Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Makubaliano na Marekani hayatasainiwa Jumapili - Iran
Iran imesema siku ya Jumamosi kwamba inaweza kusaini makubaliano ya amani na Marekani katika siku chache zijazo lakini Reuters inaripoti kwamba haitakuwa Jumapili kama ilivyosemwa Pakistan ambayo ni nchi mpatanishi.
Muhtasari
- Man City, Man Utd na Bayern zamtaka Branthwaite, Arsenal macho kwa Tzolis
- Makubaliano na Marekani hayatasainiwa Jumapili - Iran
- Nchi 22 zaionya Iran kusitisha mashambulizi ya siri ndani na nje ya nchi hiyo
- Wezi wavamia na kuiba vifaa vya mazoezi vya timu ya England
- Makubaliano kati ya Marekani na Iran kuafikiwa katika saa 24 zijazo
- Mazishi ya aliyekuwa kiongozi mkuu wa Iran, kuanza tarehe 4 Julai
- Mashambulizi mapya ya Israel yaripotiwa kusini mwa Lebanon
- Bei ya mafuta yashuka na kufikia viwango vya chini zaidi tangu vita kuanza Iran
- Partey anyimwa viza ya Canada, kukosa mechi ya ufunguzi ya Ghana
- Jeshi la Marekani lamuua kiongozi wa genge la Tren de Aragua nchini Venezuela
- Elon Musk rasmi sasa trilionea wa kwanza duniani
- Marekani yaichapa Paraguay 4-1, kufanya maajabu mwaka huu?
- Marekani yamfukuza mwanaharakati wa Iran na kumpeleka Afrika ya Kati
- Makubaliano ya kumaliza vita na Marekani yako karibu kuafikiwa- Iran
- Jeshi la Marekani ladai kudungua ndege zisizo na rubani za Iran katika Mlango bahari wa Hormuz
Moja kwa moja
Na Beldeen Waliaula
Tetesi mpya za soka: Man City, Man Utd na Bayern zamtaka Branthwaite, Arsenal macho kwa Tzolis
Manchester City, Manchester United na Bayern Munich zinaendelea kumfuatilia beki wa Everton na England, Jarrad Branthwaite, kuelekea dirisha lijalo la usajili. (Daily Mail)
Arsenal wanapanga kufanya mazungumzo ya kumsajili winga wa Club Brugge na Ugiriki, Christos Tzolis, mwenye umri wa miaka 24, katika dili linaloweza kufikia pauni milioni 34.5. Mchezaji huyo ameifungia klabu yake mabao 17 na kutoa pasi za mabao 23 msimu huu. (The Athletic)
Kiungo wa Aston Villa na England, Morgan Rogers, amesema anafahamu tetesi za usajili zinazomhusisha na Arsenal, Chelsea, Paris Saint-Germain na Manchester United, lakini amesisitiza kuwa anabaki na umakini kwenye majukumu yake ya sasa. (Sky Sports)
Manchester United wanafikiria kupeleka ofa ya kumsajili kiungo wa West Ham na Ureno, Mateus Fernandes, mwenye umri wa miaka 21, baada ya klabu hiyo kushuka daraja kutoka Ligi Kuu ya England. Hata hivyo, West Ham wanataka takriban pauni milioni 80, bei ambayo United huenda wakaipuuza. (Sky Sports, Telegraph)
Crystal Palace wako tayari kulingana na dau la Middlesbrough la pauni milioni 20 kwa kiungo Hayden Hackney, licha ya Everton pia kumwania mchezaji huyo. (Daily Mail)
Manchester City imefanya mazungumzo ya awali kuhusu uwezekano wa kumsajili beki wa kulia wa Chelsea na Ufaransa, Malo Gusto, katika harakati za kuimarisha safu yao ya ulinzi. (L’Equipe)
Makubaliano na Marekani hayatasainiwa Jumapili - Iran
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Kigeni wa Iran, Esmail Baghaei, amesema kuwa muda wa kutiwa saini kwa makubaliano kati ya Iran na Marekani bado haujaamuliwa.
“Tutasubiri muda sahihi wa kusainiwa kwa hati hiyo ya makubaliano” alisema Baqei
Alifafanua kuwa kutiwa saini kwa hati hiyo hakutafanyika siku ya Jumapili, lakini akaongezea kuwa kuna uwezekano wa kusainiwa katika siku chache zijazo.
