Matokeo ya Uchaguzi Kenya 2022: Tume ya uchaguzi Kenya imebadili mpango kazi ili kuharakisha ujumlishaji wa matokeo ya kura za urais

Chebukati

Chanzo cha picha, IEBC/Twitter

Maelezo ya picha, Mwenyekiti wa IEBC bwana Wafula Chebukati amekiri mwendo wa kupokea na kuhakiki matokeo hayo ya urais umekuwa wa kasi ya chini mno
    • Author, Idris Situma
    • Nafasi, BBC Swahili, Nairobi
  • Iliyochapishwa

Ikiwa ni siku ya nne sasa wakenya wakisubiri kwa hamu na ghamu kumjua rais wao mpya, Tume huru ya uchaguzi na mipaka ya Kenya IEBC imelazimika kubadili mpango wake wa kazi ilikuharakisha ujumlishaji wa matokeo ya uchaguzi wa urais mbali na kuhakiki stakabadhi zinazotoka katika maeneo yote nchini.

Mwenyekiti wa IEBC bwana Wafula Chebukati amekiri mwendo wa kupokea na kuhakiki matokeo hayo ya urais umekuwa wa kasi ya chini mno huku afisa mmoja akihitaji kati ya saa tatu na nne kuhudumiwa katika kituo cha kitaifa cha uchaguzi cha ukumbi wa Bomas Nairobi.

"Tume ya IEBC imegundua kuwa tunachukua kati ya saa 3 - 4 kukamilisha mchakato wa kupokea matokeo kutoka kwa afisa aliyesimamia uchaguzi katika eneo bunge moja. Tuna baadhi ya maofisa ambao wamekaa kwenye viti hivi kwa siku tatu. Maafisa 265 wameripoti. Tumefaulu kuwashughulikia 141 na kusalia na 124 ambao bado wako kwenye foleni'' Alisema Chebukati.

" Tunataka kufanya marekebisho yafuatayo: Wasimamizi wa uchaguzi watakabidhi fomu zao asili 34A kwa afisa wa kitaifa wa kujumlisha mara tu baada ya tangazo hili.

Shughuli ya kuhesabu kura inaendelea nchini Kenya baada ya raia wake kushiriki katika uchaguzi mkuu siku ya Jumanne.

Watatoa ripoti kwa dawati la TEHAMA, kwa uthibitisho wa matokeo yaliyotumwa dhidi ya Fomu 34A.

Tume hiyo ya IEBC imebadilisha orodha na hadhi ya watu wanaoruhusiwa kuingia kwenye kituo

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha, Tume hiyo ya IEBC imebadilisha orodha na hadhi ya watu wanaoruhusiwa kuingia kwenye kituo cha kitaifa cha kujumlisha kura

Baada ya hapo mawakala wa rais watapewa nakala za Fomu 34A na Fomu 34B kwa matumizi yao wenyewe. Tunageuza tu mtiririko wa mchakato. Tunaamini tutaweza kumalizana na maofisa wote ifikapo mwisho wa siku leo''.Alisema bwana Chebukati.

Wakati huo huo Tume hiyo ya IEBC imebadilisha orodha na hadhi ya watu wanaoruhusiwa kuingia kwenye kituo hicho cha kitaifa kujumlisha kura katika ukumbi wa Bomas.

Kamishna Prof. Abdi Yakub Guliye, amesema mabadiliko haya yanalenga kuhakikisha utaratibu na usalama unalindwa baada ya kuibuka majibizano kati ya wafanyakazi wa tume na mawakala wa upande wa wagombea wa urais wanaoongoza katika uchaguzi huu William Ruto na wale wa Raila Odinga.

''Kuanzia sasa ikiwa wewe si wakala mkuu wa Rais, naibu wakala mkuu, na makarani waliothibitishwa. Hakuna mtu mwingine atakayeruhusiwa kuketi katika ukumbi huu kuanzia dakika hii na kuendelea mbele.

