Moto wa nyika walazimisha watu 10,000 kuhamishwa Ufaransa

Chanzo cha picha, Reuters
Moto wa nyikani umelazimisha maelfu ya watu kuhamishwa kusini mwa Ufaransa huku nchi hiyo ikikabiliana na athari za wimbi la joto la kiangazi ambalo limeikumba sehemu kubwa ya Ulaya.
Zaidi ya watu 10,000 wameamriwa kuondoka katika miji na vijiji zaidi ya kumi na mbili katika vilima vya Pyrenees huko Ufaransa, karibu na mpaka na Uhispania.
Moto huo, ulioko Trévillach karibu na Perpignan, umeteketeza hekta 4,600 (ekari 11,366), mkuu wa mkoa Pierre Regnault de la Mothe alisema katika chapisho kwenye X.
"Asubuhi ya leo hali inazidi kuwa mbaya tena," Waziri wa Mambo ya Ndani Laurent Nunez alionya kwenye kituo cha televisheni cha Ufaransa TF1. "Leo vita vinaendelea tena."
Mamlaka zimeonya kwamba upepo mkali unachochea moto zaidi.
Rais wa Tume ya Ulaya Ursula von der Leyen alitangaza kwamba EU itatuma ndege nne zilizoko Kupro na Sweden kusaidia katika juhudi za dharura.
Moto huo pia umeathiri nchi jirani ya Uhispania ambapo zaidi ya hekta 2,200 katika hifadhi ya asili ya Les Gavarres zimeharibiwa.
Kusini mwa Catalonia, katika jimbo la mashariki la Castellon, watu 500 walihamishwa baada ya moto wa porini kuingia katika mbuga ya kitaifa ya Sierra de Espadan.
Halijoto inaweza kufikia tena nyuzi joto 40C kusini-magharibi mwa Ufaransa wiki hii na tayari imezidi nyuzi joto 40C katika sehemu za Ureno na Uhispania.
Wakati wa wimbi la joto lililovunja rekodi la Juni, halijoto ya nyuzi joto 42C katika baadhi ya maeneo, Ufaransa ilishuhudia siku yenye joto kali zaidi kuwahi kutokea kote nchini tarehe 24 Juni.
Angalau vifo 2,025 vilirekodiwa nchini Ufaransa, 1,222 nchini Ubelgiji na takriban 480 nchini Uholanzi wakati wa wimbi la joto.
Mabadiliko ya tabianchi yanaongeza halijoto duniani kote - lakini hasa barani Ulaya. Hii inasababisha kuongezeka joto la kiangazi na moto mkali wa nyikani.
Pia unaeza kusoma:






















![]](https://ichef.bbci.co.uk/ace/ws/640/cpsprodpb/vivo/live/images/2026/7/6/9bcf04d3-52db-451a-a8e2-874315828851.png.webp)










