Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Mzozo wa Israel na Palestina: Marekani, Palestina kurejesha uhusiano uliovunjika wakati wa utawala wa Trump?
Marekani itatafuta kujenga tena uhusiano wake na Wapalestina kwa kufungua ubalozi wake huko Jerusalem na kutoa msaada kusaidia kuijenga tena Gaza, Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo Antony Blinken anasema.
Baada ya kukutana na Rais Mahmoud Abbas, Bwana Blinken alisisitiza hitaji la kusimamia makubaliano ya amani ambayo yalimaliza mzozo kati ya Israeli na Hamas.
Lakini aliapa kuhakikisha kuwa kundi la wanamgambo linalotawala Gaza halifaidi.
Pia aliihakikishia Israeli juu ya "kujitolea kwa Marekani" kwa usalama wake.
Takribani watu 242 waliuawa huko Gaza na watu 13 waliuawa nchini Israel wakati wa siku 11 za mapigano makali yaliyomalizika Ijumaa na makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyosimamiwa na Wamisri.
Vurugu hizo zilikuja baada ya wiki kadhaa za mvutano wa Israel na Wapalestina katika Jerusalem Mashariki iliyokaliwa ambayo ilimalizika kwa mapigano kwenye eneo takatifu linaloheshimiwa na Waislamu na Wayahudi.
Hamas ilianza kufyatua roketi nchini Israel baada ya kuionya iondoke kwenye eneo hilo, na kusababisha mashambulio ya kulipiza kisasi kutoka Israel dhidi ya maeneo ya Gaza.
Marekani yaahidi mamilioni ya dola kuijenga upya Gaza
Bwana Blinken alisafiri kwenda Ramallah, Ukingo wa Magharibi, Jumanne alasiri kufanya mazungumzo na Rais wa Mamlaka ya Palestina Mahmoud Abbas.
"Niko hapa kusisitiza kujitolea kwa Marekani kujenga uhusiano na Mamlaka ya Palestina na watu wa Palestina, uhusiano uliojengwa kwa kuheshimiana na pia imani ya pamoja kwamba Wapalestina na Waisraeli sawa wanastahili uhuru, usalama, fursa, na hadhi sawa, "aliuambia mkutano wa pamoja wa wanahabari.
Wapalestina walikata mawasiliano na utawala wa Rais wa zamani wa Marekani Donald Trump na kukataa mpango wake wa amani wa Mashariki ya Kati wakidai kuwa uliupendelea Israel.
Alipochukua madaraka, Rais Joe Biden aliahidi kurudisha misaada kwa Wapalestina ambayo ilikatwa na mtangulizi wake na kufungua tena ujumbe wa kidiplomasia alioufunga.
Bwana Blinken alitangaza Jumanne kwamba Marekani itatafuta "kushirikiana na kutoa msaada kwa" watu wa Palestina kwa kusonga mbele na mchakato wa kufungua ubalozi wake huko Jerusalem.
Ubalozi huo ulishughulikia masuala ya Palestina hadi mwaka 2019, wakati ulipounganishwa na ubalozi mpya kwa Israel ambao serikali ya Trump iliufungua katika mazingira ya utata huko Jerusalem mwaka uliotangulia. Kuunganisha kuliashiria kupungua kwa nguvu kwa ujumbe wa kidiplomasia wa Marekani kwa Wapalestina.
Afisa mwandamizi wa Palestina aliliambia shirika la habari la AFP kwamba majadiliano yanafanyika kuhusu kufungua tena ofisi ya Chama cha Ukombozi wa Palestina (PLO) huko Washington DC, ambayo ilifungwa na utawala wa Trump.
Blinken pia alisema Marekani inafanya kazi na jamii ya kimataifa, Mamlaka ya Palestina na Israel kusaidia katika jitahada za kurejesha hali ya ahueni huko Gaza, na kuongeza: "Tunapaswa kujibu hitaji kubwa la kusaidia watu katika wakati huu."
Alisema utawala wa Biden utatoa dola milioni 5.5m , msaada wa haraka wa majanga kwa Gaza na dola milioni 32 kwa ombi la dharura la shirika la wakimbizi wa Palestina (Unrwa) la Umoja wa Mataifa.
Pia imeiarifu Congress kuhusu nia yake ya kutoa dola milioni 75 katika maendeleo ya ziada na msaada wa kiuchumi kwa Wapalestina mwaka 2021.
Lakini Bw Blinken alisisitiza kuwa Washington itahakikisha kwamba Hamas, inayodhibiti Gaza, haifaidiki. Hamas imeorodheshwa kama kikundi cha kigaidi na Marekani, EU, Uingereza na Israel.
Wakati huo huo, Bw Netanyahu aliishukuru Washington kwa "kuunga mkono kikamilifu haki ya Israel ya kujilinda" wakati mapambano yalipopamba moto.
"Sisi pia, tutamaanisha kujitolea kwetu kwa kujilinda: ikiwa Hamas itavunja utulivu na kushambulia Israel, majibu yetu yatakuwa ya nguvu sana," Waziri Mkuu alionya.
Alisema pia alikuwa amezungumza na Bwana Blinken kurejesha mfumo wa ulinzi wa makombora ya Iron Dome ambao unalinda Israel dhidi ya mashambulizi ya roketi ya Wapalestina, na pia njia za kuzuia Hamas kujipanga upya.
Blinken alisema diplomasia kali, ya nyuma ya pazia na Rais Biden ilisaidia usitishaji vita wiki iliyopita, na kwamba "sasa tunaamini lazima tuijenge zaidi".
Umoja wa Mataifa ulisema Jumapili kuwa Wapalestina 242, wakiwemo watoto 66 na wanawake 38, waliuawa katika mzozo huo, na kwamba ofisi yake ya haki za binadamu imehakikisha kuwa takribani watu 129 kati yao walikuwa raia.
Uliongeza kuwa karibu vifo 230 vya Wapalestina vilionekana kusababishwa na vikosi vya Israel, na kwamba majeruhi wengine huko Gaza huenda walitokana na kuanguka kwa roketi
Vikosi vya Ulinzi vya Israel vilisema viliwaua zaidi ya wanamgambo 200 wakati wa mapigano. Hamas na Islamic Jihad hawajatoa takwimu za jumla za majeruhi kwa wapiganaji wao.
Nchini Israel, watu 13, wakiwemo watoto wawili na raia watatu wa kigeni, waliuawa na roketi ya Palestina au moto mwingine, au wakati wa kukimbia makazi wakati wa mashambulio ya roketi, huduma za kitabibu zimeeleza.
UN ilitaja wizara ya makazi ya Palestina ikisema majengo 258, yakijumuisha nyumba 1,042 za makazi na biashara, ziliharibiwa wakati wa mapigano. Kwa kuongezea, maeneo ya nyumba 769 yaliharibiwa vibaya na nyumba 14,536 zilipata uharibifu mdogo.
Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa , vituo vya elimu hamsini na nne, hospitali sita na vituo 11 vya huduma za afya viliharibiwa, kama vile maji, usafi wa mazingira, na miundombinu ya umeme.
Maafisa wa Palestina huweka gharama za ujenzi upya kwa makumi ya mamilioni ya dola.
Serikali ya Israel bado haijachapisha makadirio yake ya uharibifu, lakini majengo na magari mengi nchini Israel yameharibiwa na moto wa roketi.