Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Kerala: Wanandoa waliobadili jinsia ambao picha zao za ujauzito zilisambaa
Picha ya ujauzito ya wanandoa wa India waliobadili jinsia - ambao walisitisha matibabu yao ya homoni ili kupata mtoto – imesambaa sana kwenye mitandao ya kijamii.
Ziya Paval, 21, na mpenzi wake Zahad, 23, wanaoishi katika jimbo la kusini la Kerala, walikuwa katika harakati za mabadiliko ya kijinsia walipoamua kupata mtoto.
Bi Paval, ambaye anasema siku zote alitaka kuwa mzazi, alikuwa mwanamume wakati wa kuzaliwa lakini sasa anajitambulisha kama mwanamke.
Bwana Zahad, ambaye anatumia jina moja tu, alikuwa mwanamke wakati wa kuzaliwa na sasa anajitambulisha kama mwanamume. Kwa sasa ni mjamzito, na wanandoa hao wanatarajia kumkaribisha mtoto wao hivi karibuni.
Pongezi zimemiminika kwa wanandoa hao kwenye kurasa zao za mitandao ya kijamii.
"Watu waliobadili jinsiawanastahili familia," mwigizaji aliyebadili jinsia S Negha alitoa maoni kwenye chapisho la Bi Paval kwenye Instagram, ambapo alikuwa ameshiriki picha hizo.
Bi Paval na Bw Zahad wanasema uzoefu wao unaweza kuwa wa nadra nchini India kwa sababu "hakuna mtu mwingine ambaye amejiita mzazi wa kibaolojia katika jumuiya ya watu waliobadili jinsia tunavyojua".
India inakadiriwa kuwa na takriban watu milioni mbili waliobadili jinsia, ingawa wanaharakati wanasema idadi hiyo ni kubwa zaidi. Mnamo 2014, Mahakama Kuu ya India iliamua kwamba wana haki sawa na watu wa jinsia nyingine.
Hata hivyo, bado wanatatizika kupata elimu na huduma za afya, na mara nyingi wanakabiliwa na chuki na unyanyapaa.
Wakati Bi Paval na Bwana Zahad walipokutana miaka mitatu iliyopita, wote walikuwa wametengwa na familia zao.
"Ninatoka katika familia ya Kiislamu ya kihafidhina ambayo haikuniruhusu kamwe kujifunza densi ya zamani," Bi Paval anasema. "[Wazazi wangu] walikuwa waaminifu hadi walionya kunikata nywele zangu ili nisicheze."
Bi Paval anasema aliondoka nyumbani na kushiriki tamasha la vijana na hakurudi tena.
Alijifunza dansi katika kituo cha jamii cha watu waliobadili jinsia. Sasa anaifundisha wanafunzi katika wilaya ya Kozhikode.
Bw Zahad, ambaye amefunzwa kama mhasibu, anatoka katika familia ya Kikristo kutoka jumuiya ya wavuvi katika jiji la Thiruvananthapuram. Hivi sasa anafanya kazi katika duka kubwa.
Alikuwa ameiacha familia yake baada ya kutoka kwao kama mtu aliyebadili jinsia. Lakini baada ya kupata ujauzito, familia yake imewakubali wenzi hao na kuwaunga mkono.
"Wanamsaidia Zahad wakati wa ujauzito," Bi Paval anasema.
Alikuwa ni mamake Bw Zahad ambaye awali aliwataka wanandoa hao kutoweka wazi ujauzito huo. Walitangaza kwenye ukurasa wao wa Instagram wiki iliyopita baada ya kupata ruhusa.
Bi Paval anasema familia yake bado haijafika.
Wanandoa hao waliamua kupata mtoto mwaka mmoja na nusu uliopita, wakati wote wawili walikuwa katika hatua tofauti za mabadiliko ya kijinsia, Bi Paval aliambia BBC.
Ovari na uterasi ya Bwana Zahad zilikuwa bado hazijatolewa, kwa hivyo wenzi hao waliacha matibabu ya homoni kwa ushauri wa madaktari wao.
Madaktari wa wanandoa hao hawajaruhusiwa kuzungumza na vyombo vya habari.
"Pindi tu ujauzito unapokwisha, wanaweza kuanza tena matibabu ya homoni za ngono," anasema Dk Mahesh DM, mtaalamu wa magonjwa ya mfumo wa endocrine katika jiji la Bangalore ambaye amefanya kazi na watu kadhaa waliobadili jinsia.
Baada ya mtoto kuzaliwa, wenzi hao wanasema itabidi watafute kazi zaidi ili kujikimu.
"Ni vigumu sana kuishi," Bi Paval anasema, akiongeza kwamba itabidi kuchukua wanafunzi zaidi wa kucheza.
"Zahad atarudi kazini karibu miezi miwili baada ya mtoto kuzaliwa. Kisha nitamtunza mtoto."
Wanandoa hao wanasema kuwa jamii ya watu waliobadili jinsia "imewakaribisha sana" ujauzito wao.
"Bila shaka, kuna watu ndani ya jumuiya ya waliobadili jinsia na nje ambao wanaamini katika dhana potofu. Wanafikiri kuwa mwanamume aliyebadili jinsia hawezi kubeba mtoto," Bi Paval anasema.
"[Lakini] haijalishi."