Moja kwa moja, Marekani yatangaza mashambulizi makubwa zaidi ya kiuchumi dhidi ya Iran

Serikali ya Iran pia imetoa onyo jipya kwa meli zinazopita katika eneo hilo, ikizitaka kutopita katika Mlango wa Hormuz bila ruhusa yake, kwa mujibu wa Reuters.

Ruka Video uendelee
  • xx
  • Besigye
  • .
  • xx
  • xx
  • xx
  • Lungu
  • xx
  • xx
  • d
  • s
  • a
  • Sonko
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • Dangote
  • Lydia Wanjiku

Moja kwa moja

Na MariamMjahid & Ambia Hirsi

  1. Iran yasema iko 'tayari' kukabiliana na vikwazo vya Marekani

    .

    Chanzo cha picha, Anadolu via Getty Images

    Iran imesema ina imani kuwa inaweza kukabiliana na vikwazo vilivyoongezwa vya Marekani, baada ya Washington kutangaza hatua ilizozielezea kama "Siku Kuu ya mashambulizi ya kiuchumi" (economic D-Day) dhidi ya nchi hiyo katika jaribio la kuitenga na uchumi wa dunia.

    Waziri wa Uchumi wa Iran, Ali Madanizadeh, amesema Tehran iko "tayari" kukabiliana na vikwazo hivyo, ambavyo alisema "vitaifedhehesha" Marekani.

    Akitangaza hatua hizo mpya, Waziri wa Fedha wa Marekani Scott Bessent alisema taifa lolote litakaloshirikiana kifedha na Iran litatengwa, na kwamba benki pamoja na kampuni za biashara zinazofanya kazi na Iran zitakabiliwa na hatama.

    Hatua hizi zinakuja kufuatia mabadiliko ya msimamo na kuongezwa kwa muda wa mwisho na Ikulu ya Marekani katika juhudi zake za kumaliza mzozo huo.

    Bessent alielezea hatua hizo kama "shambulio kubwa zaidi la kifedha lisilo na kifani" dhidi ya Iran, ambalo "litaziba kila mianya yote kuingiza mapato".

    Baadhi ya wachumi wametoa shaka iwapo vikwazo hivyo vya hivi karibuni vitakuwa na ufanisi, kwani hilo linategemea mwitikio wa washirika wa kibiashara wa Iran.

    Hawa ni pamoja na China, mnunuzi mkuu wa mafuta ya Iran, ambayo imepuuza vikwazo vya awali vya Marekani na kuendelea kufanya biashara na Tehran.

    Wiki iliyopita, mshirika mwingine wa kibiashara wa Iran, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), ilisema inasitisha miamala yote ya kifedha na nchi hiyo.

  2. Mazungumzo ya amani kati ya Iran na Pakistan yapiga hatua

    H

    Chanzo cha picha, IRNA

    Pakistan imesema kumepatikana maendeleo makubwa katika mazungumzo yaliyofanyika mjini Tehran kati ya wajumbe wake na viongozi wa Iran, yaliyolenga kutafuta njia za kufikia amani.

    Ujumbe wa Pakistan uliongozwa na Mkuu wa Majeshi, Field Marshal Asim Munir.

    Kwa mujibu wa taarifa, mazungumzo yake na Rais wa Iran, Waziri wa Mambo ya Nje pamoja na Spika wa Bunge yalijikita katika hatua za kuzuia mzozo kuongezeka, kufungua tena Mlango wa Hormuz na kutafuta njia ya kumaliza vita kati ya Iran na Marekani.

    Pia imeripotiwa kuwa Field Marshal Munir aliwasiliana na Rais wa Marekani, Donald Trump, kabla ya kusafiri kwenda Tehran.

    Taarifa zinaeleza kuwa Marekani imeiomba Pakistan kutumia ushawishi wake kuishawishi Iran kurejea kwenye meza ya mazungumzo.

    Hata hivyo, Washington haijatoa taarifa rasmi kuhusu matokeo ya mazungumzo hayo.

  3. Guterres alaani shambulio la kushtukiza dhidi ya walinda amani wa UNMISS Sudan Kusini

    António Guterres

    Chanzo cha picha, EPA-EFE/REX/SHUTTERSTOCK

    Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres amelaani shambulio la Jumatatu lililofanywa na watu wasiojulikana dhidi ya walinda amani wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini (UNMISS) katika Jimbo la Jonglei.

