Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Korea Kaskazini: Makombora tuliofyatua 'yaliongozwa kwa mbinu mpya'
Korea Kaskazini imedai kuwa makombora iliyoyafyatua siku ya Alhamisi "yaliongozwa kwa kifaa cha ufyatuzi kinachotumia mbinu mpya ", katika taarifa yake ya kwanza tangu ilipotekeleza jaribio hilo.
Ulikuwa ni uzinduzi wa kwanza wa nchi hiyo wa makombora ya masafa marefu tangu Rais Biden aingie madarakani.
Bw Biden amesema kuwa Marekani "itajibu ipasavyo". Marekani, Japan na Korea Kusini zimelaani majaribio hayo ya makombora.
Chini ya maazimio ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Korea Kaskazini imepigwa marufuku kufanya majaribio ya makombora ya masafa marefu.
Taarifa ya nchi hiyo ya Ijumaa, iliyotolewa kupitia vyombo vya habari vya kitaifa, inasema silaha hizo mbili zilipijga eneo lililolengwa lililopo umbali wa kilomita 600 (au maili 373 ) kutoka kwenye mwambao wa mashariki mwa Korea Kaskazini, kauli inayokinzana na tathmini ya Wajapan ambao wanasema kwamba yalipaa zaidi ya kilomita 400 pekee.
Iliongeza kuwa aina mpya ya kombora inaweza kubeba mzigo wa tani 2.5 , ambalo linaweza kubeba makombora ya nyuklia.
"Utengenezaji wa mfumo wa silaha hii ni wa muhimu katika kuonesha uwezo wa kijjeshi wa nchi na kuzima aina zote za vitisho vya kijeshi ," Ri Pyong Chol, afisa wa ngazi ya juu ambaye alishuhudia jaribio hilo, alinukuliwa akisema.
Kiongozi wa Korea Kskazini Kim Jong-un hakuwepo wakati wa tukio hilo..
Bwn Biden aliwaambia waandishi wa habari kwamba ufyatuaji wa makombora hayo ulikuwa ni ukiukaji wa maazimio ya Umoja wa Mataifa na kwamba Marekani inashauriana na washirika wake kuhusu hilo.
"Kutakuwa na jibu-kama wataamua kuendeleza ufyatuaji huo, tutajibu ipasavyo," alisema.
"Lakini pia nimejiandaa kwa aina fulani ya diplomasia, lakini lazima iwe na masharti ya kwamba matokeo yake yawe kuzuiwa kwa matumizi ya nyuklia Korea Kaskazini."
Bado haijaeleweka wazi ni aina ghani hasa ya makombora ambayo yamefyatuliwa na Korea Kaskazini. Vyombo vya habari vya taifa hilo vimesema kombora hilo lilikuwa na "aina iliyoboreshwa ya injini ngumu ya mafuta " na kulielezea kama kombora linaloongozwa kimkakati'' linaloweza kukwepa, ikimaanisha kuwa ni vijgumu kulilenga.
Na jaribio hilo linaonesha mafanikio katika mpango wan chi wa silaha za nyukli tangu mazungumzo ya kusitishwa kwa silaha za nyuklia yaliyokwama chini ya utawala wa Rais Trump.
Je Korea Kaskazini inamiliki makombora yapi?
Wachambuzi wamesema kuwa makombora hayo ni sawa na yale yaliyofichuliwa katika gwaride la jeshi katika mji mkuu Pyongyang mwezi Oktoba mwaka jana.
"Kama hilo ni kweli, wanaonekana kuboresha muundo wa kombora la awali lililojaribiwa aina ya KN-23 lenye "mfuniko mkubwa," Jeffrey Lewis wa kituo cha James Martin Center for Nonproliferation Studies (CNS) aliliambia shirika la habari la Reuters.
Aina hiyo ya kombora jipya inaweza kuiruhusu Korea Kaskazini kuweka makombora makubwa ya nyuklia kwenye maroketi , alisema profesa wa masomo ya usalama Vipin Narang, katika MIT kwenye ukurasa wa Twitter.
Mara ya mwisho Korea Kaskazini ilifyatua makombora mwaka mmoja uliopita huku uhusiano wa kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-Un na aliyekuwa rais wa Mareknai wakatio huo Donald Trump ukiwa mbaya.
Pyongyang bado haijatambua kwamba Bw Biden sasa yuko mamlakani, nan chi mbili zimesalia kuwa na uhasama kuhusiana na mipango ya Korea Kaskazini ya silaha za nyuklia na makombora ya baliistic.