Aidha msemaji huyo alisema wanachukua tahadhari kabla ya kutia Saini mkataba huo kutokana na kutoaminika kwa upande wa pili wa Marekani.
Pia unaweza kusoma:
Nchi 22 zaionya Iran kusitisha mashambulizi ya siri ndani na nje ya nchi hiyo
Nchi ishirini na mbili, zikiwemo Marekani, Uingereza, Ufaransa, Ujerumani na washirika wengine wa Ulaya, zimetoa onyo kali kwa Iran kuitaka kusitisha kile wanachodai ni mashambulizi na vitendo vya uhasama vinavyotekelezwa ndani na nje ya nchi hiyo.
Katika taarifa ya pamoja iliyotolewa hapo jana, nchi hizo ziliishutumu Tehran kwa kuunga mkono na kuratibu mashambulizi yanayolenga wanaharakati wa Iran walioko uhamishoni katika mataifa mengine, waandishi wa habari, pamoja na jamii za Wayahudi katika mataifa ya Magharibi.
Taarifa hiyo ilidai kuwa vyombo vya usalama vya Iran vinatumia makundi ya uhalifu kuwalenga raia wake walioko bara Ulaya, Marekani kaskazini na Australia. Nchi hizo zilisema vitendo hivyo vinahatarisha usalama wa raia wao na vinakiuka mamlaka ya taifa husika.
Miongoni mwa matukio yaliyotajwa katika taarifa hiyo ni mashambulizi dhidi ya vituo vya jamii za Wayahudi katika eneo la Golders Green jijini London. Mashambulizi hayo yanadaiwa kutekelezwa na kundi linalojulikana kama Ashab al-Yamin al-Islamiya Movement, ambalo baadhi ya mataifa ya Magharibi yanadai lina uhusiano na Iran.
Ingawa Iran haijatoa jibu rasmi kuhusu taarifa hiyo ya pamoja, imekuwa ikikanusha mara kwa mara tuhuma za kuhusika katika mashambulizi au njama za siri nje ya mipaka yake.
Hatua ya nchi hizo 22 inakuja wakati ambapo Iran na Marekani zinaripotiwa kuwa karibu kufikia makubaliano ya kusitisha mapigano.
Pia unaweza kusoma:
Wezi wavamia na kuiba vifaa vya mazoezi vya timu ya England
Timu ya taifa ya England imekumbwa na wizi wa baadhi ya vifaa vyake vya mazoezi kabla ya kuwasili Kansas City siku ya Jumamosi kwa ajili ya Kombe la Dunia 2026.
Chama cha Soka cha England (FA) kinaendelea kufuatilia ni vifaa gani hasa vimeibwa, huku mipira na viatu vya soka vikitajwa kuwa miongoni mwa vitu vinavyohofiwa kutoweka. Tukio hilo lilitokea baada ya magari yaliyokuwa yakisafirisha vifaa kuelekea kituo cha mazoezi cha Swope Soccer Village kuvunjwa.
Kocha Thomas Tuchel na kikosi chake wanatarajiwa kuwasili Kansas City Jumamosi mchana, huku vifaa hivyo vikitarajiwa kuwa tayari kabla ya kuwasili kwao.
Polisi wa Kansas City, wanaoshirikiana na FA katika uchunguzi huo, walifika eneo la tukio Ijumaa usiku. Inaelezwa kuwa watu wawili tayari wamekamatwa kuhusiana na tukio hilo.
Msemaji wa polisi wa Kansas City amesema uchunguzi unaendelea kuhusu uwezekano wa kuibwa kwa vifaa kutoka kwenye gari la timu ambalo liliwasili jijini humo huku baadhi ya vifaa vikitoweka.
Tukio hilo linaweza kuathiri maandalizi ya England kuelekea mchezo wao wa kwanza wa Kombe la Dunia dhidi ya Croatia utakaochezwa Jumatano. Wachezaji wa England wanatarajiwa kufanya mazoezi yao ya kwanza kamili siku ya Jumapili.
Makubaliano kati ya Marekani na Iran kuafikiwa katika saa 24 zijazo
Waziri mkuu wa Pakistan, ambao ndiyo wapatanishi wakuu wa Marekani na Iran, amesema makubaliano ya kusitisha vita kati ya Marekani na Iran yatakuwa tayari chini ya saa ishirini na nne zijazo.