    Walinda amani wawili wa Ethiopia waliuawa katika shambulio hilo, huku wengine saba wakijeruhiwa.

    Waliojeruhiwa ni pamoja na walinda amani watatu wa Ethiopia, wanachama wawili wa Huduma ya Kitaifa ya Polisi ya Sudan Kusini na wafanyakazi wawili wakiraia wa ujumbe UNMISS.

    Ujumbe huo wa Umoja wa Mataifa ilishambuliwa wakati ukisafiri kwenda Pajut katika Jimbo la Jonglei.

    Hakuna kundi lililodai kuhusika na Umoja wa Mataifa mpaka sasa haujawatambua washambuliaji.

    Ujumbe wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa ulisema umetuma "Kikosi cha dharura" kutoa ulinzi katika eneo hilo.

    Guterres alitoa salamu za rambirambi kwa familia za waliouawa na kusisitiza kwamba mashambulizi dhidi ya walinda amani wa Umoja wa Mataifa yanaweza kuwa uhalifu wa kivita, akisisitiza hitaji la mashambulizi kama hayo kuchunguzwa haraka na wahusika kuchukuliwa hatua.

    Jimbo la Jonglei nchini Sudan Kusini linakabiliwa na mgogoro mkubwa wa kibinadamu na usalama, unaoonyeshwa na mapigano mapya kati ya vikosi vya serikali na wanamgambo wenye silaha, umepelekea watu wengi kuhama makazi yao.

    "Ukatili mbaya kama huo unaowalenga wafanyakazi wa UNMISS wanaohudumu kuunga mkono amani Sudan Kusini haukubaliki" alisema Anita Kiki Gbeho, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na Mkuu wa UNMISS.

    Takwimu za Umoja wa Mataifa zinaonyesha kwamba takribani wafanyakazi 36 wa kibinadamu na wakandarasi waliuawa Sudan Kusini mwaka wa 2026, huku mashambulizi yakijikita zaidi katika maeneo yaliyoathiriwa na migogoro kama vile Jonglei na Upper Nile.

  4. Marekani yaweka zawadi kwa taarifa zitakazosaidia kuwabaini makamanda wa IRGC

    S

    Chanzo cha picha, X/RFJ

    Marekani imetangaza zawadi ya fedha kwa taarifa zitakazosaidia kuwabaini baadhi ya makamanda wa sasa na waliowahi kuhudumu katika Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu la Iran, IRGC.

    Idara ya Mambo ya Nje ya Marekani imetangaza zawadi ya hadi dola milioni 10 kwa taarifa kuhusu maafisa wanne waandamizi wa IRGC.

    Akaunti ya Rewards for Justice, inayohusishwa na Idara ya Mambo ya Nje ya Marekani, iliandika kwenye mtandao wa X kwamba watu hao wanaongoza vitengo vya Walinzi wa Mapinduzi ambavyo vimehusishwa na mashambulizi dhidi ya wanajeshi wa Marekani pamoja na operesheni za kimtandao zilizolenga miundombinu muhimu.

    Miongoni mwa waliotajwa ni Ahmad Vahidi, kamanda wa Walinzi wa Mapinduzi, Ali Abdollahi, kamanda wa makao makuu ya Khatam al Anbiya, na Hamidreza Lashgarian, kamanda wa kitengo cha mtandao cha Walinzi wa Mapinduzi.

    Orodha hiyo pia inawataja Saeed Aghajani, aliyekuwa kamanda wa Kikosi cha Anga na Anga za Juu cha IRGC, pamoja na Majid Khademi, aliyekuwa kamanda wa ujasusi wa IRGC. Wawili hao waliuawa katika vita vya hivi karibuni.

    Soma pia:

  5. Netanyahu ampongeza Trump kwa kuongeza vikwazo dhidi ya Iran

    N

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, amempongeza Rais wa Marekani Donald Trump na Waziri wa Hazina Scott Bessent kwa vikwazo vipya vilivyowekwa dhidi ya Iran.

    Katika ujumbe kwenye mtandao wa X, Netanyahu alisema:

    "Hongera Rais Donald Trump na Scott Bessent kwa vikwazo vipya dhidi ya serikali ya Iran."

    Netanyahu aliongeza:

    "Kwa usahihi mnaweka gharama kubwa kwa utawala huo usio na huruma na wanaounga mkono kuendelea kwa uchokozi wake."

