Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Uchaguzi Kenya 2022:David Mwaure anayegombea urais Kenya ni nani?
- Author, Asha Juma
- Nafasi, BBC Swahili
- Iliyochapishwa
David Mwaure Waihiga ni mmoja wa wa wagombea wa urais katika uchaguzi wa Kenya unaofanyoka agosti tarehe 9 mwaka huu . Baada ya kuhudhuria shule ya msingi na ya upili, alijiunga na Chuo Kikuu cha Nairobi, ambako alisomea sheria.
Mwaure ni kiongozi wa chama cha Agano kilichoanzishwa mwaka 2006.
Anagombea kiti cha urais kwa mara ya pili baada ya kujitolea kuwania nafasi hiyo mwaka wa 2013 lakini baadaye akaghairi azma yake hiyo na kujiondoa kinyang'anyironi.
David Mwaure Waihiga ambaye amejitokeza kuwania viti mbalimbali vya uchaguzi katika chaguzi zilizopita ni wakili mwandamizi na amehudumu kama wakili kwa muda mrefu akiwa na uzoefu wa zaidi ya miaka 35 baada ya kumaliza shahada yake ya Sheria mwaka wa 1981 katika Chuo Kikuu cha Nairobi.
Mwaure pia ana shahada ya uzamili katika uongozi na kwa sasa anasomea Shahada ya Uzamivu katika fani hiyo hiyo.
Bwana Mwaure, sio mgeni katika ulingo wa siasa kwasababu hapo awali aliwania viti tofauti vya uchaguzi katika ngazi ya eneo bunge na kaunti.
Baadhi ya mapendekezo katika manifesto yake
Chama cha Agano kimebandikwa jina la ''Mabadiliko'', yaani Change kwa Kiingereza, huku manifesto ya chama hicho ikitoa (ahadi) 12.
Nazo ni: Agano kwa katiba, Familia, Wanawake, Vijana, Watu Wanaoishi na Ulemavu, Serikali za Kaunti, Wafanyakazi, Wamiliki wa Biashara, Uchumi, Taasisi za Kidini, Mazingira, pamoja na Agano kwa Jumuiya ya Kimataifa.
Iwapo yeye na mgombea mwenza wake, Ruth Mutua, wataingia mamlakani mnamo Agosti, David Mwaure ameahidi kuongeza mgao wa mapato kwa kaunti hadi 40%, na kuteua 10% ya 40% kwenda moja kwa moja kwa mabaraza ya miji
Bw. Mwaure ananuia kuunda jopo kazi kuchunguza uwezekano wa kuvunjwa kwa Kaunti ya Nairobi baada ya uchaguzi huu ili baada ya 2027, gavana wa Nairobi awe anateuliwa na rais baada ya uchaguzi na mjumbe wa moja kwa moja wa baraza la mawaziri.
Katika mpango wake kwa wafanyakazi wa Kenya, ameahidi msamaha wa jumla wa 50% ya PAYE(Kodi ya mapato), pamoja na mazingira mazuri kwa sekta ya kibinafsi, watu binafsi na wengine kuanzisha biashara kwa nia ya kukuza ujasiriamali.
Hali mbaya ya kiuchumi pia iko kwenye manifesto yake, na mpango wa kuhamisha shirika la urejeshaji mali kwa afisi ya rais,kupeleka bajeti kwa mabaraza ya miji tofauti na ofisi ya hazina au bajeti ya Ikulu, na kutafuta wale vigogo waliohusishwa na sakata za rushwa na kuhakikisha wanafuatiliwa kwa mujibu wa sheria.
Wakili huyo ameapa kukabiliana na ufisadi.
"Sisi Agano tunasema ni wakati wa mabadiliko, tunasema ni wakati wa Kenya kuwa na uongozi mpya, tunasema pia Kenya haitakwenda popote tukiwachagua viongozi walewale waliokuwepo miaka nenda, miaka rudi. Ni wakati wa kumaliza laana na vitendo vya ufisadi na kashfa," anasema Mwaure.
Aidha, amesema iwapo atachaguliwa serikali yake italenga kurejesha mali zote zilizoibwa zilizofichwa nje ya nchi na ndani, kushughulikia mdororo wa kiuchumi unaoikabili nchi na kuwa sauti ya wasio na uwezo.
Mwaure pia anakusudia kuunda mfumo wa kisheria utakaohakikisha kuwa ripoti za ukaguzi wa hesabu za sekta ya umma ni ushahidi wa kimsingi katika matumizi mabaya ya ofisi na matumizi mabaya ya fedha.
"Tutahakikisha Ksh. trilioni 15 zilizoibwa na kufichwa nje ya nchi zinarejeshwa Kenya kwa mashauriano na nchi zote husika zilipo fedha hizi," ameahidi Bw Mwaure.
Serikali yake pia ina nia ya kuweka kikomo katika jumla ya malipo ya mkopo kutoka kwa serikali hadi Ksh.1 trilioni.
"Hii itatoa Ksh.350B mara moja kusaidia miradi ya serikali.
Tutaitisha kwa dharura mkutano na wakopeshaji wetu ili kufikia mpango mpya wa ulipaji ili kuhakikisha nchi haiingii katika dhiki ya madeni," alisema Mwaure.