Kupitia mtandao wa X, Waziri mkuu wa Pakistan, Shahbaz Sharif amesema “Makubaliano ya kusitisha vita yako karibu kuafikiwa, hatua ya mwisho inatarajiwa kuchukuliwa katika saa 24 zijazo”
Kiongozi huyo amesema Pakistan inajiandaa katika hafla ya kutia Saini, na baada ya hapo mazungumzo ya kitaalamu yataendelea.
Kiongozi huyo wa Pakistan aliongezea kuwa “tuna Imani kuwa makubaliano haya ya kihistoria yatakuwa msingi wa amani ya kudumu”
Aidha aliishukuru Marekani na Iran kwa kujitolea kwao katika mazungumzo hayo, pamoja na mataifa ya kanda hiyo kuwaunga mkono.
Pia unaweza kusoma:
Mazishi ya aliyekuwa kiongozi mkuu wa Iran, kuanza tarehe 4 Julai
Mazishi ya aliyekuwa kiongozi mkuu wa Iran Ali Ayatollah Khamenei itaanza tarehe 4 mwezi Julai hadi tarehe 9 mwezi Julai ambapo atazikwa Kaskazini Mashariki mwa mji wa Mashhad.
Khamenei aliuawa katika shambulio lililotekelezwa na Israel na Marekani mwezi Februari, na kumaliza utawala wake wa Zaidi ya miongo mitatu kama kiongozi mkuu wa Iran.
Mwanawe Mojtaba Khamenei ndiye kiongozi mkuu wa Iran kwa sasa.
Pia unaweza kusoma:
Mashambulizi mapya ya Israel yaripotiwa kusini mwa Lebanon
Vyombo vya habari nchini Lebanon vimeripoti mashambulizi ya Israel kusini mwa taifa hilo.
Mashambulizi hayo yametokea baada ya jeshi la Israel kutoa ilani ya watu kuondoka katika zaidi ya maeneo 20 kusini mwa Lebanon, ikiwemo mji wa Nabatieh.
Hapo jana, kundi la Hezbollah lilitangaza kuwa vikosi vyake vilipigana na wanajeshi wa Israel waliokuwa wakielekea mji wa mpakani kusini mwa Lebanon.
Mapigano kati ya jeshi la Israel na Hezbollah yanaendelea, huku Iran na Marekani zikitangaza kuwa ziko karibu kutia saini makubaliano ya kumaliza vita.
Pia unaweza kusoma:
Bei ya mafuta yashuka na kufikia viwango vya chini zaidi tangu vita kuanza Iran
Bei ya mafuta imeshuka na kufikia kiwango cha chini zaidi takriban miezi minne tangu vita vya Iran kuanza.
Kushuka kwa bei hiyo kunatokana na Imani ya wanabiashara kuwa makubaliano ya kumaliza vita kati ya Iran na Marekani yako karibu kuafikiwa.
Bei ya mafuta aina ya Brent imeshuka hadi dola 87.33 kwa pipa moja , ikiwa ni punguzo la dola 3.05 ikiwa kiwango cha chini sana tangu mapema mwezi Machi vita vilipoanza.
Kwa upande wa Marekani, mafuta yameshuka kwa dola 2.83 hadi dola 84.88 kwa pipa moja, ikiwa ni bei ya chini zaidi ya mafuta hayo tangu mwezi Aprili.
Taarifa za kuashiria kuwa huenda Marekani na Iran wakakubaliana hivi karibuni imeleta afueni katika soko la nishati duniani.
Pia unaweza kusoma:
Partey anyimwa viza ya Canada, kukosa mechi ya ufunguzi ya Ghana
Kiungo wa Ghana, Thomas Partey, atakosa mechi ya ufunguzi ya Kombe la Dunia dhidi ya Panama baada ya kunyimwa kibali cha kuingia nchini Canada. Kwa mujibu wa taarifa, maombi yake ya viza yalikataliwa na serikali ya Canada.
