Matetemeko 10 ya ardhi mabaya zaidi kuwahi kutikisa dunia

    • Author, Mariam Mjahid
  • Iliyochapishwa
  • Muda wa kusoma: Dakika 4

Jioni ya Jumatano, Venezuela ilikumbwa na matetemeko mawili makubwa yaliyotokea kwa mfululizo, yakisababisha uharibifu mkubwa, kubomoka kwa majengo na kuwalazimu wakazi wengi kukimbilia mitaani kwa hofu.

Timu za uokoaji ziliendelea na shughuli za kutafuta manusura siku iliyofuata katika maeneo yaliyoathiriwa zaidi na matetemeko hayo yenye ukubwa wa alama 7.2 na 7.5, ambayo yaliua watu wasiopungua 164, kujeruhi karibu watu 1,000 na kuwaacha wengi wakiwa wamenaswa chini ya vifusi vya majengo yaliyoanguka.

Matetemeko hayo ni miongoni mwa yaliyo na nguvu zaidi kuwahi kuikumba Venezuela katika kipindi cha zaidi ya karne moja. Mitikisiko yake ilihisiwa katika sehemu mbalimbali za ukanda huo.

Zaidi ya watu milioni 2.5 wamepoteza maisha yao katika matetemeko kumi mabaya zaidi kuwahi kurekodiwa katika historia ya binadamu.

Matetemeko ya ardhi tisa kati ya kumi mabaya zaidi katika historia yalitokea barani Asia.

China ndiyo nchi iliyopoteza watu wengi zaidi, ambapo takriban watu milioni 1.3 walifariki dunia katika matetemeko matatu tofauti, kulingana na takwimu za Taasisi ya Jiolojia ya Marekani.

Ya mwisho ndio matetemeko ya ardhi mabaya kuwahi kushuhudiwa na binadamu.

10. Kamchatka, Urusi, 2025

Tetemeko la ardhi la alama 8.8 lililoikumba Kamchatka mwaka 2025 ni miongoni mwa matetemeko sita makubwa zaidi kuwahi kurekodiwa duniani.

Lilitanguliwa na mitikisiko kadhaa mikubwa, ikiwemo tetemeko la alama 7.4 lililotokea siku kumi kabla.

Matetemeko haya yanaonyesha nguvu kubwa za asili ambazo, kwa muda mfupi, zinaweza kubadili historia ya mataifa, kuangamiza miji na kuathiri maisha ya mamilioni ya watu duniani.

9. Tetemeko Kuu la Chile, 1960

Tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa alama 9.5 lililikumba eneo la kati la Chile mwaka 1960. Linalojulikana kama Tetemeko Kuu la Chile, ndilo kubwa zaidi kuwahi kurekodiwa duniani.

Zaidi ya watu 1,600 walifariki nchini Chile na maeneo mengine, huku wengi wao wakipoteza maisha kutokana na mawimbi makubwa ya tsunami yaliyosababishwa na tetemeko hilo. Watu karibu milioni mbili walibaki bila makazi.

8. Alaska, Marekani, 1964

Tetemeko la ardhi la alama 9.2 liliikumba Alaska na kudumu kwa karibu dakika tano.

Linalojulikana kama Tetemeko Kuu la Alaska au Tetemeko la Ijumaa Kuu, liliua watu zaidi ya 130 na kusababisha hasara iliyokadiriwa kufikia dola bilioni 2.3 za Marekani. Baada ya tetemeko hilo, maelfu ya mitikisiko midogo iliendelea kwa wiki kadhaa.

7. Iran

Matetemeko mawili makubwa yaliyotokea nchini Iran zaidi ya miaka 1,100 iliyopita ni miongoni mwa mabaya zaidi katika historia.

Kwa mujibu wa vyanzo vya simulizi na maandishi ya kihistoria, watu takriban 350,000 walifariki katika matetemeko hayo mawili.

6. Haiti, 2010

Tetemeko la ardhi la alama 7 lililoikumba Haiti Januari 12, 2010 liliua takribani watu 222,000 na kujeruhi zaidi ya watu 300,000.

