Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Kuwachunguza 'waponyaji wa kiroho' wanaowanyanyasa kingono wanawake
Ulimwengu uliofichwa wa unyanyasaji wa kingono na unyonyaji unaofanywa na wanaume wanaofanya kazi kama "waponyaji wa kiroho" umefichuliwa na BBC Idhaa ya Kiarabu.
Uponyaji wa kiroho, pia unajulikana kama "uponyaji wa Kurani", ni matendo maarufu katika ulimwengu wa Kiarabu na Kiislamu. Ni wanawake wengi wanaotembelea waponyaji, wakiamini kwamba wanaweza kutatua matatizo na kuponya magonjwa kwa kuwafukuza pepo wachafu wanaojulikana kama "jini".
Ushuhuda uliokusanywa na BBC kutoka kwa wanawake 85, kwa kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja, walitaja 65 wanaojiita waganga nchini Morocco na Sudan - nchi mbili ambako vitendo hivyo vinapendwa sana - na shutuma kuanzia unyanyasaji hadi ubakaji.
Tulitumia miezi kadhaa kuzungumza na mashirika yasiyokuwa ya kiserekali, mahakama, wanasheria na wanawake, kukusanya na kuthibitisha hadithi za unyanyasaji. Mwandishi wa siri ambaye alitibiwa na mganga mmoja wa aina hiyo kwa uchunguzi wetu, yeye mwenyewe alinajisiwa kabla ya kutoroka eneo la tukio.
Dalal (si jina lake halisi) alitafuta matibabu ya mfadhaiko kutoka kwa mganga wa kiroho katika mji karibu na Casablanca miaka michache iliyopita, alipokuwa katikati ya miaka yake ya 20. Anasema mganga huyo alimwambia huzuni hiyo ilisababishwa na "mpenzi wa jini" ambaye alikuwa amepagawa naye.
Katika kikao cha mmoja mmoja alimtaka kunusa harufu aliyosema ni miski - lakini ambayo sasa anaamini kuwa ilikuwa aina fulani ya dawa, kwa sababu alipoteza fahamu.
Dalal, ambaye hakuwahi kuwa na uzoefu wowote na ngono hapo awali, anasema aliamka na kukuta amevuliwa nguo yake ya ndani, na kugundua kuwa alikuwa amebakwa. Anasema alianza kumfokea raqi (mganga wa Qur'ani), akimuuliza alichomfanyia.
"Nilisema: 'Kwa nini umenifanyia hivi?' Akasema: Ili kuwatoa majini katika mwili wako.
Anasema hakumwambia mtu yeyote kilichotokea, kwani alikuwa na aibu na alikuwa na uhakika kwamba angelaumiwa. Alipogundua wiki chache baadaye kwamba alikuwa na mimba, aliogopa sana.
Alifikiria hata kujitoa uhai.
Alipomweleza mganga kuhusu ujauzito huo, alimjibu kuwa ni lazima jini huyo ndiye aliyempa mimba. Dalal anasema alihuzunishwa na hilo kwamba wakati mtoto wake alizaliwa, alikataa kumwangalia, kumshika, au hata kumpa jina, na kumtoa ili alelewe.
Alituambia kwamba ikiwa familia yake ingejua kilichompata, wangemuua.
Wanawake wengi tuliozungumza nao walisema wanahofia wao wenyewe wangelaumiwa ikiwa wangeripoti unyanyasaji wao, na kwa hiyo ni wachache sana waliowaambia familia zao, achilia mbali polisi.
Wengine walisema pia wana wasiwasi kwamba kuripoti kilichotokea kunaweza kuwachochea majini kulipiza kisasi kwao.
Nchini Sudan, mwanamke aitwaye Sawsan alituambia kwamba wakati mume wake aliondoka nyumbani na kwenda kuishi na mke wa pili ikiwa ni haki yake chini ya Sharia (sheria za Kiislamu) alijiona kuwa maskini, na alienda kwa mganga ili kupata msaada. Alisema alitarajia angeweza kumpa aina fulani ya dawa kwa ajili ya mume wake ambayo ingemfanya amtendee vyema.
Lakini hakutarajia matibabu yake yaliyopendekezwa.
"Alisema atafanya mapenzi na mimi na kutumia vimiminika vya mwili vilivyotokana na kutengenezea dawa nitakayompa mume wangu."
"hakuwa na woga", alisema.
"Alikuwa na imani kwamba sitamripoti kwa polisi au mahakama au hata mume wangu."
Sawsan anasema aliondoka kwenye kikao mara moja na hakurejea tena. Hakuripoti tabia yake.