    Soma Pia:

  6. Bahari za dunia zafikia joto la juu zaidi kuwahi kurekodiwa huku El Niño ikizidi kuwa kali

    d

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Bahari za dunia zimefikia kiwango cha juu zaidi cha joto kuwahi kurekodiwa, kwa mujibu wa takwimu mpya, huku zikikabiliwa na athari za mabadiliko ya tabianchi yanayosababishwa na shughuli za binadamu pamoja na hali ya hewa ya El Niño inayozidi kuwa kali.

    Joto la wastani la uso wa bahari duniani, nje ya maeneo ya ncha za dunia, lilifikia nyuzi joto 21.1 Selsiasi siku ya Jumamosi, kwa mujibu wa takwimu za huduma ya Copernicus ya Umoja wa Ulaya inayofuatilia mabadiliko ya tabianchi.

    Kiwango hicho kimevuka rekodi ya nyuzi joto 21.09 Selsiasi iliyorekodiwa katika siku tatu tofauti mwezi Machi 2024, na kiko juu kwa kiasi kikubwa ya wastani wa kipindi hiki cha mwaka.

    Joto la bahari linaweza kuwa na madhara makubwa, ikiwemo kuchochea hali mbaya ya hewa, kuongeza kina cha bahari na kuhatarisha viumbe wa baharini.

    "Hii ni ishara nyingine ya wazi kwamba bahari inazidi kukabiliwa na msongo," alisema Dk Samantha Burgess, naibu mkurugenzi wa Copernicus.

    Aliongeza kuwa El Niño inaongeza joto kwenye mfumo wa hali ya hewa, lakini inafanya hivyo juu ya ongezeko la joto ambalo limechochewa na shughuli za binadamu kwa miongo kadhaa.

    Wanasayansi wanatarajia El Niño kuendelea kuimarika hadi kipindi cha Krismasi, huku wakionya kuwa huenda ikawa kali zaidi kuliko tukio lolote lililoshuhudiwa katika karne kadhaa.

    Hali hiyo inaweza kusababisha joto la bahari kuongezeka zaidi.

    Dk Jeremy Grist, mtafiti mwandamizi katika Kituo cha Kitaifa cha Utafiti wa Bahari mjini Southampton, alisema kuvunjwa kwa rekodi hizi mapema ni ishara ya jinsi El Niño inavyozidi kuwa kali.

    Soma Pia:

  7. Marekani yaiondoa Syria kwenye orodha ya nchi zinazodhamini ugaidi

    B

    Chanzo cha picha, AP

    Marekani imeiondoa Syria kwenye orodha ya nchi zinazodhamini ugaidi baada ya miaka 47, hatua inayofungua njia kwa uwekezaji wa sekta binafsi na kurejeshwa kwa Syria katika uchumi wa dunia.

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Marco Rubio, alisema uamuzi huo unatambua hatua chanya zilizochukuliwa na serikali ya Syria kujitenga kikamilifu na vitendo vya ugaidi wa kimataifa.

    Utawala wa Rais Donald Trump umeanzisha uhusiano na Rais mpya wa Syria, Ahmed al Sharaa, ambaye zamani alikuwa mpiganaji wa kundi lenye uhusiano na al Qaeda na wakati mmoja Marekani iliweka zawadi kwa taarifa zitakazosaidia kukamatwa kwake.

    Kundi lake la Hayat Tahrir al Sham, HTS, pia limeondolewa kwenye orodha ya Marekani ya mashirika ya kigaidi duniani.

    HTS, ambalo zamani lilijulikana kama al Nusra Front, lilikuwa tawi la al Qaeda nchini Syria hadi Sharaa alipokatiza uhusiano na mtandao huo mwaka 2016.

    Mwishoni mwa mwaka 2024, HTS iliongoza mashambulizi ya waasi yaliyomuondoa madarakani Rais wa zamani Bashar al Assad na sasa linatawala serikali ya mpito inayoongozwa na Sharaa.

    Marekani inalenga kuiweka Syria karibu na ushawishi wake badala ya kuiacha chini ya ushawishi wa Urusi au China. Hata hivyo, Syria bado inakabiliwa na changamoto kubwa za usalama na haina serikali inayowakilisha makundi yote ya wananchi.

    Rubio alisema uamuzi huo utaipa Syria "njia ya kuelekea ustawi".