Tumetoa maagizo kwa polisi kuchunguza upya kiingilio ndani ya Bomas (kituo cha kitaifa cha kuhesabu kura.) Waangalizi Wanadiplomasia na waandishi wa habari walioidhinishwa wanaruhusiwa kuendelea na kazi yao.

Nani yuko kwenye kinyang'anyiro cha kuiongoza Kenya ?

Fahamu zaidi kuwahusu wagombea urais wa Kenya

Chagua mgombea ili kutazama wasifu wake

Raila Amollo Odinga

Muungano wa Azimio la Umoja

  • Mgombea huyo mwenye umri wa miaka 77 ni mhandisi aliyesomea Chuo Kikuu cha Ufundi cha Magdeburg (sasa kinajulikana kama Chuo Kikuu cha Otto-von-Guericke Magdeburg) nchini Ujerumani.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya Azimio la Umoja One Kenya Coalition Party.
  • Hili litakuwa jaribio lake la tano baada ya kugombea katika: 1997, 2007, 2013 na 2017.
  • Bw Odinga alikuwa mmoja wa wapiganiaji wa demokrasia ya vyama vingi nchini Kenya. Alikamatwa, akafungwa na wakati fulani akaenda uhamishoni kwa sababu ya kupigania haki hiyo
  • Aliwahi kuwa Waziri Mkuu, kuanzia 2008-2013.
  • Odinga alihusika kufanikisha miradi mikubwa iliyotekelezwa na serikali ya Kibaki, kama vile miradi ya umeme vijijini na barabara.
  • Kuafikia ukuaji wa uchumi wa tarakimu mbili kupitia uwekezaji katika biashara ndogo ndogo na sekta ya viwanda.
  • Utoaji wa huduma bora za afya kwa wote.
  • Utoaji wa vifaa vya michezo na burudani kwa ukuaji wa kimwili, kiakili, kijamii, kimaadili na maendeleo ya watu.
  • Kufuatia jaribio la mapinduzi ya Agosti 1, 1982, Raila Odinga alikamatwa na kukabiliwa na mashtaka kadhaa, yakiwemo ya uhaini ambayo alizuiliwa bila kufunguliwa mashtaka. Tume ya Ukweli ya Haki na Maridhiano iliambiwa mwaka 2011 kwamba Odinga alikuwa na mawasiliano na mpangaji mkuu wa mapinduzi hayo. Odinga amekana kuhusika kila mara. - Makavazi ya Kitaifa ya Kenya.

William Samoei Ruto

Muungano wa Kenya Kwanza

  • Mgombea huyu mwenye umri wa miaka 55 ana Shahada ya Uzamifu/PhD katika Ikolojia ya Mimea na BSc katika Botany na Zoology kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya chama cha United Democratic Alliance ( chenye mafungamano na Kenya Kwanza).
  • Aliongoza Vuguvugu la vijana la Youth for Kanu '92 (YK'(92).
  • Wizara yake iliorodheshwa kama inayofanya bora zaidi serikalini alipokuwa Waziri wa Kilimo.
  • Alihudumu kama Naibu Rais wa kwanza wa Kenya chini ya katiba mpya ya 2010.
  • Alihudumu kama mbunge wa eneo bunge la Eldoret Kaskazini kuanzia 1997-2007.
  • Kutenga $424 milioni kila mwaka kwa biashara ndogo ndogo za kati.
  • Kuanzisha mfuko wa elimu wa kitaifa ili kukidhi gharama zisizo za masomo.
  • Tekeleza kikamilifu sheria ya usawa wa kijinsia ya thuluthi mbili katika uteuzi wa kisiasa na kutenga nusu ya baraza lake la mawaziri kwa wanawake.
  • Mnamo 2008, Mahakama Kuu ya Kenya iliamuru Naibu Rais William Ruto kusalimisha shamba la ekari 100 na kulipa $ 62,500 kwa Adrian Muteshi, mkulima ambaye alimshtaki kwa kuchukua mali hiyo baada ya uchaguzi wa 2007. - Kenya Law
  • Mnamo 2011, Bw Ruto alikabiliwa na kesi kwa makosa matatu dhidi ya binadamu: Mauaji, uhamisho wa watu kwa lazima na mateso ya watu katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu. Miaka mitano baadaye mahakama ilisitisha kesi hiyo kwa msingi kwamba - ushahidi wa upande wa mashtaka ulikuwa dhaifu. -ICC