Wanawake watatu kati ya 50 tuliozungumza nao nchini Sudan kuhusu unyonyaji au unyanyasaji walimtaja kiongozi mmoja wa kidini - Sheikh Ibrahim. Mmoja wa wanawake hao ambaye hatukumtaja jina, alisema alimdanganya na kufanya naye mapenzi. Mwingine, Afaf, alituambia ilimbidi kumsukuma kutoka kwake alipoomba kufanya naye ngono. Alisema alijisikia kukosa nguvu.
"Watu hawakubali kwamba mashekhe wanasema na kufanya mambo haya. Hawaamini. Nitapataje mashahidi? Hakuna aliyeniona chumbani kwake."
Kwa hivyo, mwandishi wa habari wa siri anayefanya kazi na timu yetu alikubali kumtembelea Sheikh Ibrahim kwa nia ya kukusanya ushahidi zaidi.
Ripota, ambaye tunamwita Reem, alijifanya kama mteja anayesumbuliwa na utasa.
Sheikh Ibrahim alisema atamswalia, na akatayarisha chupa ya "maji ya uponyaji" - inayojulikana kama "mahayya" - kwa ajili yake kwenda nyumbani na kunywa.
Reem anasema kisha akasogea kuketi karibu naye sana, na kuweka mkono wake juu ya tumbo lake. Alipomtaka aondoe mkono wake, anasema, aliusogeza tu mwilini mwake, juu ya nguo zake, hadi kwenye sehemu zake za siri. Alikimbia kutoka chumbani.
"Nilitikiswa sana naye," alituambia baadaye. "Alikuwa na sura ya wasiwasi juu yake."
Anasema alihisi kwamba tabia yake ilipendekeza hii haikuwa mara yake ya kwanza kufanya hivi.
BBC ilimhoji Sheikh Ibrahim kuhusu kilichompata Reem. Alikanusha kuwa aliwanyanyasa kingono au kuwanyanyasa wanawake akitafuta usaidizi wake, na akamaliza mahojiano yetu ghafula.
Mwanamke mmoja ambaye anatoa mbadala wa huduma kwa wale ambao wangependa uponyaji wa kiroho, bila hatari ya kunyonywa, ni Sheikha Fatima.
Akiwa na makao yake karibu na Khartoum, amefungua kituo cha matibabu cha wanawake pekee. Kwa miaka 30, hii imekuwa moja ya sehemu chache ambapo wanawake wanaweza kupata ruqyah au uponyaji kutoka kwa wanawake wengine.
Tulipewa nafasi pekee kufika. Wakati wa ziara yetu, ilikuwa ni kuangalia sana wanawake karibu nami wakipoteza ufahamu wote wa mazingira yao. Sheikha Fatima ananiambia jinsi wanawake wanavyoweza kudhurika katika hali hii, ambayo inaruhusu waganga wengine kuchukua kutumia fursa hiyo.
“Wanawake wengi walituambia kuwa wanaamini sheikh anamtoa shetani kwa kuwagusa, walidhani ni sehemu ya matibabu,” anasema. "Inashangaza unachosikia kutoka kwa wanawake hawa."
Tuliwasiliana na mamlaka za kisiasa nchini Morocco na Sudan na ushahidi wetu.
Nchini Sudan, Dk Alaa Abu Zeid, mkuu wa idara ya familia na jamii katika Wizara ya Masuala ya Kiislamu, awali alisita kuamini kwamba wanawake wengi wameripoti uzoefu wa unyanyasaji kwetu.
Lakini alikiri kwamba ukosefu wa udhibiti katika uponyaji wa kiroho ulimaanisha kuwa "kunasababisha machafuko", na kwamba jukumu hilo lilikuwa linatumika kama "taaluma kwa wale ambao hawana kazi".
Aliiambia BBC kwamba alichunguza udhibiti wake hapo awali, lakini kutokuwa na utulivu wa kisiasa nchini humo kunamaanisha kuwa sio kipaumbele kwa sasa.
Nchini Morocco, Waziri wa Masuala ya Kiislamu Ahmed Toufiq alisema haamini kuwa kuna haja ya kuwepo kwa sheria tofauti kuhusu waganga wa kiroho.
"Ni vigumu kuingilia kati kisheria katika masuala haya. Suluhisho lipo katika elimu ya kidini na mahubiri," alituambia.
Licha ya ushahidi wote tuliokusanya, mamlaka za Morocco na Sudan zinasita kuchukua hatua. Kwa hivyo mzigo unabaki kwa wanawake kusema dhidi ya wale wanaojificha nyuma ya taaluma ya uponyaji.