2022:Unaweza pia kusoma

.