Watu karibu milioni 1.3 walilazimika kuyahama makazi yao, huku nyumba karibu 100,000 zikiharibiwa.

5. Tōhoku, Japan, 2011

Tetemeko la alama 9.1 lilikumba pwani ya kaskazini mashariki mwa Japan mwaka 2011 na kusababisha tsunami kubwa iliyoikumba mitambo ya nyuklia ya Fukushima.

Tetemeko hilo lilisababisha kukatika kwa umeme na mifumo ya kupoza mitambo, hali iliyosababisha kuyeyuka kwa vinu vitatu vya nyuklia. Zaidi ya watu 18,000 walifariki na wengine zaidi ya 130,000 walilazimika kuhama makazi yao.

4. Sumatra, Indonesia, 2004

Mnamo Desemba 26, 2004, tetemeko la ardhi la ukubwa wa 9.1 lilitokea katika pwani ya Sumatra, Indonesia, na kusababisha tsunami kubwa iliyoharibu maeneo ya Kusini Mashariki mwa Asia, Kusini mwa Asia na Afrika Mashariki.

Zaidi ya watu 230,000 walifariki, wakiwemo zaidi ya 170,000 nchini Indonesia pekee. Takribani watu 50,000 walitoweka na karibu watu milioni 1.7 walilazimika kuyahama makazi yao.

Mawimbi ya tsunami yaliyofikia urefu wa mita 30 na kusafiri kwa kasi ya kilomita 700 kwa saa yalifagia kila kitu kilichokuwa katika njia yake.

3. Tetemeko la Aleppo, Syria, Oktoba 11, 1138

Tetemeko la Aleppo nchini Syria linatambuliwa kuwa la tatu kwa kusababisha vifo vingi zaidi katika historia ya binadamu. Lilitokea Oktoba 11, 1138, katika jimbo la Aleppo kaskazini mwa Syria.

Zaidi ya watu 230,000 walipoteza maisha kutokana na janga hilo. Ingawa ukubwa wa tetemeko hilo haujulikani, simulizi za kihistoria zinaeleza kuwa lilisababisha uharibifu mkubwa, likibomoa majengo, ngome na makazi katika maeneo mengi ya kaskazini mwa Syria.

Tetemeko hilo limesalia kuwa mojawapo ya majanga mabaya zaidi ya asili kuwahi kurekodiwa katika historia ya Mashariki ya Kati.

2. Tetemeko la Tangshan, China, Julai 28, 1976

Tetemeko la Tangshan nchini China ndilo la pili kwa kusababisha vifo vingi zaidi katika historia ya binadamu na ndilo lililosababisha maafa makubwa zaidi katika kipindi cha karne iliyopita.

Tetemeko hilo, lenye ukubwa wa alama 7.8, liliikumba mji wa viwanda wa Tangshan mnamo Julai 28, 1976, na kusababisha vifo vya takribani watu 255,000 huku wengine karibu 800,000 wakijeruhiwa.

Ndani ya takribani sekunde 10 pekee, tetemeko hilo liliharibu karibu majengo 180,000 na kusababisha uharibifu uliosikika hadi mji mkuu wa China, Beijing.

Janga hilo limesalia kuwa moja ya majanga mabaya zaidi ya asili kuwahi kutokea katika historia ya kisasa ya China.

1. Tetemeko la Shaanxi, China, Januari 23, 1556

Tetemeko la Shaanxi linatambuliwa kuwa tetemeko la ardhi lililosababisha vifo vingi zaidi katika historia ya binadamu. Lilitokea Januari 23, 1556, katika jimbo la Shaanxi, kaskazini magharibi mwa China, ambalo wakati huo lilijulikana kama Shensi.

Inaaminika kuwa tetemeko hilo lilikuwa na ukubwa wa alama 8 na lilisababisha vifo vya takribani watu 830,000.

Tetemeko hilo liliharibu eneo la takribani kilomita 840, huku karibu asilimia 60 ya wakazi wa eneo hilo wakipoteza maisha. Uharibifu wake mkubwa umeendelea kulifanya kuwa mojawapo ya majanga mabaya zaidi ya asili kuwahi kurekodiwa duniani.