Virusi vya corona:Rwanda kuwarejesha nyumbani raia wake waliokwama Ulaya na Marekani.

Chanzo cha picha, Reuters
Raia wa Rwanda waliokwama Marekani na Ulaya kutokana na marufuku zilizowekwa za kudhibiti maambukizi wataanza kurudishwa nyumbani.
Hii ni baada ya baada ya serikali ya nchi hiyo kukamilisha mkataba na shirika la safari za ndge za taifa hilo, RwandAir, pamoja na washirika wengine wa kuanzisha safari za kila wiki kutoka Ubelgiji.
Wasafiri wote watakaorudi Rwanda watalazimika kukaa karantini kwa muda wa siku 14 katika maeneo ya karantini yaliyotengwa na Serikali.
Ndege za shirika hilo zitakuwa zikiwasafirisha nyumbani raia wa Rwanda, wakiwemo wanafunzi wanaosoma nje, na wakazi kwa ndege itakayokuwa ikisafiri kutoka katika mji mkuu wa Ubelgiji Brassels kuanzia kuanzia tarehe Mosi Mei.

Chanzo cha picha, Getty Images
Hatua hii inakuja baada ya balozi za Rwanda katika mataifa mbalimbali ya Ulaya pamoja na Marekani kuwataka raia na wanafunzi wa Rwanda katika nchi hizo wanaotaka kurejea nyumbani watume maombi kwa balozi hizo ili wapewe usaidizi.
Waziri wa mambo ya nje wa Rwanda Vincent Biruta ameliambia gazeti la The New Times nchini humo kwamba mpango uliopo ni kuwawezesha Wanyarwanda walioko nchi za ng'ambo kurudi kwao, hususan wanafunzi ambao wanahangaika baada ya shule kufungwa.
Kampuni ya Rwandair ilianza safari za mizigo kuelekea Brussels, na waziri Biruta anasema kila mara ndege huwa na viti vilivyo wazi ambavyo vinaweza kutumiwa kuwaleta Wanyarwanda waliokwama kutokana na corona.

Wanyarwanda hususan wale walioko nchini Marekani wameshauriwa kujisajili mapema kwa ajili ya safari ya kwenda Brussels kupitia makampuni ya ndege ya KLM, Delta, au United Airlines kutoka katika miji waliyomo ili waunganishwe na RwandAir.
Kwa mujibu wa balozi wa Rwanda nchini Marekani, Matilde Mutantabana, kuna jumla ya wanafunzi 495 wa Rwanda nchini Marekani ambao wameelezea nia yao ya kutaka kurejea nyumbani, na watu wengine 16 ambao sio wanafunzi.
"Kwa vyovyote vile inawezekana kuna Wanyarwanda wengine au wakazi ambao wanaweza kutaka kutumia fursa hii kwenda nyumbani ," alisema.
Hatua ya Rwanda ya kuwarejesha nyumbani raia wake waliokwamba ng'ambo kutokana na janga la virusi vya corona inakuja huku baadhi ya Waafrika wanaoishi katika taifa la Uchina wakilalamika juu ya ubaguzi wanaofanyiwa na Wachina baada mlipuko wa janga la virusi vya corona.

Picha zilizotumwa kwenye mitandao ya kijamii za watu wanaodaiwa kuwa ni Waafrika waliokwama kwenye mitaa ya Uchina baada kufurushwa kwenye nyumba na hoteli na kubaki bila makazi.
Baadhi ya Wakenya wanaoishi nchini Uchina wamekua wakizungumza na vyombo vya habari wakielezea masaibu wanayoyapata nchini Uchina, huku wakiiomba serikali yao iwasaidie kurejea nyumbani.

Wizara ya mambo ya nje nchini Kenya ilithithitisha kutambua kuhusu visa vya kutowatendea haki raia wa kigeni, na ikasema kuwa kupitia ubalozi wake nchini Uchina imepokea hakikisho kuwa serikali ya Uchina inalichukulia suala hilo kwa umakini na maafisa wa Guangzou wamepewa jukumu la kuchukua hatua za mara moja kulinda haki za Waafrika.













