Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Rais wa Malawi, Peter Mutharika atakata rufaa dhidi ya uamuzi wa Mahakama
Rais wa Malawi, Peter Mutharika amekosoa uamuzi wa Jumatatu wa mahakama ya kikatiba kuwa ulikuwa wenye kujaa dosari ambazo zilipaswa kurekebishwa.
Akizungumza kwa mara ya kwanza tangu kutolewa kwa hukumu, Mutharika ameshutumu mahakama kwa kushambulia demokrasia ya nchi hiyo.
Mapema Alhamisi, alitangaza nia yake ya kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa mahakama katika Mahakama Kuu.
Ni wazi kuwa sasa Mutharika hatapoteza nafasi yake bila mikikimikiki.
Baada ya kuweka wazi nia yake ya kupinga uamuzi wa Jumatatu, Mutharika anafikiria kutetea ushindi wake wa mwezi Mei.
Amesema uamuzi huo ni kitendo cha 'uharibifu wa haki', na kusisitiza kuwa inahusisha na masuala ya utaratibu na si wizi wa kura.
Muthatika amewashukuru viongozi wa upinzani kwa kupeleka malalamiko yao mahakamani, akisema kuwa nchi yenye demokrasia pekee huruhusu hatua hiyo.
Lakini amekemea uamuzi wa majaji akisema ni mwanzo wa 'kifo cha demokrasia ya Malawi.'
Upinzani umekuwa ukishangilia uamuzi wa mahakama kama mwanzo wa uwepo wa demokrasia nchini humo, lakini huenda rufaa inayokuja inaweza kuzima furaha hiyo.