G20: Unyanyasaji wa haki za binadamu ambao ni sugu Saudi Arabia

Chanzo cha picha, Getty Images
Kwa Saudi Arabia kuwa mwenyeji wa mkutano wa wa nchi zenye uchumi mkubwa duniani- G20 ni fahari kubwa kwa taifa hilo.
Lakini kwa wanaharakati wa haki za binadamu kote duniani ni sababu ya kuwa na wasiwasi.
Na sasa kumetolewa wito kwa nchi za G20 kutumia fursa hiyo kushinikiza serikali ya Saudi Arabia.
Fahamu mambo matatu yanayowatia wasiwasi makundi ya haki za binadamu.
Wanaharakati wanawake kufungwa gerezani
Loujain al-Hathloul ni mwanamke maarufu wa kundi la wanaharakati wanawake aliyekamatwa 2018. Kwa mujibu wa familia yake alipigwa, akapewa mishtuko ya umeme na kutishiwa kubakwa baada ya kukamatwa.
Mwanamke huyo, 31, alikuwa amepigania wanawake kuruhusiwa kuendesha gari - haki iliyoruhusiwa Juni 2018 na serikali ya Saudi Arabia ikiwa ni muda mfupi tu baada ya mwanaharakati huyo kukamatwa.
Hata hivyo serikali ya Saudi Arabia imekanusha madai ya unyanyasaji dhidi ya raia wake na kusema kuwa mwenyekiti wa mkutano wa G20 mwaka huu, "ni kujitolea kikamilifu" katika kuwezesha kina mama na wasichana kote duniani.

Chanzo cha picha, FORD
Lakini wakati mkutano huo unaanza, afya ya Bi. Loujain al-Hathloul inaendelea kudhoofika kwasababu alianza mgomo wa chakula mwezi uliopita akishinikiza familia yake iruhusiwe kumuona mara kwa mara.
Inasemekana kuwa kazi aliotuma maombi ya Umoja wa Mataifa ndio ilitumiwa kama ushahidi dhidi yake.
Baroness Helena Kennedy, wakili wa haki za binadamu Uingereza, ametoa ripoti kuhusu wanaharakati wanawake wanaozuiliwa gerezani Saudi Arabia akiwemo Loujain al-Hathloul.
Wakili huyo anasema wafungwa wanazuiliwa katika mazingira mabaya, na pia wako katika hatari ya kunyanyaswa king'ono.
Shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International lilimuandikia Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson wiki iliyopita, kumuomba atumue fursa ya mkutano wa G20, kutaka wanaharakati wanawake waachiwe huru Saudi Arabia.


Chanzo cha picha, Getty Images
Mauaji ya kikatili
Mauaji ya mwanahabari ndani ya ubalozi wa Saudi uliopo Istanbul mwaka 2018 kulisababisha mshtuko mkubwa kote duniani na mgogoro wa kidiplomasia wa muda fupi.
Jamal Khashoggi alibanwa na kunyimwa pumzi na kikosi cha Saudi. Wanaume wanane walishitakiwa na kuhukumiwa katika kesi iliyoshtumiwa vibaya kwa kushindwa kukamata waliotekeleza mauaji ya mwanahabari huyo.
Lakini Saud al-Qahtani, mshauri wa karibu wa kiongozi wa nchi hiyo Mohammad Bin Salman, hakupatikana na hatia na aliachiwa huru.

Chanzo cha picha, Reuters
Mshauri huyohuyo alikuwepo wakati Loujain al-Hathloul anateswa gerezani, kwa mujibu wa familia yake. Aliwaambia kuwa Bwana al-Qahtani ametishia kumbaka, kumuua na kutupa mwili wake kwenye mfereji wa maji taka.
Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch limeshutumu serikali ya Saudi kwa kujifanya kutoona manyanyaso inayotekeleza.
"Miaka miwili tangu kuuawa kinyama kwa mwanahabari Jamal Khashoggi Oktoba 2018, hakuna afisa yeyote wa ngazi ya juu aliyeshitakiwa kwa mauaji hayo," Shirika hilo limesema.

Vita visivyo na mwisho
Vita vya miaka mitano kati ya Saudi Arabia na waasi wa Yemen umesababisha kile ambacho Umoja wa Mataifa unakiita mgogoro mbaya wa kibinadamu huku pande zote mbili zikishitumiwa kwa uwezekano wa kusababisha uhalifu wa kivita.
Mauaji ya raia yanaendelea kutekelezwa kwasababu ya mashambulizi ya anga yanayotekelezwa na muungano unaoongozwa na Saudi unaounga mkono serikali ya Yemen.
Timu ya Umoja wa Mataifa ilisema mwezi Septemba kuwa kuna idadi kubwa ya raia waliojeruhiwa kutokana na mashambulizi ya anga yaliyolenga masoko na mashamba.

Hata hivyo Saudi Arabia imekanusha madai hayo na kusema hailengi raia.
Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch linataka nchi za G20 kusihi Saudi Arabia iruhusu timu ya Umoja wa Mataifa kuingia Yemen, pamoja na makao makuu ya muungano unaofanya mashambulizi yaliyoko Riyadh.
Aidha, mashirika ya kutoa msaada na makundi ya kutetea haki za binadamu yametoa wito wa kukomeshwa kwa uuzaji wa silaha kwa Saudi Arabia.
"Wakati viongozi wa dunia wa G20 watakuwa wanakutana chini ya uongozi wa Saudi Arabia, watoto wa Yemen watakuwa wanaishi kwa hofu majumbani, huku vita vikiendelea kusababisha vifo vya ndugu zao katika mji wao wa nyumbani," amesema mkurugenzi wa shirika la Save the Children nchini Yemen, Xavier Joubert.
Pia amesihi nchi za G20 ambazo bado zinauzia silaha Saudi Arabia kukatisha makubaliano yao.
Bwana Joubert amesema: "Uuzaji wa silaha kunafanya vita hivi vinavyosababisha mauaji ya watoto kote nchini Yemen kuongezeka, huku idadi ya watoto waliojeruhiwa kutokana na mashambulizi ya anga ikiongezeka mara tano tangu wezi Juni ikilinganishwa na kipindi cha robo mwaka kilichotangulia."

Chanzo cha picha, Reuters
Waziri wa mambo ya nje wa Saudi Arabia Adel al-Jubeir wiki jana aliikosoa Ujerumani kwa kupiga marufuku uuzaji wa silaha kwa nchi hiyo akielezea vita vya Yemen kuwa "halali".
"Tunanunua silaha kutoka kwa nchi kadhaa, huwa tunafanya hivyo," amezungumza na shirika la Ujerumani la DPA.
"Kwahiyo kusema hatutauzia Saudi Arabia silaha, hakutapunguza lolote kwetu."












