Moja kwa moja, Mazungumzo ya Marekani na Iran kuanza Uswisi

Jumamosi jioni, Makamu wa Rais wa Marekani, JD Vance, aliondoka Washington kuelekea Uswisi kwa ajili ya mazungumzo hayo

Muhtasari

Skip Video and continue reading
  • xx
  • xx
  • d
  • s
  • a
  • Sonko
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • Dangote
  • xx
  • Lydia Wanjiku

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Dunia yasherehekea Siku ya Baba huku mjadala wa malezi ukiongezeka

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Dunia leo inaungana kuadhimisha Siku ya Baba, siku maalum inayotambua na kuenzi mchango wa baba katika malezi ya watoto, ustawi wa familia na maendeleo ya jamii kwa ujumla.

    Maadhimisho haya, yanayofanyika kila Jumapili ya tatu ya mwezi Juni, yamekuwa fursa muhimu ya kuonyesha shukrani kwa baba, kutafakari nafasi yao katika maisha ya watoto, pamoja na kujadili changamoto mbalimbali zinazowakabili katika kutimiza majukumu yao ya kifamilia na kijamii.

    Wengi hutumia siku hii kuwatakia heri baba zao, kuwapatia zawadi au kutumia muda pamoja nao kama njia ya kuonyesha shukrani kwa mchango wao.

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Katika baadhi ya familia, siku hii pia hutumika kuwakumbuka kina baba waliofariki dunia au wale ambao wamekuwa na mchango mkubwa katika maisha ya watoto wao licha ya changamoto mbalimbali.

    Hata hivyo, baadhi ya baba wanakabiliwa na changamoto za kiuchumi, majukumu ya kazi na mabadiliko ya kijamii yanayoathiri uwezo wao wa kutumia muda wa kutosha na familia zao.

    Maadhimisho ya Siku ya Baba mwaka huu yanakuja wakati ambapo mijadala kuhusu usawa wa majukumu ya malezi kati ya wazazi inaendelea kushika kasi katika sehemu mbalimbali duniani.

    Kwa wengi, siku hii si tu ya kusherehekea, bali pia ya kutafakari namna ya kuimarisha mahusiano ya kifamilia na kuhakikisha watoto wanapata malezi bora kutoka kwa wazazi wote wawili.

    Pia unaweza kusoma:

  2. Shambulio la Israel chanzo cha kifo cha mwanaharakati wa uhifadhi Lebanon

    .

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Mwanaharakati wa mazingira wa Lebanon, Mona Khalil, ambaye kazi yake ilisaidia kubadilisha sehemu ya pwani ya kusini mwa Lebanon kuwa moja ya maeneo muhimu zaidi ya mashariki ya Bahari ya Mediterania kwa viota vya kasa wa baharini walio hatarini kutoweka, amefariki baada ya kujeruhiwa katika shambulio la Israel.

    Khalil, mwenye umri wa miaka 76, alijeruhiwa wakati nyumba yake iliyopo ufukweni mwa Mansouri, karibu na mji wa kusini wa Tyre, iliposhambuliwa wakati wa mashambulizi ya Israel kusini mwa Lebanon wiki mbili zilizopita.

    Alifariki siku ya Ijumaa baada ya kukaa hospitalini kwa siku kadhaa, kulingana na shirika moja la mazingira la eneo hilo.

    Kifo chake kilitokea wakati mashambulizi ya anga ya Israel yalipoongezeka kusini mwa Lebanon, hali inayozua wasiwasi kuhusu uwezekano wa kuongezeka tena kwa ghasia licha ya juhudi za kidiplomasia za kudumisha amani tete ya kikanda.

    BBC imewasiliana na jeshi la Israel kwa ajili ya maoni.

    Soma zaidi:

  3. Ziara hii haimaanishi kuanza kwa awamu ya pili ya mazungumzo - Iran

    .
    Maelezo ya picha, Msemaji wa Iran Esmail Baghaei

    Shirika la habari la Iran IRNA linaripoti kuwa ujumbe wa Iran uliowasili Uswisi umepangwa kufuatilia “jinsi ya kutekeleza ahadi zilizomo katika makubaliano ya maelewano kati ya Iran na Marekani.”

    Kabla ya ujumbe huo kuondoka Iran, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Ismail Baghaei, alisisitiza kuwa ziara hii haimaanishi kuanza kwa awamu ya pili ya mazungumzo ya kufikia makubaliano ya mwisho, bali lengo lake kuu ni “kudai utekelezaji wa ahadi za upande wa pili.”

