Mkataba wa nyuklia wa Iran : Ni nini na je utaanza tena?

Iliyochapishwa

Iran na kundi la mataifa yenye nguvu duniani wanakutana mjini Vienna wiki ijayo (29 Novemba) kujaribu kufufua makubaliano muhimu ya nyuklia.

Mvutano katika Mashariki ya Kati umekuwa ukiongezeka hivi karibuni kuhusu nia ya mradi wa nyuklia wa Iran - Israel imetenga $ 1.5bn kuandaa vikosi vyake vya kijeshi kwa ajili ya mashambulizi dhidi ya maeneo ya nyuklia ya nchi hiyo.

Na Shirika la Kimataifa la nguvu za Atomiki linaonya kuwa limeshindwa kufikia makubaliano na Iran kuhusu ukaguzi wa vifaa muhimu.

Iran daima imekuwa ikikanusha kujaribu kutengeneza silaha za nyuklia na inasema itaunga mkono kurejea kwa makubaliano ya awali na mataifa yenye nguvu duniani ambayo yalizuia shughuli zake za nyuklia ili kulegeza vikwazo vya kiuchumi.

Iwapo mazungumzo yatafanikiwa inaweza kusababisha mwisho wa vikwazo vya kiuchumi dhidi ya Iran na kupunguza uzalishaji wowote wa baadaye wa nyenzo hatari za nyuklia.

Lakini ikiwa mazungumzo hayatafanikiwa inaweza kuweka Mashariki ya Kati kwenye njia ya hatari.

Makubaliano ya awali ya nyuklia ya Iran yalikuwaje?

Yalikuwa ni makubaliano kati ya "P5+1" (hilo ni jina la kuvutia kwa wanachama watano wa kudumu wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa - Marekani, Urusi, China, Uingereza na Ufaransa - pamoja na Ujerumani) na Iran kuhusu mpango wa nyuklia wa nchi hiyo.

Iran ilikubali kukubali vikwazo vya urutubishaji na hifadhi yake ya uranium, kufunga au kurekebisha vifaa katika maeneo kadhaa ya nyuklia na kuruhusu ziara za wakaguzi wa kimataifa.

Kwa upande wake, vikwazo vingi vya kifedha vya kimataifa vilivyolemaza nchi viliondolewa.

Kundi la P5+1 liliamini kuwa makubaliano hayo yangezuia Iran kuendeleza uwezo wa kutengeneza silaha za nyuklia (Iran imekana kuwahi kutaka kufanya hivyo lakini imeshutumiwa kwa kujaribu hapo awali na nchi kadhaa na Shirika la Kimataifa la Nishati ya Atomiki).

Iran ilikuwa na matumaini kuwa kuondolewa kwa vikwazo kutaimarisha kwa kiasi kikubwa uchumi wake unaosuasua.

Baada ya mfululizo mrefu wa mazungumzo, mpango huo ulianza kutumika Januari 2016.

Kwanini makubaliano yalivunjika?

Jibu fupi ni Donald Trump.

Makubaliano hayo yalitiwa saini wakati wa uongozi wa Barack Obama, lakini Trump aliweka wazi muda mrefu kabla ya kufika Ikulu ya White House kwamba alidhani ni "makubaliano mabaya zaidi kuwahi kuona yakijadiliwa", na mara kwa mara akayadhihaki kuwa "ya kutisha" na "ya kucheka" .

Aliamini kuwa udhibiti wa shughuli za nyuklia za Iran ni dhaifu sana, kwamba ilipaswa pia kujumuisha vikwazo kwa mpango wa makombora ya masafa marefu ya Iran na kwamba masharti ya makubaliano hayakuchukua muda wa kutosha.

Rais Trump aliiondoa Marekani katika makubaliano hayo mwezi Mei mwaka 2018 na kurejesha vikwazo kwa Iran.

Katika kujibu hilo, Iran ilianza kurutubisha uranium zaidi ya viwango vilivyoruhusiwa na makubaliano na kupunguza ushirikiano wake na wakaguzi wa kimataifa.

Nani anataka kuyafufua?

Iran haikutaka kamwe makubaliano hayo yafutiliwe mbali ni Marekani tu wakati wa urais wa Trump ndiyo ilitaka kuona yakivunjwa.

Rais Biden aliunga mkono mpango huo alipokuwa makamu wa rais wa Obama na wengi wa washauri wake wa sasa wa Iran walikuwa watu waliosaidia kujadili masharti ya mkataba mwaka 2015.

Mazungumzo yatafanikiwa?

Kuna vikwazo

Iran ilikasirishwa na Marekani kutokana na kusambaratika kwa makubaliano hayo, na kuyataja kuwa ni "utawala mbovu".

Kipaumbele cha Iran ni kwa Marekani kuondoa vikwazo vyake, wakati lengo la Washington ni kuifanya Tehran kuacha kurutubisha madini ya uranium - kila mmoja anataka mwenzake achukue hatua kwanza.

Kwa sababu ya masuala haya Marekani inaweza isikutane moja kwa moja na Iran wakati wa mazungumzo.

Iran pia ilimchagua rais mpya mwezi Juni, Ebrahim Raisi, ambaye anaonekana kuchukua mtazamo mkali zaidi kuhusu uhusiano wa kimataifa kuliko serikali iliyopita.

Rais Raisi ameahidi hataruhusu mazungumzo ya mjini Vienna kuburuzwa.

Vile vile ametupilia mbali uwezekano wa kufanyika mazungumzo yoyote kuhusu mpango wa makombora ya balistiki ya Iran na sera zake za kieneo, ikiwa ni pamoja na uungaji mkono wake wa makundi yenye silaha katika nchi kadhaa, licha ya wito wa nchi za Magharibi kuwataka wawe sehemu ya makubaliano yoyote mapya yaliyofikiwa mjini Vienna.

Sababu hizi zinaweza kuifanya iwe ngumu zaidi kufufua mpango huo kuliko inavyoweza kuonekana mwanzoni.

Je, kila mtu atafurahi kuona mpango huo ukifanyika?

Saudi Arabia, mpinzani mkubwa wa kikanda wa Iran, iliunga mkono kwa uangalifu makubaliano ya zamani.

Lakini Israel (inadhaniwa kuwa ndio nguvu pekee ya nyuklia ya Mashariki ya Kati, ingawa haijawahi kuthibitisha hili) ilikosoa sana makubaliano ya awali, ikiamini kwamba ingeruhusu Iran kuelekea kupata silaha za nyuklia.

Baada ya hapo awali kufanya mashambulizi ya anga kwenye vituo vya nyuklia katika nchi nyingine mbili za eneo hilo, Israel imesema kamwe haitairuhusu Iran kutengeneza silaha za nyuklia.