Picha ya mzee Norbert Schemm akipiga funda za bia ilisambaa kwenye mitandao ya kijamii.

Iliyochapishwa
Muda wa kusoma: Dakika 2

Kwanini picha ya Babu aliye karibu kuaga dunia akinywa funda za mwisho za bia imewavutia watu wengi sana duniani?

Norbert Schemm, 87,wa Appleton, Wisconsin, alitaka kutumia muda wa mwisho alionao akiwa na wapendwa wake pembeni wakati akinywa bia.

Pamoja na familia yake walizungumza, walicheka na kukumbuka matukio mbalimbali kabla ya kupiga picha ya pamoja ambayo mtoto wake aliituma kwenye kundi la Whats App la familia.

Lakini saa chache baadae wakati Bwana Schemm alipofariki na mjukuu wake kutuma picha mtandaoni, familia nzima waliguswa sana na idadi ya watu wengi waliowafariji kwenye picha yake ya mwisho.

Tayari ilikuwa ina maoni ya watu 4,000, na wengine 30,000 wakisambaza kwenye kurasa zao za Twitter na wengine 317,000 wakipendezwa na picha hiyo kwenye ukurasa wa Twitter pekee na kwenye mitandao mingine ya kijamii kama Reddit.

Unaweza pia kusoma

Adam anasema: ''Babu yangu alikuwa na afya siku zote, lakini siku ya Jumapili juma lililopita alipokuwa hospitali madaktari walibaini kuwa ndio mwisho wa maisha yake.

Aliwaita wajukuu zake ili kutuambia siku ya Jumatatu. Tukapiga picha siku ya Jumanne usiku na kisha alipoteza maisha siku ya Jumatano kwa ugonjwa wa saratani ya utumbo mpana''.

''Baba yangu alituambia babu alikuwa anataka bia na sasa nikitazama picha hii inanifariji.

''Ninaweza kusema babu yangu anatabasamu. Anafanya kile alichotaka kukifanya.

Adam anasema alisita kuweka picha kwenye mtandao wa kijamii mara ya kwanza kwasababu ya hali ya simanzi na uchungu wa mazingira ya picha hiyo, lakini aliamua kuendelea kwa sababu ulikuwa wakati mzuri sana.

''Inatusaidia katika machungu tuliyonayo. Inatufariji kuona wazee wetu na watoto wao wako pamoja, sote tuko pamoja katika wakati huu wa mwisho.''

Alisema familia imekuwa ikitazama picha hii imewafikia watu kwa kiasi gani na walipenda kuona namna watu walivyoiweka kwenye kurasa zao.

Ben Riggs, ni miongoni mwa watu walioguswa na picha hiyo, akaweka picha ya babu yake Leon Riggs, 86, akifurahia kitendo chake cha mwisho cha kuvuta sigara na kunywa bia.

Ben ameiambia BBC kuwa aliiona picha hiyo kweye kurasa za Twitter ikamkumbusha babu yake kuhusu ombi lake la mwisho kabla ya kifo chakwa mwaka 2015.

Ben alisema babu yake alikuwa na tatizo la kupoteza kumbukumbu, lakini mwishowe, yeye na baba yake walihisi ni muhimu kutimiza matamanio yake kabla ya kifo.

Ben alisema jioni moja babu yake alifariki, kaka zake na baba yake walikutana kwa ajili ya kusherehekea maisha yake. Wakapiga picha nyingine ya familia.

Kwanini picha hii imewagusa watu wengi?

Ann Neumann, mwandishi wa kitabu cha 'The Good Death, amesema: ''imewagusa wengi kwa sababu picha hutupa nafasi ya kufikiria kuhusu wapendwa wetu na kuungana na familia ya Schemm''.

Amesema picha ambazo kila mtu angependa ni zile za kuwa na wale uwapendao katika siku yako ya mwisho.

Kuna mamilioni ya hadithi kuhusu wazazi wanaopoteza maisha wakiwa hawana fahamu siku za mwisho za maisha yao.

Kukosa nafasi ya kusema kwaheri, ni hofu ambayo binaadamu wengi wanayo.

''Kama kuna cha kujifunza kutokana na picha hii ni kushikamana na wale tunaowapenda, kunywa bia, shikana nao mikono na mshirikiane kwa hadithi mbalimbali.

Kwa kuwa maisha yana mwisho''.