Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Ukraine: Urusi inapanga vita vikubwa Ulaya tangu 1945- Boris Johnson
Ushahidi unaonesha kuwa Urusi inapanga "vita kubwa zaidi barani Ulaya tangu 1945," Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson amesema.
Alimwambia mwandishi wa BBC Sophie Raworth katika mahojiano: "Ishara zote ni kwamba mpango huo tayari kwa maana fulani umeanza."
Ujasusi unapendekeza kwamba Urusi inakusudia kufanya uvamizi ambao utauzingira mji mkuu wa Ukraine Kyiv, Bw Johnson alisema.
"Watu wanapaswa kuelewa gharama kubwa katika maisha ya binadamu ambayo inaweza kutokea," alisema.
Waziri mkuu alikuwa akizungumza kutoka Munich, ambapo viongozi wa dunia wanakutana kwa mkutano wa kila mwaka wa usalama.
Makadirio ya hivi punde ya serikali ya Marekani yanaonesha kuwa kati ya wanajeshi 169,000 na 190,000 wa Urusi sasa wako kwenye mpaka wa Ukraine, nchini Urusi na nchi jirani ya Belarus - lakini idadi hii pia inajumuisha waasi mashariki mwa Ukraine.
Bw Johnson pia alionyesha kwamba Uingereza italeta vikwazo vikubwa zaidi dhidi ya Urusi kuliko ilivyopendekezwa hapo awali.
Alisema Uingereza na Marekani zitazuia makampuni ya Kirusi "kufanya biashara ya pauni na dola" - hatua ambayo alisema "itapiga sana" na athari zake.
Vikwazo vya awali vilivyopendekezwa na mawaziri ni pamoja na kupanua wigo wa watu wa Urusi na biashara ambazo Uingereza inaweza kulenga.
Maafisa wa nchi za Magharibi wameonya katika wiki za hivi karibuni kwamba Urusi inaweza kujiandaa kuivamia wakati wowote, lakini Urusi imekanusha madai hayo, ikisema wanajeshi wanafanya mazoezi ya kijeshi katika eneo hilo.
Alipoulizwa ikiwa uvamizi wa Urusi bado unafikiriwa kuwa karibu, Bw Johnson alisema: "Ninaogopa kwamba ndivyo ushahidi unavyoelekeza...
"Ukweli ni kwamba dalili zote ni kwamba mpango huo tayari kwa maana fulani umeanza."
Waziri Mkuu alisema Rais wa Marekani Joe Biden aliwaambia viongozi wa nchi za kijasusi wa nchi za Magharibi kwamba vikosi vya Urusi havikuwa vinapanga tu kuingia Ukraine kutoka mashariki, kupitia Donbas, lakini kutoka Belarus na eneo linaloizunguka Kyiv.
"Ninaogopa kusema kwamba mpango tunaouona ni wa kitu ambacho kinaweza kuwa vita vikubwa kabisa barani Ulaya tangu 1945 kwa kiwango kikubwa," waziri mkuu alisema.
Watu walihitaji sio tu kuzingatia uwezekano wa kupoteza maisha ya Waukrani , lakini pia ya "Warusi vijana", aliongeza.
Bw Johnson alikuwa akizungumza baada ya kukutana na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky na kuwaambia viongozi wa dunia katika hotuba yake kwamba uvamizi wowote wa Ukraine unaofanywa na Urusi "utalaaniwa kote ulimwenguni".