FIFA imethibitisha kuwa mchezaji huyo wa zamani wa Arsenal, ambaye kwa sasa anachezea Villarreal, hakuweza kusafiri kutoka kituo cha mazoezi cha Ghana kilichopo Boston kwenda Marekani kutokana na kukosa kibali cha kuingia nchini humo. Shirikisho hilo limesema linaheshimu taratibu za uhamiaji za nchi mwenyeji.
Partey anakabiliwa na kesi ya kujibu mashtaka ya ubakaji na unyanyasaji wa kingono, lakini bado hajahukumiwa na amekana mashtaka yote. Hali hiyo imekuwa moja ya sababu zilizoathiri uamuzi wa viza yake.
Serikali ya Canada imesema kila ombi la kuingia nchini linachunguzwa kwa kina kulingana na sheria za uhamiaji na usalama, na kwamba kuwa mwenyeji wa Kombe la Dunia hakubadilishi sheria hizo.
Kocha wa Ghana, Carlos Queiroz, amesema hana mashaka na uteuzi wa mchezaji huyo, akisisitiza kuwa uamuzi wake wa kumjumuisha kikosini ni wa kiufundi na haoni haja ya kuingia kwenye mjadala wa kimaadili kwa sasa.
Ghana inatarajiwa kuendelea na mechi zake za Kundi L bila Partey, huku uwezekano wa mchezaji huyo kurejea baadaye kwenye mashindano ukibaki wazi endapo timu yake itasonga mbele.
Pia unaweza kusoma:
Jeshi la Marekani lamuua kiongozi wa genge la Tren de Aragua nchini Venezuela
Niño Guerrero, ambaye jina lake kamili ni Héctor Rusthenford Guerrero Flores, alikuwa kiongozi wa muda mrefu wa Tren de Aragua. Genge hilo ni moja ya makundi hatari Marekani Kusini na imekuwa ikilengwa na utawala wa Trump.
Rais Trump amelituhumu genge hilo kwa kushiriki katika “vita visivyo vya kawaida” dhidi ya Marekani na kulitangaza kuwa kundi la kigaidi.
Rais Trump alichapisha picha za video za shambulio hilo la angani, zikionyesha jengo la kijani na kibanda kilichokuwa karibu kikilipuliwa.
Trump aliongezea kuwa operesheni hiyo ya kijeshi ilifanikishwa na “marafiki wetu nchini Venezuela, ambao tunafanya kazi nao vizuri sana”.
Mamlaka za Venezuela zimethibitisha kushiriki kwao katika kile walichokiita “operesheni ya pamoja”.
Mwezi Januari, vikosi vya Marekani vilimkamata Rais wa wakati huo wa Venezuela Nicolás Maduro na kumfungulia mashtaka mjini New York, hati ya mashtaka ikimtaja Guerrero Flores kama mshirika wake katika kutekeleza uhalifu.
Pia unaweza kusoma:
Elon Musk rasmi sasa trilionea wa kwanza duniani
Elon Musk ameandika historia kwa kuwa mtu wa kwanza duniani kufikisha utajiri wa zaidi ya dola trilioni moja, baada ya hisa za kampuni yake ya SpaceX kupanda kwa kasi katika siku ya kwanza kuorodheshwa kwenye soko la hisa la Nasdaq.
Kwa mujibu wa orodha ya matajiri ya Bloomberg, utajiri wa Musk umefikia dola trilioni 1.11 (sawa na zaidi ya shilingi trilioni 2,800 za Tanzania), jambo lililomfanya kuimarisha nafasi yake kama mtu tajiri zaidi duniani.
Mafanikio hayo yamechochewa na kuorodheshwa kwa SpaceX katika soko la hisa kwa thamani ya dola trilioni 2.2. Hisa za kampuni hiyo zilianza kuuzwa kwa dola 150 na kufikia dola 176.50 katika muda mfupi kutokana na hamasa kubwa ya wawekezaji.
Musk anamiliki asilimia 42 ya SpaceX, huku thamani ya hisa zake katika kampuni hiyo ikikadiriwa kufikia zaidi ya dola bilioni 767. Pia ana hisa Tesla zenye thamani ya mamia ya mabilioni ya dola.
Marekani yaichapa Paraguay 4-1, kufanya maajabu mwaka huu?
Marekani imeanza vyema kampeni yake ya Kombe la Dunia 2026 baada ya kuichapa Paraguay mabao 4-1 mjini Los Angeles na kuongoza Kundi D.
