Matokeo ya uchaguzi Kenya 2022: Raila Odinga na William Ruto katika ushindani mkali

Raila na Ruto

Chanzo cha picha, AFP

Maelezo ya picha, Raila na Ruto
Iliyochapishwa

Huku takriban nusu ya matokeo ya uchaguzi wa urais nchini Kenya yakiwa yamethibitishwa, wagombea wawili wakuu wamekabana koo.

Naibu Rais William Ruto amechukua uongozi kidogo dhidi ya aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga - 51% dhidi ya 48%.

Mkuu wa tume ya uchaguzi amekiri kwamba utangazaji wa matokeo ya uchaguzi wa Jumanne unaendelea polepole.

Uhakiki wa matokeo umesitishwa mara kadhaa baada ya malalamiko kutoka kwa wafuasi na wagombea wakuu.

Jumamosi usiku, wafuasi wa Bw Odinga waliingia katika eneo lililozuiliwa na kuwashambulia maafisa wa uchaguzi, wakiwashutumu kwa kuvuruga kura.

Huku kukiwa na ghasia hizo, meneja mkuu wa kampeni za Bw Odinga aliweza kufika kwenye jukwaa lililotumiwa na maafisa wakuu wa tume ya uchaguzi, ambako alikosoa mchakato wa kuhakiki matokeo.

"Nataka kutangaza kwa taifa kwamba Bomas of Kenya ni eneo la uhalifu," alisema Saitabao Ole Kanchory, kabla ya kipaza sauti kuzimwa na kuchukuliwa''.

Nani yuko kwenye kinyang'anyiro cha kuiongoza Kenya ?

Fahamu zaidi kuwahusu wagombea urais wa Kenya

Chagua mgombea ili kutazama wasifu wake

Raila Amollo Odinga

Muungano wa Azimio la Umoja

  • Mgombea huyo mwenye umri wa miaka 77 ni mhandisi aliyesomea Chuo Kikuu cha Ufundi cha Magdeburg (sasa kinajulikana kama Chuo Kikuu cha Otto-von-Guericke Magdeburg) nchini Ujerumani.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya Azimio la Umoja One Kenya Coalition Party.
  • Hili litakuwa jaribio lake la tano baada ya kugombea katika: 1997, 2007, 2013 na 2017.
  • Bw Odinga alikuwa mmoja wa wapiganiaji wa demokrasia ya vyama vingi nchini Kenya. Alikamatwa, akafungwa na wakati fulani akaenda uhamishoni kwa sababu ya kupigania haki hiyo
  • Aliwahi kuwa Waziri Mkuu, kuanzia 2008-2013.
  • Odinga alihusika kufanikisha miradi mikubwa iliyotekelezwa na serikali ya Kibaki, kama vile miradi ya umeme vijijini na barabara.
  • Kuafikia ukuaji wa uchumi wa tarakimu mbili kupitia uwekezaji katika biashara ndogo ndogo na sekta ya viwanda.
  • Utoaji wa huduma bora za afya kwa wote.
  • Utoaji wa vifaa vya michezo na burudani kwa ukuaji wa kimwili, kiakili, kijamii, kimaadili na maendeleo ya watu.
  • Kufuatia jaribio la mapinduzi ya Agosti 1, 1982, Raila Odinga alikamatwa na kukabiliwa na mashtaka kadhaa, yakiwemo ya uhaini ambayo alizuiliwa bila kufunguliwa mashtaka. Tume ya Ukweli ya Haki na Maridhiano iliambiwa mwaka 2011 kwamba Odinga alikuwa na mawasiliano na mpangaji mkuu wa mapinduzi hayo. Odinga amekana kuhusika kila mara. - Makavazi ya Kitaifa ya Kenya.

