Watu wanne wa familia moja wakiwemo watoto wawili
wamefariki katika mlipuko wa gesi kusini mwa Italia.
Nyumba yao ya ghorofa mbili katika mji wa Saviano, karibu
na Naples, iliporomoka kwa kiasi fulani katika mlipuko huo, na kuwaua ndugu -
mvulana na msichana - pamoja na mama na bibi yao.
Baba na mtoto mchanga walipatikana kutoka kwenye vifusi
wakiwa hai, wazima moto wa Italia walisema.
Bado yuko hospitalini huko Naples akiwa katika hali
mbaya, wakati majeraha ya mtoto sio ya kutishia maisha, vyombo vya habari vya
ndani viliripoti.
Idara ya zimamoto ya Vigili del Fuoco, Italia, iliripoti
kwamba wazazi na watoto watatu waliishi kwenye ghorofa moja ya nyumba hiyo,
wakati mwanamke mwingine - anayesemekana kuwa bibi - aliishi kwenye ghorofa ya
juu.
"Wazima moto waliwaokoa baba na mtoto mchanga wakiwa
hai, na kuwakabidhi chini ya uangalizi wa wafanyikazi wa afya mahali hapo,
wakati hawakuweza kufanya chochote kwa watoto wawili, mvulana na msichana,
ambao kwa bahati mbaya miili yao ilitolewa wakiwa washafariki dunia," Idara
ya zimamoto ilisema katika taarifa.
Ingawa mamlaka haijathibitisha umri wa watoto hao, vyombo
vya habari vya ndani viliripoti kwamba walikuwa wa miaka minne na sita.
Wazima moto waliwapata watoto na baba asubuhi, kisha ikawachukua
siku nzima kutafuta kwenye vifusi, na hawakumpata mama huyo hadi saa 16:45.
Vikosi vya utafutaji na uokoaji, vinavyofanya kazi na
mbwa wa kunusa, viliendelea na utafutaji wa bibi huyo hadi usiku, na kutangaza
kuwa wamempata na walikuwa wamemaliza shughuli hiyo kufikia saa 01:00.
Uchunguzi
unaendelea kubaini chanzo hasa cha kuporomoka kwa jengo hilo, lakini nadharia
za awali zinaonyesha kuwa nyumba hiyo ilianguka baada ya mlipuko wa gesi.