Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Virusi vya Corona: Hatimaye Trump avaa barakoa
Rais wa Marekani Donald Trump amevaa barakoa kwa mara ya kwanza hadharani tangu lilipoanza janga la virusi vya corona.`
Rais huyo amevaa barakoa alipotembelea hospitali ya kijeshi ya Walter Reed iliyopo nje ya jiji la Washington, ambako alikutana na wanajeshi waliojeruhiwa na wahudumu wa afya.
"Sijawahi kamwe kupinga uvaaji wa barakoa, lakini ninaamini kuwa zina mahali na muda wake," alisema alipokuwa akiondoka katika ikulu ya White House.
Awali alisema kuwa hawezi kuvaa barakoa na akamkejeli hasimu wake wa chama cha Democrat Joe Biden kwa kufanya hivyo.
Lakini Jumamosi alisema kuwa : "Ninafikiri pale unapokua hospitali, hasa katika hali fulani, ambapo unaongea na wanajeshi na watu, ambao wakati fulani wametoka kwenye meza za upasuaji, nafikiri ni kitu kizuri kuvaa barakoa ."
Akizungumza na kituo cha habari za biashara cha - Fox Business Network wiki iliyopita Bwana Trump alisema : "Ninaunga mkono barakoa."
Aliongeza kuwa "ni kama ninapenda " anavyofanana akiwa ameivaa, akijifananisha na aliyovaa Lone Ranger, shujaa wa kufikirika ambaye pamoja na rafiki yake mzawa wa Marekani, Toronto, walipigana na wahalifu katika Marekani ya zamani ya Magharibi.
Lakini wakati vituo vya Marekani vya udhibiti wa magonjwa (CDC) mwezi Aprili vilipopendekeza kuwa watu wavae barakoa au vitambaa vinavyofunika midomo na pua wawapo katika maeneo ya umma ili kusaidia kuzuwia kusambaa kwa virusi, Bwana Trump aliwaambia waandishi wa habari kuwa hatafuata agizo hilo.
"Sidhani nitakua nikifanya hilo" alisema wakati huo. " Kuvaa barakoa huku nikiwasalimia marais, mawaziri wakuu, madikteta, wafalme na mamalkia -sioni hili likifanyika."
Baadhi ya taarifa za vyombo vya habari zimesema kuwa washirika wake wamekua wakimuomba mara kwa mara rais Trump avae barakoa awapo hadharani.
Hali iko vipi kwa sasa Marekani?
Marekani imeshuhudia maambukizi mapya ya watu 66,528 katika kipindi cha saa 24 zilizopita, rekodi ya siku moja, na jumla ya takriban vifo 135,000 tangu janga la virusi vya corona lilipoanza, kulingana na data za Chuo Kikuu cha Johns Hopkins.
Louisiana ni jimbo la hivi karibuni lililoagiza watu wavae barakoa katika maeneo ya umma.
Gavana kutoka chama cha Democratic John Bel Edwards pia ameagiza kufungwa kwa baa kote Louisiana, na kuweka sheria kalio kuhusu uendeshwaji wa migahawa ya chakula, ambayo haitaweza kuwahudumia wateja ndani yake. Hatua hizozitaanza kutekelezwa kuanzia Jumatatu.
Wabunge wa Republican wanatarajiwa kupinga hatua hiyo.
"Kama hupendi kuvaa barakoa, basi haupendi unapoivaa," Gavana Edwards alisema. "Kama unataka kunikasirikia kuihusu, basi nikasirikie."
Jimbo jirani la Texas limerekodi ongezeko jingine la maambukizi ya virusi vya corona , likirekodi watu 10,500 wapya wenye maambukizi vya virusi hivyo Jumamosi pekee.
Gavana wa jimbo la South Carolina ametoa amri ya marufuku ya mauzo ya pombe baada ya saa tano za usiku katika baa na migahawa ya chakula kujaribu kuzuwia kusambaa kwa virusi.
Mahakama katika jimbo la Indiana imesitisha hukumu ya vifo dhidi ya wafungwa waliopatikana na hatia ya mauaji kwasababu jamaa zao walisema kuwa wana wasiwasi wa kusafiri wakati huu wa janga kushuhudia ndugu zao wakifa.
Daniel Lee alikua amepangiwa kuuawa Jumatatu katika tukio ambalo lingekua ni la kwanza la hukumu ya mauaji baada ya miaka 17.