Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Je, ni rahisi kuifanya Iran kuwa maskini kuliko kuilazimisha kusalimu amri?
Siku moja baada ya kutangazwa kwa kampeni mpya ya Marekani ya kuweka shinikizo la kiuchumi dhidi ya Iran, vyombo vikuu vya habari nchini humo vilikubaliana katika jambo moja: vikwazo vinaweza kuendelea kuharibu uchumi wa Iran, lakini bado kuna mashaka makubwa kuhusu uwezo wake wa kubadili msimamo au tabia ya Tehran.
Fox News, mtandao unaomuunga mkono Donald Trump, ulikuwa na mtazamo chanya zaidi kuliko mingine, ukieleza kuwa mauzo ya mafuta ya Iran yameshuka kutoka mapipa takriban milioni moja na nusu kwa siku, ambayo iliuzia hasa China kabla ya kipindi cha mzozo, hadi kufikia takriban nusu milioni kwa siku.
Huku ikisisitiza kuhusu mfumuko wa bei wa juu na kupanda kwa kasi kwa bei za vyakula, chombo hicho kilisema: "Iran inaathirika vibaya sana."
Hata hivyo, hata Fox News, chombo cha habari kilicho karibu na Donald Trump, hatimaye kilihitimisha: "Sera za Waziri wa Fedha wa Marekani zinaweza kuifanya Iran kuwa maskini zaidi, lakini haijulikani kama zitasababisha Iran kusalimu amri."
Fox News, ikichunguza shinikizo la kiuchumi lililowekwa dhidi ya Iran wakati wa utawala wa Obama, iliandika kuwa ingawa vikwazo hivyo hatimaye vilisababisha mazungumzo ya nyuklia na makubaliano ya JCPOA, Iran iliweza kudumisha haki yake ya kurutubisha urani.
Katika sehemu ya uchambuzi wake, chombo hicho kilisema: "Si vigumu kuonyesha kuwa vikwazo vimeharibu uchumi wa Iran. Lakini iwapo shinikizo hili la kiuchumi limeweza kutufikisha kwenye malengo yetu ya sera za kigeni ni swali ambalo ni vigumu zaidi kulijibu."
Bloomberg pia iliuliza katika kipindi chake cha sauti (podcast) chenye kichwa "Mshipa wa Uhai wa Uchumi wa Iran" iwapo Iran inaweza kuendelea kupata mapato ya kutosha kuhakikisha utawala wake unasalia madarakani.
Chombo hicho kilihusisha jibu la swali hilo na mambo kama vile sera za China, kiwango ambacho Iran imefanikiwa kukwepa vikwazo, na mwenendo wa bei za mafuta duniani.
Podikasti hiyo ilisema kuwa swali si tu iwapo Iran inakabiliwa na shinikizo; ni wazi kuwa inakabiliwa nalo.
Swali la msingi ni iwapo Iran inaweza kuhimili mashinikizo haya kwa muda usiojulikana bila mfumo wake wa kisiasa kuanguka. Wachambuzi wanasema kuwa jibu la swali hili si dhahiri sana.
Kwa upande mwingine, podikasti ya The Daily Beast imejikita katika athari za ndani za vita hivyo kwa utawala wa Trump.
Kichwa cha uchambuzi huo kinaashiria mwelekeo wake: "Sera ya Trump kuhusu Iran Inageuka kuwa Janga la Kisiasa."
Uchambuzi huo, ukibainisha kuwa hakuna hata moja kati ya malengo yaliyotangaza Trump mwanzoni mwa vita hivyo lililofikiwa, unasema: "Athari za kiuchumi za vita, hasa kupanda kwa bei ya nishati, zinazidi kuwa kero ya kisiasa taratibu.
Trump hayuko kwenye njia ya ushindi; anatafuta njia ya kujinasua kutoka katika mzozo huu bila kuonekana kana kwamba ameshindwa."
