Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Serikali ya Msumbiji imesema viongozi wa kundi la kigaidi waliouawa nchini humo ni Watanzania
Serikali ya Msumbiji imetangaza kuwa vikosi vya ulinzi nchini humo (FDS) vimedhibiti mji wa Macomia, katika jimbo la Cabo Delgado Kaskazini mwa Msumbiji na kuwaua viongozi wawili wa kundi la kigaidi.
'' Viongozi wawili wakuu wa makundi hayo waliuawa baada ya kuwepo kwa majibizano ya risasi,'' Waziri wa Ulinzi Jaime Neto alisema katika taarifa yake kupitia kituo cha televisheni (TMV)
Kwa mujibu Neto, waasi 78 walikufa katika operesheni ya kuurejesha mji na kuwa viongozi wawili waliouawa ni raia wa Tanzania, mmoja wapo aliyeongoza mashambulizi katika eneo la Mocimboa da Praia mwezi Oktoba mwaka 2017.
''Inaelezwa kuwa Njoroge ndiye aliyeanza mashambulizi Mocimboa da Praia tarehe 5 mwezi Oktoba mwaka 2017,'' Waziri alieleza akinukuliwa na shirika la habari la DW Afrika.
Hakuna taarifa zaidi zilizotolewa kuhusu vifo au madhara kwa raia au wanajeshi.
Makundi ya watu wenye silaha walitajwa kuwa magaidi na 'wafuasi wa kundi la Islamic state' waliudhibiti mji wa Macomia, mji mkuu katikati ya jimbo la Cabo Delgado, tangu siku ya Alhamisi.
Operesheni ya uvamizi imekuja baada ya kumekuwepo na mashambulizi tangu mwezi Machi hali iliyosababisha vijiji vingine kudhibitiwa kwa muda kama Mocimboa da Praia, Quissanga na Muidumbe, kukiwa na ripoti ya vifo kadhaa miongozi mwa raia, wanamgambo na wanajeshi.
Kundi la wanamgambo wa kiislamu limekuwa likidai kuhusika na matukio ya uvamizi kwa muda wa mwaka mmoja sasa.
Katika mzozo wa miaka miwili na nusu, inakadiriwa kuwa watu 550 wamepoteza maisha na wengine karibu 200,000 wamelazimika kuyaacha makazi yao kwenda sehemu salama, wakipoteza makazi na mali zao.
Tanzania yapeleka vikosi vyake mpakani na Msumbiji na Msumbiji
Tanzania ilipeleka vikosi vyake kwenye mpaka kati ya nchi hiyo na Msumbiji baada ya kuibuka kwa mashambulizi yaliyotekelezwa na wanamgambo kutoka kaskazini mwa nchi hiyo, wanamgambo ambao wamekuwapo tangu mwaka 2017.
Hatua ya kupeleka vikosi ilichukuliwa kama hatua ya tahadhari baada ya kutokea machafuko katika eneo la Cabo Delgado, gazeti la the Citizen limeripoti, likinukuu maafisa wa serikali.
Waziri wa nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, anayeshughulikia masuala ya sera, ajira, wenye ulemavu, kazi, bunge na vijana Jenista Mhagama alisema mwezi Machi, serikali ilipeleka vikosi katika eneo la Sindano mkoani Mtwara na Chiwindi, wilaya ya Nyasa, mkoani Ruvuma kusini mwa Tanzania.
Balozi wa Marekani anayeshughulikia masuala ya Afrika Tibor P Nagy, alisema uasi kaskazini wa Msumbiji unatia hofu.
Alisema ana matumaini Msumbiji itashughulikia hali hii kwa umakini mkubwa.