    “Uelewa au makubaliano yoyote hupimwa katika hatua ya utekelezaji, na kwa kuzingatia uzoefu wa upande wa pili katika kuvunja ahadi zake, lazima tuwe thabiti na makini sana katika kudai haki zetu katika hatua ya utekelezaji,” Baghaei alisema.

    Soma zaidi:

  4. Mashambulizi ya Israel yawaua watu sita Gaza, akiwemo mpiga picha wa Al Jazeera

    .

    Chanzo cha picha, Saeed M. M. T. Jaras/Anadolu via Getty Images

    Mashambulizi ya Israel huko Gaza yameua takriban watu sita, akiwemo mpiga picha wa Al Jazeera na mtoto mmoja, kwa mujibu wa maafisa wa afya na waokoaji.

    Al Jazeera ilisema “inalaani vikali uhalifu huu wa kikatili wa kulenga na kumuua” mwandishi wake Ahmed Wishah, ambaye aliuawa katika shambulio la bomu lililolenga nyumba moja katikati ya Gaza siku ya Jumamosi.

    Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) lilidai kuwa Wishah alikuwa “gaidi katika kitengo cha kijeshi cha Hamas ambaye alihudumu kama mpiga risasi wa kuvizia”.

    Wizara ya Afya ya Gaza inayoendeshwa na Hamas, ambayo takwimu zake zinachukuliwa kuwa za kuaminika na Umoja wa Mataifa, inasema jeshi la Israel limeua watu 1,007 tangu makubaliano ya kusitisha mapigano kati ya Israel na Hamas yalipoanza Oktoba iliyopita.

    Al Jazeera ilisema kifo cha Wishah siku ya Jumamosi “kinawakilisha ukiukaji mpya na mkubwa wa sheria zote za kimataifa na kanuni, na kinaonyesha sera inayoendelea ya kuwanyima sauti waandishi wa habari na kunyamazisha ukweli”.

    IDF ilisema Wishah katika miezi ya hivi karibuni alikuwa akipanga mashambulizi ya kuvizia dhidi ya wanajeshi wa Israel, bila kutoa ushahidi.

    Watu wengine wawili waliuawa pamoja na Wishah katika shambulio hilo lililolenga nyumba katika kambi ya wakimbizi ya Bureij, kwa mujibu wa hospitali ya eneo hilo na shirika la ulinzi wa kiraia linaloendeshwa na Hamas, ambalo hufanya kazi za uokoaji.

    IDF pia ilidai kuwa wawili hao waliouawa walikuwa sehemu ya Hamas.

    Ndugu yake Wishah, Mohamed, ambaye pia alikuwa mwandishi wa Al Jazeera, aliuawa katika shambulio la Israel mwezi Aprili. IDF ilidai kuwa alishirikiana na Hamas katika makao makuu ya uzalishaji wa makombora na silaha ya kundi hilo, bila kutoa maelezo zaidi.

    Soma zaidi:

  5. Kombe la Dunia 2026: Curaçao waweka historia, wapata sare ya kwanza dhidi ya Ecuador

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Timu ya taifa ya Curacao walipata pointi yao ya kwanza kabisa katika Kombe la Dunia baada ya uchezaji wa kuvutia kutoka kwa kipa Eloy Room aliyefanikisha kuizuia timu ya taifa ya Ecuador iliyopoteza nafasi nyingi.

    Kipa wa Miami FC, Room, aliweka rekodi kwa kuokoa jumla ya mipira 15, akizuia mashambulizi ya Wamarekani Kusini katika Kundi E.

    Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 37 alionyesha kiwango cha juu sana cha uchezaji, akilingana na rekodi ya kipa wa Marekani Tim Howard ya kuokoa mara nyingi zaidi katika mechi ya Kombe la Dunia.

    Howard aliokoa mara 15 dhidi ya timu ya taifa ya Ubelgiji mnamo mwaka 2014 katika mechi iliyokwenda hadi muda wa ziada (na pia kuruhusu mabao mawili katika kipigo cha 2-1) — lakini Room aliwezesha timu ya kocha Dick Advocaat kupata sare ya kihistoria.

