Mlipuko Beirut: Maandamano ya kupinga serikali yashuhudiwa Lebanon

Chanzo cha picha, Reuters
Waandamanaji katika mji wa Beirut walikabiliana na vikosi vya usalama vya Lebanon wakipinga serikali siku ya Alhamisi.
Maafisa wa usalama walirusha vitoza machozi kwa kundi la waandamanaji waliokuwa karibu na bunge.
Waandamanaji hao walikasirishwa na mlipuko uliotokea Jumanne, ambapo maafisa wanasema ulisababishwa na tani 2,750 za kemikali ya ammonium nitrate ambazo zimekuwa zikihifadhiwa kwa njia isiyo sahihi tangu mwaka 2013.
Raia wengi wa Lebanon wanasema upuuzaji wa serikali ndio chanzo cha mlipuko huo, uliosababisha vifo vya watu karibu 137 na kujeruhi wengine 5,000.
Mlipuko huo uliharibu eneo zima la mji huo huku nyumba na biashara zikiharibiwa kabisa.
Watu kadhaa bado hawajulikani walipo.

Chanzo cha picha, Reuters

Chanzo cha picha, Reuters
Shirika la habari linalomilikiwa na serikali limesema kwamba watu 16 wametiwa mbaroni kama sehemu ya uchunguzi uliotangazwa na serikali wiki hii.
Tangu kutokea kwa mkasa huo maafisa wawili wamejiuzulu.
Mbunge Marwan Hamadeh alijiuzulu Jumatano, huku balozi wa Lebanon nchini Jordan, Tracy Chamoun akijiuzulu Alhamisi, na kusema kwamba janga hilo limeonesha haja ya mabadiliko katika uongozi.
Mapema Alhamisi, Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron pia alitembelea mji huo na kusema Lebanon inahitaji mabadiliko ya kina katika ngazi ya mamlaka.
Pia alitoa wito wa kufanyika kwa uchunguzi wa kimataifa kuhusu janga hilo.