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Syria, Asaad Hassan al Shaibani, aliuita uamuzi huo "hatua ya kihistoria", akisema nchi hiyo itaendelea kufanya kazi kuondoa madhara ya kutengwa na kujenga mazingira yanayozingatia uwazi, maslahi ya pamoja na heshima.

    Syria ilikuwa kwenye orodha hiyo tangu mwaka 1979. Baada ya kuondolewa kwake, nchi tatu pekee zimesalia kwenye orodha hiyo ya Marekani: Cuba, Korea Kaskazini na Iran.

    Kuwekwa kwenye orodha hiyo kunaambatana na vikwazo vya kifedha, vizuizi vya misaada ya Marekani, pamoja na mauzo ya silaha na vifaa vya ulinzi. Pia kunaweza kuwaadhibu watu binafsi na nchi nyingine zinazofanya biashara na nchi iliyowekewa vikwazo.

  8. Trump atishia kuongeza ushuru wa magari kutoka Canada

    G

    Chanzo cha picha, EPA

    Rais Donald Trump ametishia kuongeza ushuru wa Marekani kwa magari, malori na vipuri vinavyotoka Canada, huku vita vya kibiashara kati ya nchi hizo mbili vikiendelea kupamba moto.

    Trump alisema ushuru huo utaongezwa kutoka asilimia 25 hadi asilimia 50 kuanzia Januari 1, baada ya mazungumzo ya kibiashara kati ya Marekani na Canada kuvunjika mwishoni mwa wiki.

    Pande hizo mbili zimetuhumiana kutoa matakwa yasiyokubalika katika hatua za mwisho za mazungumzo.

    Waziri Mkuu wa Canada, Mark Carney, amesema tishio hilo halikumshangaza, akimtuhumu Trump kutaka kuangusha sekta ya magari ya Canada.

    Carney alisema Canada iko tayari kurejea kwenye mazungumzo iwapo Marekani itakuja na "mtazamo unaofaa".

    Serikali ya Canada imetangaza mkutano na waandishi wa habari Jumanne, kueleza hatua itakazochukua kukabiliana na vita hivyo vya kibiashara na kulinda wafanyakazi pamoja na biashara za Canada.

    Canada ilijiondoa kwenye mazungumzo ya kibiashara Ijumaa usiku, muda mfupi kabla ya kuanza kwa makataa ya Marekani ya kutoza ushuru wa asilimia 50 kwa bidhaa za Canada zenye thamani ya karibu dola bilioni 20 za Marekani.

    Soma Zaidi hapa:

  9. Waziri Mkuu wa Uingereza aahidi kuendelea kuisaidia Ukraine licha ya 'vitisho vikali' kutoka Urusi

    d

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Waziri mkuu wa Uingereza Andy Burnham ameahidi kuendelea kuongeza shinikizo dhidi ya Urusi, licha ya kile alichokiita "vitisho vya kupindukia" kutoka Moscow, wakati wa ziara yake rasmi ya kwanza nchini Ukraine akiwa Waziri Mkuu wa Uingereza.

    Burnham alikutana na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky na kuongoza mkutano wake wa kwanza wa "muungano wa walio tayari", ulioanzishwa na Uingereza na Ufaransa chini ya mtangulizi wake, Sir Keir Starmer.

    Alisema muungano huo "unafanya kila uwezalo", huku akiitaka Bunge la Marekani kuongeza shinikizo la kiuchumi dhidi ya Urusi.

    Serikali ya Uingereza imekubali kuikabidhi Ukraine michoro ya kiufundi ya vipengele vinavyotengenezwa nchini humo kwa ajili ya kombora la Scalp, toleo la Ufaransa la kombora la masafa marefu la Storm Shadow la Uingereza. Hatua hiyo itawezesha Ukraine kuzalisha silaha hiyo ndani ya nchi.

    "Huu ndio wakati wa kuendelea kuongeza shinikizo dhidi ya Urusi na kudhoofisha uwezo wake wa kugharamia vita hivi visivyo halali," Burnham alisema, huku akisifu "nguvu" ya watu wa Ukraine.

    Alisema Ukraine imekuwa "mlinzi wa Ulaya, si mzigo kwa usalama wetu, bali mstari wa mbele katika kuhakikisha Ulaya inabaki salama."

    Kauli hiyo imekuja baada ya msemaji wa Kremlin, Dmitry Peskov, kuikosoa Uingereza kwa uamuzi wake wa kushiriki michoro hiyo ya makombora. Peskov alisema hatua hiyo inazuia "hata dalili ndogo ya maendeleo" kuelekea amani.