George Wajackoyah

Chama cha Roots

  • Profesa huyo mwenye umri wa miaka 61 ana shahada ya uzamili katika sheria kuhusu maendeleo kutoka Chuo Kikuu cha Warwick na shahada ya uzamili , sheria (sheria za Marekani kutoka Chuo Kikuu cha Baltimore.
  • Bw Wajackoyah anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Roots Party.
  • Alihudumu kama Inspekta katika idara ya usalama ya Special branch wakati wa utawala wa marehemu Rais Daniel Moi kabla ya kulazimika kutorokea ng'ambo ili kuepuka kufunguliwa mashtaka na mamlaka.
  • Yeye ni mshirika katika kampuni ya mawakili aliyoianzisha mwaka wa 2018.
  • Alifunnza somo la sheria na uchumi katika vyuo vikuu vya Marekani, Uingereza na Kenya.
  • Kuhalalisha matumizi ya kiviwanda ya bangi
  • Badilisha siku za kazi hadi Jumatatu hadi Alhamisi.
  • Huduma ya afya ya bure na msaada kwa wazee, walio hatarini na wajawazito

David Mwaure Waihiga

Chama cha Agano

  • David Mwaure anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Agano.
  • Ni kiongozi wa Chama cha Agano.
  • Alihitimu na shahada ya sheria kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi na ana Shahada ya Uzamili katika masomo ya uongozi.
  • Yeye ni wakili mkuu na amehudumu kama mwanasheria kwa zaidi ya miongo mitatu.
  • Ana kampuni ya uwakili na amewania viti mbalimbali vya kisiasa.
  • Ilianzishwa chama cha Agano mwaka 2006.
  • Kupambana na ufisadi uliokithiri.
  • kuunda nafasi za ajira.
  • Kurejesha mali ya Kenya iliyofichwa nje ya nchi.

Pata maelezo zaidi kuhusu sera za wagombea urais hapa

Baadhi ya mawakala wa mgombea wa urais wa Muungano wa Azimio, Raila Odinga walionesha kutoridhishwa na kauli hiyo ya IEBC. Alisema Prof Guliye.

Haya yanajiri katika kituo cha kitamaduni kiitwacho Bomas katika mji mkuu, Nairobi, ambapo maafisa kutoka Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) wanashughulika na kuthibitisha matokeo.

Wanalinganisha picha za fomu za matokeo kutoka zaidi ya vituo 46,000 vya kupigia kura nchi nzima na fomu halisi zinazoletwa na maafisa kutoka kila moja ya maeneo bunge 290. Hii ni kuhakikisha kuwa matokeo yanalingana.

th

Haya yanashuhudiwa na maajenti wa vyama kutoka vyama vikuu, ambao Bw Chebukati anasema wanaendelea kuchelewesha hilo kwa kuligeuza kuwa la "uchunguzi" wa matokeo.

Shughuli ya kuhesabu kura katika baadhi ya vituo pia ilicheleweshwa na kusafiri hadi Nairobi, haswa na maafisa kutoka maeneo ya mbali, kunaweza kuwa sababu zaidi ya kupunguza kasi ya mambo.

Tutakuwa tukiwapa taarifa kuhusu matokeo ya uchaguzi kadiri taarifa rasmi zitakavyokuwa zikitufikia.

th

Uchaguzi Kenya 2022:Unaweza pia kusoma

th