    Alianza kuokoa baada ya dakika tatu tu, na wengi wanasema kuwa ndiye aliyekuwa mchezaji bora zaidi wa usiku huo, na kumfuatilia kwa karibu mchezaji Enner Valencia aliyemzuia kufunga kwa karibu kabisa na lango.

    Baada ya hapo, John Yeboah naye alinyimwa nafasi ya kufunga, kabla ya Room kuokoa tena shuti la Valencia katika jumla ya mara sita za kuokoa katika kipindi cha kwanza.

    Kipindi cha pili kilikuwa na kasi zaidi baada ya mapumziko, huku kipa Room akifanya kazi ya ziada ya kuokoa mipira ya hatari iliolenga lango ya Moisés Caicedo, Pedro Vite, Kevin Rodríguez, Nilson Angulo, Gonzalo Plata na wachezaji wengine.

    Curaçao nao walipata nafasi nzuri sana karibu na dakika ya 60, lakini shuti la Leandro Bacuna lilizuiliwa, kabla ya Liviana Comenencia naye kujaribu bahati yake na mpira kuokolewa.

    Ecuador watajilaumu kwa kupoteza nafasi zao za wazi za kufunga, baada ya kupiga mashuti 27 kwa jumla bila mafanikio.

    Sasa wanapaswa kuishinda Ujerumani, ambao ni vinara wa kundi, katika mchezo wao wa mwisho ili kujihakikishia nafasi ya kusonga mbele kwenye hatua ya mtoano, baada ya kuanza vibaya kwa kupoteza dhidi ya Ivory Coast kwenye mchezo wao wa ufunguzi.

    Kwa upande mwingine, Curacao—ambao walichapwa mabao 7-1 na Ujerumani kwenye mchezo wao wa kwanza—bado wana nafasi ya kusonga mbele hadi hatua ya 32 bora iwapo wataifunga Ivory Coast katika mechi yao ya mwisho ya hatua ya makundi.

    Soma zaidi:

  6. Mazungumzo ya Marekani na Iran kuanza Uswisi huku Tehran ikidai kufunga Mlango-Bahari wa Hormuz

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Mazungumzo ya Marekani na Iran kuanza Uswisi huku Tehran ikidai kufunga Mlango-Bahari wa Hormuz

    Mazungumzo ya moja kwa moja kati ya Marekani na Iran yanatarajiwa kuanza nchini Uswisi licha ya jeshi la Iran kusema kuwa limefunga tena Mlango-Bahari wa Hormuz kufuatia mashambulizi ya Israel kusini mwa Lebanon.

    Jeshi la Marekani limepinga madai hayo, likisema kuwa "usafiri wa meli unaendelea kama kawaida". Iran ilisema kuwa Mlango-Bahari wa Hormuz ulifungwa kujibu mashambulizi mabaya ya Israel nchini Lebanon, ambayo Tehran ilisema yalikiuka makubaliano yake na Marekani ya kumaliza vita.

    Jumamosi jioni, Makamu wa Rais wa Marekani, JD Vance, aliondoka Washington kuelekea Uswisi kwa ajili ya mazungumzo hayo.

    Ujumbe wa Iran unaojumuisha Spika wa Bunge, Mohammad Bagher Ghalibaf, na Waziri wa Mambo ya Nje, Abbas Araghchi, tayari umewasili.

    Duru mpya ya mazungumzo inatarajiwa kuanza Jumapili. Vance alisema ana matumaini ya kupiga hatua “kuhusu suala la nyuklia” na pia “suala la usitishaji mapigano nchini Lebanon”.

    Akizungumza na waandishi wa habari kabla ya kupanda ndege yake, aliulizwa kuhusu mapigano kati ya Israel na Hezbollah pamoja na mashambulizi ya anga ya Israel kusini mwa Lebanon.

    "Hali kwa kweli inaendelea kuimarika zaidi huko, na mambo yanaanza kutulia kidogo," Vance alisema.

    "Hili ni jambo ambalo tutalazimika kuendelea kulisimamia ili kuhakikisha kwamba Israel na Lebanon zote mbili ziko salama na zenye usalama. Hilo ndilo lengo kuu — kufanya eneo lote liwe salama na utulivu," Vance aliongeza.

    Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmail Baghaei, alisema kuwa nchi yake itakuwa "ikisisitiza upande mwingine kutimiza ahadi zake."

    Soma zaidi:

  7. Hujambo na karibu katika matangazo yetu Mubashara.