Tulsi Gabbard : Nini kinachofahamika kuhusu Mkurugenzi mpya wa Ujasusi wa Marekani mwenye utata?

Iliyochapishwa
Muda wa kusoma: Dakika 7

Bunge la seneti nchini Marekani lilimuidhinisha aliyekuwa mbunge Tulsi Gabbard, ambaye aliilaumu Marekani na NATO kwa kuanzisha vita vya Ukraine na kukutana na kiongozi aliyeondolewa madarakani wa Syria, Bashar al-Assad, kuwa Mkurugenzi wa Ujasusi wa Kitaifa.

Tulichunguza uteuzi wake una maana gani kwa sera za kigeni za Marekani.

Nafasi yenye ushawishi mkubwa

Mkurugenzi wa Ujasusi wa Kitaifa ni kiongozi rasmi wa jamii ya ujasusi ya Marekani, ambayo inajumuisha mashirika 18 tofauti, ikiwa ni pamoja na CIA, FBI, na mashirika ya ujasusi ya Idara ya Ulinzi.

Mkurugenzi anaratibu majukumu miongoni mwao, lakini hawaripoti moja kwa moja kwake. Ni ofisi yake inayokusanya kile kinachoitwa "Muhtasari wa Kila Siku wa Rais," muhtasari wa siri wa ujasusi unaowekwa mezani kwa rais kila asubuhi.

Nafasi hii ilianzishwa baada ya mashambulizi ya kigaidi ya Septemba 11, 2001, ambapo kukosekana kwa uratibu na ushirikiano wa taarifa kati ya mashirika ya ujasusi kulitajwa kama moja ya sababu za mashambulizi kutoshughulikiwa.

"Mojawapo ya majukumu makuu ya idara za ujasusi ni kulinda vyanzo vyao, na kabla ya ofisi ya Mkurugenzi wa Ujasusi wa Kitaifa kuanzishwa, walikuwa wakikawia kushirikiana taarifa kwa hofu ya kufichua vyanzo vyao," alisema Ian Kelly, mtaalamu wa zamani wa diplomasia wa Marekani ambaye alifanya kazi kama msemaji wa Idara ya Jimbo na balozi wa Georgia, akizungumza na BBC Russian Service.

Jukumu lingine muhimu la ofisi hii ni kushirikiana kijasusis na washirika. Kelly alisema kuwa kuratibu juhudi za ujasusi za Marekani na kufuatilia taarifa ambazo washirika wa Marekani wanapokea kunafanya nafasi hii kuwa na ushawishi mkubwa.

Na anaamini kuwa Tulsi Gabbard hafai kwa nafasi hiyo, kwa sababu ya kukosa uzoefu wa ujasusi na kwa sababu ya historia yake ya matamshi ya utata.

"Mara nyingi alionekana kama anakariri propaganda ya Kremlin kuhusu Ukraine," alisema mtaalamu huyo wa zamani wa diplomasia, akiongeza kuwa uteuzi wa Gabbard unaweza kuathiri imani na ushirikiano wa ujasusi kati ya Marekani na washirika wake.

Mtaalamu wa masuala ya kijeshi John Foreman, ambaye alihudumu kama mjumbe wa kijeshi wa Uingereza huko Moscow, anaafiki "Washirika [wa Marekani] watakuwa na wasiwasi kwamba taarifa wanazotoa zinaweza kuangukia mikononi mwa maadui wao," alisema kwa BBC Russian Service.

"Uhusiano wake na Assad, kurudia hoja za Putin, na makosa yake yanamfanya kuwa hafai kabisa kwa moja ya nafasi nyeti zaidi katika serikali ya Marekani."

Gabbard amekosolewa kwa kurudia propaganda ya Kirusi kwa matamshi yake yenye utata kuhusu vita vya Urusi na Ukraine. Alisema wasiwasi kuhusu maabara ya biolojia ya Marekani nchini Ukraine baada ya taarifa hii kuenezwa na wahusika wa kidiplomasia wa Urusi na vyombo vya habari, na siku ya kwanza ya uvamizi wa kijeshi, alisema vita hivi vingeweza kuzuiwa kama serikali ya Biden na NATO wange "kukubali tu wasiwasi halali wa Urusi kuhusu Ukraine kujiunga na NATO."

