Virusi vya corona: Ni mataifa gani yamepata chanjo ya corona Afrika

    • Author, Peter Mwai
    • Nafasi, BBC Reality Check
  • Iliyochapishwa

Watu zaidi ya 100,000 wamefariki kutokana na ugonjwa wa corona barani Afrika kufikia sasa, na kuna wasiwasi kuhusu kuchelewa kwa utoaji wa chanjo za virusi hivyo.

Tumeangazia kinachofanyika kuhusu utoaji wa chanjo hizo barani humo.

Mataifa ya Afrika yanapataje chanjo?

Kumekuwepo na ushindani mkali wa kupata chanjo duniani, na mataifa ya Afrika hayajafanikiwa kwani mataifa tajiri mengi yao yakiwa Ulaya na Marekani yamekuwa yakijitwalia chanjo zinazopatikana.

"Si haki kamwe kwamba Waafrika walio hatarini wanalazimika kusubiri chanjo huku makundi ya watu wasio hatarini katika mataifa tajiri wakipewa kinga (chanjo)," anasema Matshidiso Moeti, mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) katika ukanda wa Afrika.

Anasema anataka dozi za chanjo hizo zitolewe kwa mataifa ya Afrika upesi.

Mataifa ambayo yamepata chanjo za corona kufikia sasa yamefanya hivyo kupitia kununua moja kwa moja kutoka kwa watengenezaji wa chanjo hizo, au kupitia kupokea kama msaada au zawadi kutoka kwa mataifa kama vile China, Urusi, India na Umoja wa Milki za Kiarabu (UAE).

Mataifa ya Afrika yamekuwa yakitarajia kupuata chanjo kupitia mipango ya kimataifa na kikanda.

Moja ya mipango hiyo ni mpango wa Covax unaoungwa mkono na WHO. Chini ya mpango huo, mataifa yalileta pamoja rasilimali zao kusaidia utengenezaji wa chanjo kwa lengo la kuhakikisha kwamba kila taifa linapata chanjo kwa viwango vya kutosha.

WHO inatarajia kwamba mataifa ya Afrika yataanza kupokea dozi za chanjo kupitia mpango huo kuanzia mwisho wa mwezi huu, na chanjo za kwanza milioni 90 zinatarajiwa kufaidi 3% ya watu barani huo.

Dozi hizo za chanjo zitatumiwa kuwapa chanjo wanaohitaji zaidi, ambao ni pamoja na wahudumu wa afya na makundi mengine yaliyo hatarini.

Lengo kuu la Covax ni kutoa dozi 600 milioni za chanjo kwa Afrika, ambazo zitatosha asilimia 20 ya watu barani Afrika kufikia mwisho wa mwaka 2021.

Lakini John Nkengasong, mkuu wa Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa Afrika (Africa CDC), anasema chanjo zitakazopatikana kupitia mpango huo "hazitoshi kumaliza janga hilo" barani.

Anasema mataifa ya Afrika yatahitaji kutoa chanjo kwa angalau asilimia 60 ya raia wake, na lengo lake kwa mwaka huu ni asilimia 35 ya watu wawe wamepewa chanjo kufikia mwisho wa mwaka huu.

Upo pia mpango wa Umoja wa Afrika wa kuunganisha nguvu za mataifa yote 55 wanachama barani, na kutafuta chanjo kwa pamoja.

Kampuni kubwa zaidi ya mawasiliano ya simu barani Afrika MTN imetoa msaada wa $25m (£17.8m) kwa mpango huu kununua dozi milioni saba za chanjo kusaidia mpango huu wa AU, ambazo zitatumiwa kuwapa chanjo wahudumu wa afya.

Africa CDC inasema dozi milioni moja za kwanza zilizopatikana kupitia mpango huu zitasafirishwa kwa mataifa 20 ya Afrika kufikia mwisho wa mwezi Februari.

Orodha ya mataifa yatakayonufaika haijatolewa.

Ni mataifa gani yanayotoa chanjo kwa sasa?

Baadhi ya mataifa yalianza kutoa chanjo katika kipindi cha mwezi mmoja uliopita, lakini mengi hayajaanza.

Kufikia sasa, mataifa yanayotoa chanjo na chanjo wanazotumia Afrika Kaskazini ni:

  • Morocco (AstraZeneca na Sinopharm)
  • Algeria (Sputnik V)
  • Misri (Sinopharm)

Kusini mwa jangwa la Sahara, mataifa yanayotoa chanjo ni:

  • Afrika (Johnson & Johnson)
  • Ushelisheli (Sinopharm na AstraZeneca)
  • Rwanda (taarifa zinasema wanatumia Pfizer na Moderna)
  • Mauritius (AstraZeneca)
  • Zimbabwe (Sinopharm)

Mataifa mengine kama vile Senegal na Guinea ya Ikweta yamepokea chanjo za Sinopharm lakini bado hazijaanza kutoa chanjo kwa umma.

Guinea ilitoa chanjo 60 za Sputnik V kutoka Urusi kwa watu kwa majaribio.

Nini kinatokea Afrika Kusini?

Afrika Kusini, taifa lililoathirika zaidi na corona barani Afrika, lilichelewesha mpango wake wa kuanza kutoa chanjo kwa kutumia chanjo ya AstraZeneca kutokana na wasiwasi kuhusu ufanisi wake dhidi ya aina mpya ya kirusi kilichoongeza kasi ya maambukizi mapya nchini humo majuzi.

Taifa hilo lilianza kutoa chanjo tarehe 17 Februari baada ya kupokea dozi 80,000 za chanjo ya Johnson & Johnson, ambayo hutolewa mara moja na utafiti umebaini inafanikiwa dhidi ya aina mpya ya kirusi.

Rais Cyril Ramaphosa anasema taifa hilo limeahidiwa dozi milioni tisa za chanjo hiyo.

Pfizer pia wameahidi kutoa dozi 20 milioni za chanjo, za kwanza zikitarajiwa kuwasilishwa Afrika Kusini kabla ya mwisho wa mwezi Machi.

Afrika Kusini imetoa chanjo milioni moja za AstraZeneca ambazo haipangi kutumia kwa sasa kwa Umoja wa Afrika, ambao utayauzia mataifa yanayotaka dozi za chanjo hiyo.

Taarifa zaidi kuhusu virusi vya corona: