Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Soko lingine kubwa Tanzania laungua
Rais Samia Suluhu ametuma salamu za pole kwa wafanyabiashara wote wa soko la mitumba la Karume jijini Dar-es-salaam nchini Tanzania ambalo limeungua usiku wa kuamkia leo na kusababisha asilimia 98 ya mali zote za eneo hilo kuteketea.
Taarifa zinasema hakuna madhara kwa wananchi yaliyotokea mbali na hasara ya mali zilizopotea.
Aidha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Amos Makalla amewataka wafanyabiasha wa soko la Karume kuwa watulivu huku akiahidi kuundwa kamati itakayochunguza kujua chanzo cha moto huo.
"Chanzo cha moto huo katika soko la Karume au mchikichini bado hakijulikani huku kukiwa na makisio ya hitilafu ya umeme, soko hilo limeungua kwa takribani asilimia 98 licha ya jitihada za kuudhibiti," Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam ameeleza.
Imeelezwa kuwa moto huo ulioteketeza sehemu kubwa ya soko hilo lenye wafanyabiashara zaidi ya 3,500 ulianza usiku wa kuamkia leo huku Jeshi la zimamoto na uokoaji likijitahidi kuuzima lakini uliteketeza soko hilo sehemu kubwa.
"Tutaaunda kamati itakayoongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Ilala kuchunguza kwa siku 14 kisha tutapokea majibu na kujua cha kufanya na wakati wote wa uchunguzi hakuna mfanyabiashara atakayeruhusiwa kuendelea na biashara katika eneo hili tutaangalia utaratibu mwingine,"amesema bwana Makalla.
Kwa mujibu wa gazeti la Mwananchi kamanda wa Jeshi la Zimamoto na uokoaji Wilaya ya Ilala, Elisa Mugisha amesema;
"Na kwa bahati nzuri wakati huo tulikuwa tunatoka Mabibo ambako nako kuna nyumba ilikuwa inaungua moto na tulifika hapa ndani ya muda mfupi tulifika eneo la tukio lakini moto ulikuwa mkali kutokana na asili ya bidhaa wanazouza hapa mbao, maturubahi na nguo ambazo vinasambaza moto kwa haraka tulijitahidi kuzunguka soko na kuanza kuzima."
"Tunachoshukuru Mungu hakuna madhara kwa binadamu na wala moto haukuvuka kwenda kwenye nyumba za wananchi kwa sababu tulikuwa na gari nne ," aliongeza mkuu wa zima moto.
Mnamo mwezi Julai, Soko la Kariakoo liliungua huku chanzo cha Moto kikiwa hakijafahamika.
Tathmini zilionesha kuwa maduka zaidi ya 220 yalitekeketea kwa moto katika soko la Kariakoo lililopo jijini Dar es salaam.
Na serikali iliagiza masoko yote na vituo vya mabasi kuwa na huduma za zima Moto ili kupunguza changamoto zinazotokea majanga kama hayo.