Kwa matamshi haya, alijumuishwa kwenye orodha ya wazungumzaji "wanaoendeleza simulizi zinazolingana na propaganda ya Kirusi," iliyotungwa na Kituo cha Kupambana na Upotoshaji chini ya Baraza la Usalama na Ulinzi la Ukraine. Orodha hiyo iliondolewa baadaye, lakini nakala ya kumbukumbu bado inapatikana mtandaoni.

Madai ya uhusiano na Bashar al-Assad yanahusiana na safari ya siri aliyofanya Gabbard kwenda Damascus mnamo Januari 2017 bila idhini ya serikali ya Marekani. Nchini Syria, alikaribishwa mara mbili na Assad na kukutana na mkewe, waziri wa mambo ya nje, na balozi wake katika Umoja wa Mataifa, kulingana na ratiba ya safari iliyotolewa baada ya kurejea kwake.

Gabbard pia alikosoa hitimisho la upelelezi wa Marekani kwamba jeshi la Syria lilitumia silaha za kemikali, na alijaribu kuonyesha upinzani wote wa Syria kama wanamgambo walioungana na ISIS au Al-Qaeda (ambao wameorodheshwa kama mashirika ya kigaidi na kupigwa marufuku katika nchi nyingi, ikiwemo Urusi), wakati CIA ikitoa msaada mdogo kwa vikundi vya upinzani.

Katika kikao mbele ya Kamati ya Upelelezi ya Seneti mwezi Januari mwaka huu, Gabbard alisema hakuwahi kumwabudu Assad na alikuwa amemuuliza "maswali magumu kuhusu matendo ya utawala wake." Alipozuiliwa kwa kuonekana kurudia propaganda ya Kirusi, alijibu kwamba hakufuata vyombo vya habari vya serikali ya Urusi na alijitolea kusema ukweli.

Shelby Magid, mkurugenzi msaidizi wa Kituo cha Eurasia cha Baraza la Atlantiki (kilichotambuliwa kama shirika lisilotakikana katika Shirikisho la Urusi), anasema ni makosa kusema kwamba mitazamo ya Gabbard isiyo ya kawaida ingeweza kuathiri sera za kigeni za Marekani.

"Ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Kitaifa haijui sera za kigeni; nguvu hiyo iko kwa Rais Trump. Tunatarajia watoa maamuzi wote kufuata mwelekeo wake," alisema Magid kwa BBC Russian.

Kutoka kuwa nyota wa Chama cha Democratic hadi mshirika wa Trump

Kabla ya kuteuliwa kwake kuwa Mkurugenzi wa Upelelezi wa Kitaifa (DNI), Gabbard alijulikana hasa kama mkosoaji wa sera za kigeni za Marekani, sifa aliyojipatia katika miaka yake nane ya utumishi katika Bunge.

Msimamo wake wa ukosoaji ulikuwa matokeo ya kuwa mwanajeshi wa jeshi wa Jeshi la ziada la Marekani. Alihudumu kwa hiari katika Jeshi wakati wa "vita dhidi ya ugaidi" vilivyotangazwa baada ya mashambulizi ya 9/11, alifikia cheo cha Luteni Kanali katika upelelezi, na alipokea Medali ya Heshima.

Kufanya kazi nchini Iraq na Kuwait imemfanya Gabbard kuwa mkosoaji wa ushiriki wa Marekani katika migogoro ya Mashariki ya Kati. Alipokuwa akichaguliwa kwa mara ya kwanza kuwa mbunge mwaka 2012, hiyo haikuwa msimamo wa utata ndani ya Chama cha Kidemokrasia, ambacho Rais Barack Obama aliongoza kwa lengo la kupunguza ushiriki wa Marekani katika vita.

Nancy Pelosi alimtaja Gabbard kama nyota inayoibuka kati ya Wademocrat, na katika mwaka wake wa kwanza bungeni alikua makamu mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya chama. Lakini Gabbard na viongozi wakuu wa chama walipishana hivi karibuni.

Wakati wa kampeni za 2016, mbunge huyo alijiuzulu kama makamu mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Democrats kwa sababu ilionyesha uamuzi wa kutokuwa na upande—na Gabbard alitaka Bernie Sanders, si Hillary Clinton, kuwa mgombea urais.

