Rais Samia aridhia Makamu wa Rais Tanzania Nchimbi kujiuzulu

.

Chanzo cha picha, Ikulu

Iliyochapishwa
Muda wa kusoma: Dakika 2

Makamu wa Rais wa Tanzania, Emmanuel John Nchimbi, ametangaza kujiuzulu nafasi hiyo na kustaafu siasa pamoja na utumishi wa umma, na Rais Samia suluhu Hassan ameridhia.

Taarifa iliyotolewa na Ikulu kupitia kwa Katibu Mkuu kiongozi, Balozi Moses Kusiluka imesema: "Mheshimiwa Rais ameridhia ombi hilo" inasema taarifa hiyo ya Ikulu na kuongeza; "Taratibu za kikatiba za kumpata Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwingine zitachukuliwa.

Awali katika taarifa yake iliyochapishwa kwenye ukurasa wake rasmi wa Instagram , Nchimbi, amesema amemwandikia Rais Samia Suluhu Hassan barua ya kujiuzulu.

Nchimbi amesema kwamba uamuzi huo umefanywa kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Uamuzi huo utaanza kutekelezwa Septemba 4, 2026.

Amesema wakati akiteuliwa kuwa Makamu wa Rais, alimuahidi Rais Samia kwamba angemsaidia kwa uwezo wake wote na kwa uaminifu. Na kwamba alimwahidi pia Rais kwamba endapo siku moja angeona anahitaji Makamu mwingine wa Rais, angeachia nafasi hiyo.

"Siku yoyote akiona anahitaji Makamu mwingine wa Rais, nitaacha nafasi hii.", anasema Nchimbi.

Kwenye taarifa hiyo, Nchimbi amesema amejiridhisha kuwa Rais Samia anatamani mabadiliko, hivyo ameamua kutimiza ahadi hiyo.

Katika taarifa hiyo, Nchimbi amesema pia ameamua kustaafu siasa na utumishi wa umma.

Nchimbi amehudumu kama Makamu wa Rais kwa chini ya mwaka mmoja, tangu alipoapishwa kushika nafasi hiyo Novemba 3, 2025.

Alimrithi Philip Isdor Mpango, aliyekuwa Makamu wa Rais kati ya mwaka 2021 na 2025.

Nchimbi amesema uamuzi wake wa kujiuzulu ni sehemu ya kutimiza ahadi aliyowahi kutoa kwa Rais kwamba angeachia nafasi hiyo iwapo Rais angeona anahitaji Makamu mwingine wa Rais.

Katika siku za hivi karibuni, kumekuwa na joto la ndani ya chama chake cha Chamapinduzi (CCM), na hata taarifa za kujiuzulu kwakwe zilianza kuzagaa kwa wiki kadhaa sasa.