William Samoei Ruto

Muungano wa Kenya Kwanza

  • Mgombea huyu mwenye umri wa miaka 55 ana Shahada ya Uzamifu/PhD katika Ikolojia ya Mimea na BSc katika Botany na Zoology kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya chama cha United Democratic Alliance ( chenye mafungamano na Kenya Kwanza).
  • Aliongoza Vuguvugu la vijana la Youth for Kanu '92 (YK'(92).
  • Wizara yake iliorodheshwa kama inayofanya bora zaidi serikalini alipokuwa Waziri wa Kilimo.
  • Alihudumu kama Naibu Rais wa kwanza wa Kenya chini ya katiba mpya ya 2010.
  • Alihudumu kama mbunge wa eneo bunge la Eldoret Kaskazini kuanzia 1997-2007.
  • Kutenga $424 milioni kila mwaka kwa biashara ndogo ndogo za kati.
  • Kuanzisha mfuko wa elimu wa kitaifa ili kukidhi gharama zisizo za masomo.
  • Tekeleza kikamilifu sheria ya usawa wa kijinsia ya thuluthi mbili katika uteuzi wa kisiasa na kutenga nusu ya baraza lake la mawaziri kwa wanawake.
  • Mnamo 2008, Mahakama Kuu ya Kenya iliamuru Naibu Rais William Ruto kusalimisha shamba la ekari 100 na kulipa $ 62,500 kwa Adrian Muteshi, mkulima ambaye alimshtaki kwa kuchukua mali hiyo baada ya uchaguzi wa 2007. - Kenya Law
  • Mnamo 2011, Bw Ruto alikabiliwa na kesi kwa makosa matatu dhidi ya binadamu: Mauaji, uhamisho wa watu kwa lazima na mateso ya watu katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu. Miaka mitano baadaye mahakama ilisitisha kesi hiyo kwa msingi kwamba - ushahidi wa upande wa mashtaka ulikuwa dhaifu. -ICC

George Wajackoyah

Chama cha Roots

  • Profesa huyo mwenye umri wa miaka 61 ana shahada ya uzamili katika sheria kuhusu maendeleo kutoka Chuo Kikuu cha Warwick na shahada ya uzamili , sheria (sheria za Marekani kutoka Chuo Kikuu cha Baltimore.
  • Bw Wajackoyah anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Roots Party.
  • Alihudumu kama Inspekta katika idara ya usalama ya Special branch wakati wa utawala wa marehemu Rais Daniel Moi kabla ya kulazimika kutorokea ng'ambo ili kuepuka kufunguliwa mashtaka na mamlaka.
  • Yeye ni mshirika katika kampuni ya mawakili aliyoianzisha mwaka wa 2018.
  • Alifunnza somo la sheria na uchumi katika vyuo vikuu vya Marekani, Uingereza na Kenya.
  • Kuhalalisha matumizi ya kiviwanda ya bangi
  • Badilisha siku za kazi hadi Jumatatu hadi Alhamisi.
  • Huduma ya afya ya bure na msaada kwa wazee, walio hatarini na wajawazito

David Mwaure Waihiga

Chama cha Agano

  • David Mwaure anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Agano.
  • Ni kiongozi wa Chama cha Agano.
  • Alihitimu na shahada ya sheria kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi na ana Shahada ya Uzamili katika masomo ya uongozi.
  • Yeye ni wakili mkuu na amehudumu kama mwanasheria kwa zaidi ya miongo mitatu.
  • Ana kampuni ya uwakili na amewania viti mbalimbali vya kisiasa.
  • Ilianzishwa chama cha Agano mwaka 2006.
  • Kupambana na ufisadi uliokithiri.
  • kuunda nafasi za ajira.
  • Kurejesha mali ya Kenya iliyofichwa nje ya nchi.

Pata maelezo zaidi kuhusu sera za wagombea urais hapa

Bomas ni jina la kituo cha kitamaduni katika mji mkuu, Nairobi, ambacho kinatumika kama kituo kikuu cha kuhesabia kura.

Wafuasi wa Bw Ruto walishutumu wapinzani wao kwa kuingilia mchakato wa kujumlisha kura.

Polisi wa kutuliza ghasia wametumwa ndani ya jengo hilo ili kuimarisha usalama.

Kumekuwa na wito wa amani kutoka kwa viongozi na vyombo kadhaa likiwemo kanisa katoliki ambalo liliomba "uvumilivu na ustaarabu" na kuwataka wagombea wakuu "kujizuia na kuonesha ustaarabu" huku wasiwasi ukiongezeka.

"Nataka kuwa chombo cha kuleta amani, kuponya, kuunganisha na kudumisha matumaini katika nchi yetu," Bw Odinga alisema Jumapili asubuhi kwenye ibada ya kanisa jijini Nairobi, ikiwa ni matamshi yake ya kwanza kwa umma tangu siku ya uchaguzi.

Matokeo ya majimbo 141 kati ya 292 sasa yamethibitishwa, kwa mujibu wa ripoti ya BBC ya matangazo rasmi.

Mashirika ya habari yamekuwa yakitoa hesabu za muda kwa kutumia data rasmi kutoka kwa vituo 46,000 vya kupigia kura. Pia hesabu zao zinaonyesha ushindani mkali kati ya wagombea hao wawili.

Takriban kura milioni 14 zilipigwa - waliojitokeza kupiga kura ni 65%.

Tume ya uchaguzi ina hadi Jumanne tarehe 16 Agosti kutangaza mshindi.