"Tunapaswa kumaliza sera za kuingilia kati na mabadiliko ya utawala ambazo zimegharimu sana," Gabbard alielezea uamuzi wake.

Hali halisi ni kwamba Hillary Clinton alitetea ushiriki wa Marekani katika vita vya wenyewe nchini Syria. Alipendekeza kuanzisha eneo la ulinzi wa anga nchini Syria ili kulinda raia kutokana na mashambulizi ya anga kutoka kwa ndege za Urusi na utawala wa Assad.

Lakini wakosoaji waliona hiyo kama tishio la kuibua mgogoro kati ya Urusi na Marekani na inaweza kuwa tu kisingizio cha operesheni ya kubadilisha utawala. Hatua kama hiyo nchini Libya mwaka 2011 ilielezewa kama kulinda raia, lakini ilimalizika kwa uingiliaji wa kijeshi unaoongozwa na NATO, wakosoaji walisema.

Clinton, ambaye kinyume na matarajio yote, alishindwa na Donald Trump, alikua mgombea wa Democrats. Lakini, alipojitenga na chama chake, Gabbard pia aliwakosoa Republican.

Mnamo Aprili 2017, Donald Trump aliamuru shambulizi la makombora kwenye kituo cha anga cha Syria kama hatua ya kujibu shambulizi la kemikali kwenye mji wa Khan Sheikhoun.

Mbunge huyo wa Hawaii aliiita hatua hiyo kuwa ni kuongezeka kwa mivutano ambayo ingeweza kuimarisha magaidi na kupelekea vita vya kinyuklia kati ya Marekani na Urusi.

Pia aliandika muswada uitwao "Hatutaki Vita vya Rais Tena." Muswada huo ulisema kwamba "Trump ameonyesha nia yake ya kutumia jeshi la Marekani dhidi ya Syria, Urusi, na Iran," na kupendekeza kuzuia rais kutumia jeshi bila kibali cha bunge. Muswada huo ulishindwa kupitishwa na kamati husika.

Mnamo 2020, aliacha azma yake ya kugombea tena nafasi ya Ubunge ili kuzingatia uchaguzi wa urais wa Democrats, lakini alijiondoa haraka kutoka kwenye kinyang'anyiro hicho. Akiwa hana kazi huko Washington, Gabbard alianzisha podikasti na kuwa mgeni wa mara kwa mara katika vipindi vya televisheni vya kihafidhina.

Ukosoaji wake kwa Democrats ulizidi kuwa mkali; aliondoka rasmi kwenye chama hicho mwaka 2022. Mwishowe, mwaka jana, alijiunga na upande wa Republican na kumtangaza Trump kama mgombea wake wa urais.

Utafiti wa maoni umeonyesha uchaguzi wa 2024 kuwa ulitabirika kidogo zaidi katika miongo kadhaa, ukiwaonyesha Trump na Kamala Harris, ambaye kwa ghafla alichukua nafasi ya Joe Biden kama mgombea wa urais wa Democrats, wakiwa na tofauti ndogo sana ya asilimia.

Katika hali hii, pande zote mbili za kampeni zilijaribu kuvutia watu maarufu. Hatimaye, Harris na Democtrat walikuwa wakifadhiliwa na wawakilishi wa moja ya familia maarufu za Republican: aliyekuwa Makamu wa Rais Dick Cheney, anayeonekana kama mbunifu wa Vita vya Iraq, na binti yake Liz Cheney, ambaye alipoteza kiti chake cha Ubunge baada ya kumkosoa Trump.

Cheney baadaye alipokea medali kutoka kwa Biden na aliongezwa kwenye orodha ya watu waliopata msamaha wa kinga dhidi ya kushtakiwa.

Trump aliwateua Gabbard na Robert Kennedy Jr., mfuasi mwingine aliyehama chama cha democrats kwa kuwapa nyadhifa katika utawala wake.

Wadadisi wa siasa nchini Marekani wanasema uteuzi huu ni jaribio la Trump kujumuisha wapiga kura wote, ikiwa ni pamoja na baadhi ya Wanachama wa zamani wa Democrats.