    Aliwaambia waandishi wa habari Jumatatu kuwa jeshi la Urusi tayari linakusanya taarifa za kubaini maeneo yanayozalisha makombora hayo ili kuyaangamiza.

    "Uingereza inahusika katika vita hivi upande wa serikali ya Kyiv. Uingereza inaendelea kuongeza kuni kwenye moto kwa utaratibu na mara kwa mara," alisema.

    Akijibu, Burnham alisema: "Ni nani aliyeanzisha mashambulizi? Hilo ndilo swali, sivyo?"

    Alisema suala la makombora ya kuzuia mashambulizi litakuwa mada kuu katika mkutano wa muungano wa walio tayari.

    Soma Zaidi Hapa:

  10. Marekani yatangaza mashambulizi makubwa zaidi ya kiuchumi dhidi ya Iran

    d

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Iran yakabiliwa na kile Waziri wa Hazina wa Marekani, Scott Bessent, alichokiita "shambulio kubwa zaidi la kifedha kuwahi kutekelezwa", baada ya Marekani kutangaza mfululizo wa vikwazo dhidi ya Iran na kutishia nchi zinazoiunga mkono.

    Bessent alieleza hatua hiyo kama "siku kubwa ya kiuchumi" kwa Iran, akisema Marekani itasitisha mahusiano yote ya kiuchumi na nchi hiyo. Aliongeza kuwa taifa lolote litakaloshirikiana kifedha na Iran pia litatengwa.

    Hata hivyo, tishio hilo jipya dhidi ya serikali ya Iran linakuja baada ya Ikulu ya Marekani kubadili msimamo mara kadhaa na kuongeza muda wa makataa katika juhudi za kumaliza mzozo huo.

    Kwa upande wake, Waziri wa Uchumi wa Iran, Ali Madanizadeh, alisema Tehran ina mpango wa miaka miwili wa kukabiliana na vikwazo hivyo, akidai mpango huo utasababisha Washington kushindwa tena.

    Vita hivyo vimesababisha kupanda kwa bei ya mafuta duniani. Kufuatia tishio la hivi karibuni la Marekani, Iran imeonya kuwa inaweza kusitisha usafirishaji wote wa mafuta kutoka eneo hilo iwapo vita vitaendelea.

    Serikali ya Iran pia imetoa onyo jipya kwa meli zinazopita katika eneo hilo, ikizitaka kutopita katika Mlango wa Hormuz bila ruhusa yake, kwa mujibu wa Reuters.

    Kwa kawaida, takribani moja ya tano ya mafuta na gesi duniani hupitia Mlango wa Hormuz, njia nyembamba ya bahari iliyoko kusini mwa Iran. Hata hivyo, tangu kuanza kwa mzozo mwishoni mwa Februari, Iran imezuia kwa kiasi kikubwa usafirishaji kupitia njia hiyo, hatua iliyochangia kupanda kwa bei ya mafuta duniani.

    Katika mkutano na waandishi wa habari Jumatatu, Bessent alieleza kile Marekani imekiita "Operesheni ya kuwatenga kiuchumi", akisema Washington inaanzisha "shambulio la kiuchumi dhidi ya miunganisho ya kifedha ya Iran kote duniani".

    Bessent alisema Iran sasa inakabiliwa na chaguo mbili zilizo wazi: "kutengwa kabisa na dunia" au kurejea katika hali ya kawaida na kupata fursa ya kujiunga tena na uchumi wa dunia.

    Waziri huyo wa Hazina alisema Marekani "haitawali tena tishio la Iran, bali inalimaliza".

    Bessent alisema Wizara ya Hazina ya Marekani imebaini mitandao, wawezeshaji na njia za kifedha zinazotumiwa na Iran kukwepa vikwazo na kuendelea kufanya biashara ya mafuta.

    Wizara hiyo imesema imechukua hatua dhidi ya sekta tano, ambazo ni mali za kidijitali, teknolojia, dhahabu, usafiri wa anga na usafirishaji wa majini.

    Aidha, Hazina ya Marekani imetangaza vikwazo dhidi ya karibu taasisi, watu binafsi na meli 60 zinazohusishwa na Iran.

    Soma pia:

  11. Hujambo natumai umzima karibu kwa matangazo yetu ya moja kwa moja ya Jumanne ya 25/08/2026.