Gazeti la The Wall Street Journal pia limeangazia matokeo ya shinikizo la kiuchumi lililowekwa na utawala wa Trump dhidi ya Iran. Gazeti hilo lilibainisha kuwa mauzo ya mafuta ya nchi hiyo yameshuka kwa kiasi kikubwa, huku likirejelea ripoti za watu kukimbilia kununua bidhaa kwa hofu na uhaba wa mafuta katika baadhi ya maeneo ya nchi hiyo.
Hata hivyo, katika sehemu nyingine ya uchambuzi wake, The Wall Street Journal inasisitiza kuwa shinikizo hizo bado hazijaweza kuharibu uchumi wa Iran.
Kama ilivyo kwa Bloomberg, gazeti hilo linaiona China kuwa nguzo muhimu zaidi katika kuendeleza uhai wa mshipa mkuu wa uchumi wa Iran.
Aidha, The Wall Street Journal liliandika kuwa mkakati mpya wa utawala wa Trump wa kuimarisha vikwazo una udhaifu wa kimsingi: Ikulu ya Marekani bado haijaonyesha utayari wowote wa kukabiliana moja kwa moja na benki pamoja na taasisi za kifedha za China.
Gazeti hilo liliandika kuwa, mradi njia hizo ziendelee kuwa wazi, uwezo wa Iran wa kuendeleza baadhi ya miamala yake ya kifedha na mauzo ya mafuta utaendelea kudumishwa.
Wakati huo huo, wanadiplomasia na maafisa wa ngazi ya juu kutoka serikali zilizopita za Marekani wamezidi kueleza waziwazi kuwa sera ya shinikizo na vikwazo vya kiuchumi imeshindwa.
Robert Malley, mwakilishi maalum wa serikali ya Biden katika mazungumzo ya kufufua makubaliano ya JCPOA, aliandika: "Wahanga wakuu [wa vikwazo vya Marekani] watakuwa wananchi wa kawaida wa Iran. Mateso yao yamekuwa kipimo kikuu cha mafanikio ya sera hiyo."
Alikuwa akirejelea kupanda kwa mfumuko wa bei na kushuka zaidi kwa thamani ya sarafu ya rial, viashirio ambavyo Donald Trump na Waziri wake wa Fedha wamevitaja mara kwa mara kama ishara ya ufanisi wa sera zao.
Ben Rhodes, mshauri mkuu wa Barack Obama, pia alisema katika mahojiano kwenye kipindi cha podcast cha Hassan Minhaj: "Netanyahu alijaribu kumvuta Obama kwenye vita na Iran wakati wa miaka yake minane madarakani kama rais, lakini hakufanikiwa.
Hatimaye, aliweza kumshawishi Trump kuishambulia Iran. Lakini tulishindwa katika vita hivi."
Nick Swanson, afisa wa zamani wa serikali ya Trump ambaye alikuwa katika timu ya mazungumzo ya Marekani na Iran katika miezi kabla ya vita na ambaye amefanya kazi katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ikulu ya Marekani kwa karibu miongo miwili, aliandika katika makala ya jarida la Foreign Affairs yenye kichwa "Shinikizo la Juu Zaidi dhidi ya Iran Litashindwa" kwamba vita wala shinikizo la kiuchumi havitawezesha kufikiwa kwa malengo ya Washington.
Bw. Swanson hasemi tu kwamba Marekani imeshindwa vita hivyo; anahoji kuwa hatua hiyo imedhoofisha sana hadhi ya kimkakati ambayo Marekani imejenga kwa miaka mingi kupitia vitisho vya kijeshi na vikwazo vya kiuchumi.
Sasa ni wazi kwa Jamhuri ya Kiislamu, anaandika, kwamba Washington haitawahi kufanya uvamizi wa nchi kavu dhidi ya Iran, na kwamba mashambulizi ya anga na ulipuaji pekee havitaweza kubadilisha mfumo wa kisiasa wa Iran.
Anahitimisha kuwa katika mazingira hayo, serikali zijazo za Marekani zitapata ugumu kutumia tishio la vita kama njia ya kushinikiza na kupata makubaliano au hatua fulani kutoka kwa Iran.