Rubani mdogo mwenye miaka 19 aliyerusha ndege akiwa peke yake

Iliyochapishwa

Rubani kijana akawa mwanamke mwenye umri mdogo zaidi kuruka peke yake kuzunguka dunia baada ya changamoto ya miezi mitano.

Zara Rutherford, 19, alitua kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kortrijk-Wevelgem nchini Ubelgiji miezi miwili baadaye kuliko ilivyotarajiwa kutokana na hali mbaya ya hewa.

Wakati wa safari hiyo, alinaswa huko Nome, Alaska, kwa mwezi mmoja na siku 41 nchini Urusi. Aliporejea Ubelgiji, alikaribishwa na familia yake, waandishi wa habari na wafuasi wake.

Katika mkutano na waandishi wa habari, alisema "anafurahi sana" kupata changamoto ya kuruka kilomita 51,000.

"Sehemu ngumu zaidi ilikuwa kuruka juu ya Siberia: kulikuwa na baridi kali na kama injini ingesimama, alikuwa amesalia saa kadhaa kabla ya kuokolewa.

Sina uhakika kwamba angenusurika," alisema. "Ninataka sana kuwaambia watu kuhusu uzoefu wangu na kuhimiza watu kufanya kitu katika maisha yao," aliongeza. "Ikiwa una fursa, fanya hivyo."

Mzunguko huo ulijumuisha vituo zaidi ya 60 kwenye mabara matano na ulianza Agosti 18.

Mrusha ndege huyo wa Uingereza na Ubelgiji, ambaye wazazi wake ni marubani, alisema anatumai kuwatia moyo wasichana wengine kufuata fani za STEM (sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati).

Safari hiyo iliwezekana kutokana na wafadhili, ikiwemo shule aliyosoma Hampshire, Uingereza, na Shark, mtengenezaji wa Kislovakia wa ndege yake ya Shark UL.

Shule yake ya zamani ilikuwa mojawapo ya za kwanza kumpongeza, akiandika kwenye Twitter kwamba "inajivunia" mafanikio yake.

Hapo awali, mwanamke huyo mdogo zaidi kuruka peke yake duniani kote alikuwa Mmarekani Shaesta Waiz, ambaye alikuwa na umri wa miaka 30 mnamo mwaka wa 2017.

Kijana mwenye umri mdogo zaidi mwenye rekodi ana umri wa miaka 18. Pamoja na kuwa mtu mwenye umri mdogo zaidi kukamilisha mzunguko huo, Rutherford ndiye rubani wa kwanza mdogo na Mbelgiji wa kwanza kuzunguka dunia akiwa peke yake kwa ndege.

Miezi mitano kuzunguka dunia

Safari hiyo ilitarajiwa kudumu kwa miezi mitatu, lakini ucheleweshaji mwingi wa hali ya hewa ulikuwa na athari kubwa, na kusababisha visa yake ya Urusi kuisha msimu wa baridi wa Siberia ulipokuwa ukikaribia.

Alipofika Nome, ni safari tatu pekee kati ya 39 ndizo zilikuwa zimeenda kama ilivyopangwa, na ilimbidi angoje huku pasi yake ya kusafiria ikitumwa kwa ubalozi mdogo wa Urusi huko Houston.

Lakini hata akiwa na visa yake mpya, ilibaki wiki nyingine tatu kabla ya kuweza kuvuka Mlango-Bahari wa Bering.

Katika video iliyotumwa kwenye mtandao wa kijamii wa Instagram, alisema: "Ni baridi la -18C na mikono yangu inaganda. Nimekuwa hapa kwa karibu mwezi mmoja." "Nimekuwa nikishughulika, nimekuwa nikituma maombi kwa vyuo vikuu na kuweka ndege tayari kupaa," aliongeza. "Hali ya hewa haijawa nzuri. Kila wakati (nataka kwenda nje), hali ya hewa nchini Urusi ni mbaya sana au huko Nome ni mbaya sana."

Changamoto njiani

Wakati mmoja huko Siberia, ambapo halijoto ilikuwa chini ya -35°C ardhini na -20°C hewani, fundi alizuia baadhi ya maeneo ya kuingia hewa ya ndege yake ili kuweka injini joto katika baridi kali.

Licha ya marekebisho hayo, Rutherford alilazimika kukaa Magadan kwa juma moja kisha Ayan kwa majuma matatu.

Na baada ya hali ya hewa kulazimisha mapumziko bila kupangwa katika uwanja wa ndege wa Bandar Udara Rahadi Osman nchini Indonesia, ilimbidi kulala kwenye kituo hicho kwa siku mbili kwa sababu hakuwa na karatasi zinazohitajika kuondoka kwenye uwanja huo.

Licha ya vikwazo, na baada ya kutumia Krismasi na Mwaka Mpya mbali na familia yake, kijana huyo alikuwa na furaha na kutabasamu katika ujumbe wake wa Instagram.

Changamoto nyingine aliyokumbana nayo ni kuruka kupitia moshi kutoka kwenye moto wa nyika wa California.

Ndege yake pia ilifeli huko New Mexico kwa sababu ya bomba la Pitot lililoziba, na tairi kupasuka vilimwacha akiwa amekwama huko Singapore wakati wa Krismasi.

Akiwa Veracruz, Mexico, alipata tetemeko la ardhi katika chumba chake cha hoteli kwenye ghorofa ya sita. "Ghafla, jengo lilianza kuyumba.

Sidhani kama nimewahi kushuka ngazi kwa kasi kiasi hicho. Nilitarajia sehemu hatari zaidi ya safari hii iwe angani."

Mkuu wa shule yake, Jane Gandee, alisema wanafunzi na wafanyakazi wamekuwa wakifuatilia safari ya Rutherford "kwa shauku na kupendezwa naye." "Kama vile safari za ndege na urambazaji hazikuwa na changamoto ya kutosha, ilimbidi kukabiliana na hali mbaya ya hewa na urasimu mgumu," alisema.

"Tunajivunia sana ucheshi na ujasiri alioonesha wakati wote," aliongeza. "Wanafunzi wetu hamsini walitiwa moyo na Zara kujaribu kuruka, na nina hakika mfano wao utawatia moyo wanawake wengi zaidi vijana duniani," alihitimisha.