Tetesi za Soka Ulaya Alhamisi 16.05.2024

Iliyochapishwa

Manchester United wanataka kumsajili mshambuliaji wa Uingereza Ollie Watkins kutoka Aston Villa kwani mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 28 analingana na wasifu wa mchezaji ambaye wanataka kumsajili. (Talksport)

Arsenal wanafikiria kuwasilisha dau la pauni milioni 60 kumnunua mshambuliaji wa RB Leipzig wa Slovenia Benjamin Sesko, 20. (Telegraph - usajili unahitajika)

Mshambulizi wa Liverpool na timu ya taifa ya Misri, Mohamed Salah,31 na kipa wa Brazil Alisson Becker, 31, ni miongoni mwa wachezaji wanaosakwa na klabu za Saudi Pro League msimu huu. (Guardian)

Nafasi ya Erik ten Hag kubaki kocha wa Manchester United inalegalega, huku mustakabali wa Mholanzi huyo mwenye umri wa miaka 54 ikitarajiwa kuamuliwa baada ya fainali ya Kombe la FA mnamo Mei 25. (Guardian)

Thomas Tuchel, ambaye yuko kwenye orodha fupi ya Manchester United ya wachezaji wanaotarajiwa kuchukua nafasi ya Ten Hag, yuko kwenye mazungumzo ya kusalia Bayern Munich, baada ya kupangwa kuondoka mwishoni mwa msimu huu. (Times - usajili unahitajika)

Chelsea wameandaa ofa mpya kwa winga wa Palmeiras Willian Estevao baada ya kuafikiana na mchezaji huyo wa kimataifa wa Brazil mwenye umri wa miaka 17 wiki iliyopita. (Fabrizio Romano)

Licha ya kufuzu kwa Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya Aston Villa italazimika kuuza angalau mchezaji mmoja kwa ada kubwa msimu huu wa joto ili kuzingatia Kanuni za Faida na Uendelevu za Ligi Kuu. (Sun)

Kocha wa zamani wa Chelsea, Manchester United na Tottenham Jose Mourinho ananyatiwa na klabu ya Al-Qadsiah ya Saudi Arabia. (Mail)

Chelsea watapata nyongeza ya pauni milioni 5 chini ya masharti ya uhamisho wa Eden Hazard kwenda Real Madrid 2019 baada ya timu hiyo ya Uhispania kutinga fainali ya Ligi ya Mabingwa - licha ya mshambuliaji huyo wa zamani wa Ubelgiji mwenye umri wa miaka 33 kustaafu miezi saba iliyopita. (Telegraph - usajili unahitajika)

Imetafsiriwa na Ambia Hiris