Coronavirus: Idadi ya wagonjwa wa corona Tanzania yafikia 12

Chanzo cha picha, IKULU TANZANIA
Rais wa Tanzania John Pombe Magufuli ametangaza kuwa nchi hiyo ina wagonjwa 12 walioambukizwa ugonjwa wa corona.
Wanane kati ya wagonjwa hao ni raia wa Tanzania na wengine wanne ni raia wa kigeni.
Akihutubia taifa rais Magufuli alisema: ''Tumetishana sana Tanzania kana kwamba hakuna mogonjwa yanayouwa watu''
''Nimeanza kuwa na wasiwasi kwamba imefika mahali hata watu wanamsahau mungu kwamba Mungu ndiye mponyaji wa kweli katika maisha yetu, ile tuweze kushinda hili balaa lakini pia tunachukua tahadhari.'' aliongezea kusema.
Aidha Bw. Magufuli alisema kuwa ana matumaini kuwa janga hilo litapita.
''Tuchape kazi, tuendelee kumuomba mungu. Tusitishane, tusiogopeshana. Natoa wito kwa ndugu zangu wanaoandika mitandaoni kwa sababu kila mmoja amekuwa akiandika lake. Mengine wanapeleka kama mzaha. Huu ugonjwa sio wa kufanyiwa mzaha.''

Chanzo cha picha, AFP
Shirika la Afya Duniani (WHO) liliutangaza ugonjwa wa Covid-19 kuwa Dharura ya Kimataifa (yaani Global Health Emergency).
Hata hivyo, kutokana na kasi ya kusambaa kwake, tarehe 11 Machi, 2020,WHO iliutangaza ugonjwa huu kuwa Janga la Kimataifa.
Katika juhudi za kudhibiti kuenea kwa maaambukizi Rais Magufuli amesema kuanzia Jumatatu, wageni wote watakaoingia nchini humo kutoka mataifa yaliyo na visa vya ugonjwa huo watatengwa kwa siku 14 kwa gharama zao.
Agizo hilo linawajumuisha Watanzania wanaorejea nyumbani kutoka nchi zingine.
Ugonjwa wa Corona mpaka sasa hivi haujauwa mtu nchini Tanzania.
Hatua zingine zilizochukuliwa kudhibiti maambukizi ni zipi?
- Jumanne wiki hii nchi hiyo ilitangaza kufunga shule zote kwa siku 30 ikiwa ni hatua ya kuzuia kuenea kwa maambukizi ya corona nchini humo.
- Pamoja na kuzuia mikusanyiko yote ya watu wengi yakiwemo matamasha ya muziki, mikutano ya hadhara mbalimbali ikiwemo ya kisiasa.














