Mbwana Samatta ajiunga na klabu ya Fenerbahce ya Uturuki

Iliyochapishwa
Muda wa kusoma: Dakika 1

Mshambuliaji wa timu ya soka nchini Tanzania Mbwana Samatta amejiunga na klabu ya Uturuki Fenerbahce kwa mkataba wa miaka minne kutoka Aston Villa.

Klabu hiyo imeandika katika mtandao wake kwamba imemuongeza nahodha wa timu ya taifa ya Tanzania katika kikosi chake kwa mkataba wa miaka minne.

Klabu hiyo imemkaribisha mchezaji huyo.

Mchezaji huyo aliyeshinda taji la mfungaji bora mara kadhaa nchini Ubelgiji kabla ya kujiunga na Aston Villa nchini Uingereza atahudumu katika klabu hiyo kwa mkopo wa mwaka mmoja kabla ya kuandikisha kandarasi ya kudumu ya miaka minne.

Ripoti kutoka Istanbul zinasema kwamba mshambuiaji huyo atavalia jezi nambari 12 mgongoni katika klabu yake mpya.

Fenerbahce inayoshiriki katika ligi kuu ya Uturuki siku ya Ijumaa ilimzindua Samatta rasmi ikichapisha kanda ya video katika akaunti yake ya Twitter .

Akionesha furaha yake baada ya kuandikisha mkataba huo , Samatta akinukuliwa na mtandao huo amesema: Najua jinsi klabu ya Fenerbahce ilivyo kubwa sio tu hapa Uturuki bali pia duniani kwa jumla. Nafurahia kujiunga na klabu hii kwasababu itakuwa mpya na changamoto kubwa kwangu. Fenerbahce ina mashabiki wengi na wanataka kushinda kila mara. Nimekuja na ombi hili na ninatumai kwamba tutashinda mataji mengi, alisema.

Tutakujuza zaidi.....