"Lazima tufanye mabadiliko" ili kuharakisha mchakato wa kuhakiki matokeo, mkuu wa baraza la uchaguzi Wafula Chebukati alisema katika mkutano wake wa hivi wa leo.

"Inachukua saa tatu hadi nne" kushughulikia matokeo kutoka eneo bunge moja, alisema. "Baadhi ya maafisa wetu wanaorejea wamekaa hapa kwa siku tatu wakiwa wameketi kwenye viti, jambo ambalo halikubaliki kabisa."

Ni nini kinaendelea katika kituo kikuu cha kuhesabia kura?

Maafisa wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) bado wanashughulika na uhakiki wa matokeo katika kituo kikuu cha Bomas.

Wasimamizi wa uchaguzi wanalinganisha picha za fomu za matokeo kutoka vituo vya kupigia kura na fomu halisi ambazo maafisa wameleta kituoni ili kuhakikisha matokeo yanalingana.

Jitihada hizi kuu zimemfanya Bw Chebukati kuwashutumu maajenti kutoka vyama vikuu vinavyoshuhudia mchakato huo kwa kubadili zoezi la moja kwa moja kuwa la "uchunguzi".

Wakenya wanajisikiaje?

Kuna hali ya wasiwasi nchini kwani chaguzi zilizozozaniwa huko nyuma zilisababisha vurugu au mchakato mzima kufutwa.

Viongozi na mashirika kadhaa mashuhuri wamekuwa wakitoa wito wa uvumilivu na kuwataka Wakenya kudumisha amani.

Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Anthony Muheria amesema yeyote ambaye atatangazwa kuwa mshindi anapaswa "kukubali ushindi kwa heshima na unyenyekevu."

"Ikiwa umedhulumiwa, tafuta suluhu kupitia mchakato wa mahakama. Hakuna walioshindwa katika mchakato huu, mchakato wa kidemokrasia wenye mafanikio ni ushindi wetu sote," alisema.

"Tunalenga kujenga Kenya ambayo demokrasia yake inahimiza siasa za ushindani. Wagombea ambao hawajafaulu lazima wasichukuliwe kama walioshindwa, lakini kama Wakenya ambao wamechukua nafasi yao kupanua nafasi ya kidemokrasia."

Kufuatia kura ya 2007, takriban watu 1,200 waliuawa na 600,000 wakitoroka makazi yao kufuatia madai ya kuibiwa kwa kura.

Mnamo 2017, hitilafu kubwa za vifaa zilisababisha Mahakama ya Juu kubatilisha matokeo na kuamuru uchaguzi wa urais urudiwe.

Wakti huu viongozi wanakabiliwa na shinikizo la kurekebisha mambo.

Nchi mara nyingi hukabiliwa na mkwamo wakati wa uchaguzi, shughuli kote nchini zimepungua na shule zinasalia kufungwa hadi angalau Alhamisi 18 Agosti. Katikati ya jiji la Nairobi , mitaa yenye shughuli nyingi haina watu.

Madai ya wizi wa kura ni ya zamani kwani yalikuwepo hata kabla ya chaguzi za vyama vingi kuanzishwa tena katika miaka ya 1990, lakini msukumo wa uchaguzi huru na wa haki haujawahi kulegalega.

Baada ya ghasia zilizofuata uchaguzi wa 2007, vyama vya siasa na wanaharakati walibishania matumizi ya teknolojia badala ya sajili halisi, ambayo inaweza kubadilishwa kwa urahisi, ili kuhakiki wapiga kura.

Uchaguzi wa mwaka huu ni wa mara ya tatu kwa teknolojia kutumika lakini ni uchaguzi ambao haujazuia kupingwa mahakamani.

Tutajua matokeo lini?

Bado haijafahamika ni lini matokeo ya mwisho yatatangazwa.

Iwapo kuna uongozi wa wazi katika kinyanganyiro hicho, sherehe zinaweza kuzuka miongoni mwa wafuasi wake - lakini IEBC pekee ndiyo inaweza kutangaza matokeo.

Ili kushinda kinyang'anyiro cha urais katika awamu ya kwanza, mgombea anahitaji:

  • zaidi ya nusu ya kura zote zilizopigwa kote nchini
  • angalau 25% ya kura zilizopigwa katika angalau kaunti 24.
  • Vinginevyo upigaji kura unakwenda kwa duru ya pili ambayo kwa mujibu wa sheria inapaswa kufanyika ifikapo tarehe 8 Septemba.

Rais Uhuru Kenyatta anaondoka madarakani baada ya kuhudumu kwa mihula miwili. Amemuunga mkono mpinzani wake wa muda mrefu, Bw Odinga, badala ya naibu wake, Bw Ruto.

Uchaguzi
Uchaguzi