Gen Z maarufu kwa kauli ya "Mr Speaker Sir" afikishwa mahakamani kwa kesi ya uvamizi wa Bunge
Ezekiel Kyama Nzoki, mwanaharakati wa maandamano ya Gen Z anayefahamika kwa kauli ya "Mr Speaker Sir," alifika mbele ya Hakimu Mkuu Mwandamizi wa Mahakama ya Milimani, Caroline Mugo, Jumatatu, ambapo alikana mashtaka yanayohusiana na maandamano ya kupinga Muswada wa Fedha wa Juni 25, 2024.
Kwa mujibu wa mahakama, Nzoki anakabiliwa na shtaka la kuharibu mali katika Majengo ya Bunge kwa makusudi akiwa pamoja na watu wengine ambao hawajafikishwa mahakamani.
Hati ya mashtaka inaeleza kuwa:
"Ezekiel Kyama Nzyoki, mnamo Juni 25, 2024, katika Majengo ya Bunge ndani ya Kaunti ya Jiji la Nairobi, akiwa pamoja na wengine ambao hawapo mahakamani, aliharibu kwa makusudi na kinyume cha sheria sehemu za jengo, uzio wa eneo la Bunge, mlingoti wa bendera katika Mausoleum, samani, vifaa vya TEHAMA na skrini za televisheni, vifaa vya jikoni, magari na mifumo ya umeme, vyenye thamani ya shilingi 41,248,570, mali ya Tume ya Huduma za Bunge."
Nzoki aliachiliwa kwa dhamana binafsi ya Shilingi 100,000 akisubiri kusikilizwa na kuamuliwa kwa kesi hiyo.
Mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino, alifika mahakamani na kumwakilisha Nzoki wakati wa kesi hiyo.
Nzoki alijulikana sana wakati wa maandamano ya Gen Z baada ya kusambaa kwa video zilizomuonesha akiwa ndani ya ukumbi wa Bunge la Taifa wakati wa uvamizi wa waandamanaji waliokuwa wakipinga Muswada wa Fedha wa 2024.
Unaweza kusoma;