Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Ngiri maji lenye uzani wa kilo 20 lavunja ndoto ya mkulima Matayo Kudenya Tanzania
- Author, Aboubakar Famau
- Nafasi, BBCSwahili, Tanzania
- Iliyochapishwa
Hujafa hujaumbika. Ni maneno ya wahenga. Hii inaonekana dhahiri katika maisha ya kijana Matayo Kudenya, mkazi wa kizota, jijini Dodoma.
Kudenya ambae awali alikuwa akijishughulisha na ukulima, kwa miaka kadhaa sasa shughuli zake zote zimesimama kutokana na tatizo la ngiri maji au busha ambayo imekuwa mwilini mwake na kufikia uzito wa takriban kilo ishirini.
Kudenya anasema anausikia uzito wa busha ukimlemea mwilini.
"Imekuwa ikikua kidogo kidogo na ilikuja kuzidi baada ya vidonda kuziba, hapo ndipo nilipojikuta tatizo linakuwa kwa kasi," anasema Kudenya.
Bila shaka, wengi watakuwa wanajiuliza, Kudenya anawezaje kuishi huku akiwa na ngiri maji yenye uzito wa takriban kilo ishirini mwilini?
"Ni shida kubwa sana ninayoipata," anasema na kuendelea, "Kwanza kutembea kwenyewe natembea kwa taabu. Natembea kama mtu aliyefanyiwa jando, natembea kwa kutanua miguu, kukaa kwenyewe hata kwenye kiti cha plastiki siwezi."
Ama kwa upande wa utafutaji, hakuna kinachoendelea kwa sasa. Tofauti na alivyokuwa awali akijishughulisha na ukulima, hivi sasa hakuna anachoweza kufanya zaidi ya kukaa ndani muda wote, hivyo kuwa tegemezi kwa ndugu, jamaa na marafiki.
Kudenya anasema tatizo la ngiri maji limebadilisha sana maisha yake.
"Nilikuwa ni kijana ninaejishughulisha na shughuli mbalimbali ikiwemo za kilimo, nilikuwa nimeanza kujiwekeza kiujumla, maisha yangu yamesimama kwa sasa," anasema.
Matumaini ya kupata tiba nayo yanaonekana kufifia. Gharama zinazohitajika kwa ajili ya tiba ni kubwa hivyo ndugu kushindwa kuzimudu.
"Baada ya kumtoa kijijini tumekuja nae hadi hapa mjini, na tulimpeleka hospitali ya Benjamen Mkapa, na kule madaktari walimtizama na wakasema siku zimekuwa nyingi, kama angewahi mapema kufanyiwa matibabu, ingekuwa rahisi, lakini kwa sasa inaonekana maji yale kwa ndani yameshaganda na wakasema inahitajika kufanyika upasuaji utaogharimu karibu shilingi laki nane, lakini bado zinatakiwa chap tatu za damu, gharama za kitanda na kulazwa hospitali mbali na gharama za kumuhudumia mpaka atakapopona ndio hayo makisio tuliyoyafanya kama shiligi milioni tatu, ambazo kwa kweli kama familia hatuna," anasema Steven John ambae ni mjomba wa Kudenya.
Dokta Peleus Kato ni daktari bingwa wa upasuaji katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Dodoma anasema chanzo kikubwa cha ngiri maji ni pale mishipa ya fahamu inaposhindwa kurudisha baadhi ya maji kwenye mfumo wa damu katika sehemu za korodani.
"Sasa yale maji yasiporudishwa kwenye mfumo wa damu, kwa hiyo unakuta yanajaa kwenye kurodani, na muda unavyozidi kwenda, yanaendelea kujaa," anafafanua Dk Kato.
Wataalamu wanashauri watu wawe na tabia ya kujichunguza mara kwa mara ili kuweza kubaini iwapo kuna tofauti yoyote inayoonekana kwenye korodani.
Ingawa hakuna takwimu rasmi zinazoonyesha ukubwa wa tatizo la ngiri maji nchini Tanzania, lakini wataalamu wanasema, ugonjwa huo umeendea hasa katika maeneo ya pwani, na unaathiri zaidi wazee.