Nyota wa zamani wa Arsenal, Folarin Balogun, alifunga mabao mawili katika ushindi huo mkubwa wa wenyeji wenza wa mashindano hayo.
Katika mchezo mwingine, mwenyeji mwingine Canada ililazimishwa sare ya mabao 1-1 dhidi ya Bosnia-Herzegovina na kujikusanyia alama moja katika mechi yake ya kwanza ya kundi.
Nayo Mexico ilianza kwa ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Afrika Kusini, ikiweka wazi dhamira yake ya kufanya vizuri mbele ya mashabiki wake.
Hadi sasa, mataifa yote matatu yanayoandaa Kombe la Dunia 2026 yamecheza mechi zao za ufunguzi, huku Mexico na Marekani zikianza kwa ushindi na Canada ikipata sare. Zitafanya maajabu mwaka huu?
Marekani yamfukuza mwanaharakati wa Iran na kumpeleka Afrika ya Kati
Mwanasheria wa mwanamke mmoja ambaye mwanaharakati wa demokrasia kutoka Iran amesema kuwa Marekani imemfukuza mteja wake na kumpeleka katika taifa la Central Africa Republic (CAR), na kusema ni hatua inayohatarisha maisha ya mteja wake.
Kwa mujibu wa wakili huyo aliyezungumza na Reuters, Maisha mwanaharakati huyo yapo hatarini kutokana na vurugu na ukosefu wa amani ambao unashuhudia katika taifa hilo la Afrika ya Kati.
Taasisi ya Iranian American Legal Defense Fund iliripoti kuwa wanawake watatu wa Iran waliokimbia nchi yao walikuwa katika hatari ya kufukuzwa kutoka Marekani.
Pia unaweza kusoma:
Abbas Araqchi: Makubaliano ya kumaliza vita na Marekani yako karibu kuafikiwa
Waziri wa Mambo ya Kigeni wa Iran, Abbas Araqchi, amesema kuwa makubaliano ya kumaliza vita kati ya Iran na Marekani yako katika hatua za mwisho, na kwamba Mlango bahari wa Hormuz utafunguliwa tena kama sehemu ya makubaliano hayo.
Kwa mujibu wa BBC Persian, Araqchi alisema katika mahojiano ya televisheni kuwa “hatujawahi kuwa karibu hivi na makubaliano kama ilivyo sasa,” akiongezea kuwa makubaliano hayo yanaweza kuafikiwa ndani ya siku moja au mbili zijazo.
Waziri huyo pia aliviambia vyombo vya habari nchini Iran kuepuka kutoa taarifa za uvumi ambazo zinaweza kuharibu mchakato huo wa kidiplomasia na kuathiri mazingira ya mazungumzo.
Araqchi alisema kuwa makubaliano hayo yana ukurasa mmoja na nusu hadi mbili tu, lakini yamejadiliwa kwa zaidi ya miezi miwili, ambapo kila kipengele na kila sentensi imepitiwa na kuhaririwa kwa maslahi ya raia wa Iran.
Pia unaweza kusoma:
Jeshi la Marekani ladai kudungua ndege zisizo na rubani za Iran katika Mlango bahari wa Hormuz
Kituo kikuu cha kuendesha oparesheni za kijeshi Marekani (CENTCOM) imedai kuwa vikosi vyake vimeangusha ndege kadhaa zisizo na rubani zilizorushwa na Iran kuelekea Mlango bahari wa Hormuz.
Katika taarifa iliyochapishwa kwenye mtandao wa X, CENTCOM ilisema Iran ilirusha ndege zisizo na rubani kadhaa kwa lengo la kulenga meli za kibiashara zilizokuwa zikisafiri kupitia Mlango bahari wa Hormuz.
Taarifa hiyo iliongeza kuwa, "Vikosi vya Marekani vimedungua ndege hizo zote zisizo na rubani katika saa chache zilizopita, na usafiri wa meli kupitia Mlango wa Hormuz unaendelea bila usumbufu wowote."
Centcom ilisema ndege hizo za Iran zilikuwa tishio kwa usalama wa meli za kibiashara zinazopitia eneo hilo.
Pia unaweza kusoma:
Hujambo na karibu katika matangazo yetu ya moja kwa moja Jumamosi ya leo