Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Trump amshinikiza gavana wa Georgia amsaidie kupindua ushindi wa matokeo ya uchaguzi
Rais wa Marekani Donald Trump amemshinikiza gavana wa Republican wa jimbo la Georgia kumsaidia kupindua ushindi wa Joe Biden jimboni humo.
Katika mfululizo wa ujumbe aliotuma kupitia mtandao wa Twitter, Donald Trump amemtaka mgombea Brian Kemp kuitisha kikao maalum cha bunge.
Hatua hiyo inawadia saa kadhaa baada ya Bwana Trump kuhudhuria mkutano wa kampeni huko Georgia wakati jimbo hilo linajitayarisha katika marudio ya uchaguzi wa seneti.
Rais bado amekataa kukubali kuwa alishindwa katika uchaguzi mkuu akidai kulikuwa na wizi wa kura ingawa hajawahi kutoa ushahidi wowote kuthibitisha kwamba ushindi wa Biden ulitokana na wizi wa kura.
Trump amefungua kesi mahakamani katika majimbo kadhaa lakini hadi kufikia sasa zote zimeshindwa kufaulu.
Jimbo la Georgia lilikuwa ngome muhimu katika uchaguzi huo ambapo Joe Biden aliibuka na ushindi mdogo - ikiwa ni mara ya kwanza jimbo hilo linampigia kura mgombea urais wa chama cha Democrat tangu mwaka 1992.
Sasa kampeni katika jimbo hilo zimeshika kasi. Ikiwa chama cha Democrat kitapata ushindi katika uchaguzi huo wa marudio utakaofanyika Januari 5, chama cha Republican kitapoteza udhibiti wa bunge hilo la juu.
Trump alisema nini?
Kulingana na gazeti la Washington Post, Bwana Trump alimuita gavana Kemp Jumamosi asubuhi na kumtaka adai kuchunguzwa kwa saini za kura za ambao hawakupiga.
Bwana Kemp - ambaye hana mamlaka ya kuitisha uchunguzi wa aina hiyo - alikataa ombi hilo, kwa mujibu wa vyanzo vya gazeti hilo.
Katika kipindi chote, Bwana Trump amekuwa akidai kuwa kura zilizopigwa kwa njia ya posta zilisababisha kusambaa kwa wizi wa kura lakini hana ushahidi wa kuthibitisho madai hayo.
Lakini kama haitoshi, Trump aligeukia mtandao wa Twitter kumshinikisha gavana huyo:
"Nitapata ushindi wa jimbo la Georgia kwa urahisi sana ikiwa gavana @BrianKempGA au waziri wa jimbo ataitisha kuthibitishwa tena kwa sahihi ... Kwanini wabunge hawa wa 'Republican' wanakataa kufanya hivyo?"
Bwana Kemp alijibu ujumbe huo kwa kusema "aliitisha kuthibitishwa tena kwa sahihi hizo mara tatu hadharani" na Trump akajibu: "Watu wako wanakataa kufanya unachotaka. Kwani wanaficha nini?"
Aliongeza: "Basi itisha hata kikao maalum cha bunge. Hilo ni jambo ambalo unaweza kulifanya kwa haraka na urahisi."
Katika mkutano wa kisiasa akizungumza na wafuasi wake, Trump aliendelea kusema kuwa Bwana Kemp anahitajika kuwa "jasiri kidogo".
Trump aliendelea kuambia hadhira kuwa bado anaweza kushinda uchaguzi. Akirejelea madai ya wizi wa kura: "Walidanganya na kutumia njia za ulaghai katika uchaguzi wetu wa urais lakini bado tutashinda."
Afisa wa uchaguzi katika jimbo hilo, Gabriel Sterling, pia wa chama cha Republican amemtaka rais kufuta madai yake ya wizi wa kura, akisema yanachochea vurugu.
Bwana Biden alishinda uchaguzi kwa kura 306 za wajumbe - mfumo unaotumika na Marekani kubaini mshindi - huku Trump akitia kibindoni kura 232.
Wajumbe watakutana Desemba 14, kuidhinisha matokeo hayo.