Watanzania sita wameuawa kwenye mpaka wa Msumbiji na Tanzania

Watu sita wameuwawa na watu wasiojulikana
Maelezo ya picha, Watu sita wameuwawa kusini mwa Tanzania, katika mkoa wa Mtwara,
Iliyochapishwa

Walionusurika kwenye shambulio la siku ya Jumanne kusini mwa Tanzania, ambapo watu sita waliuawa kwa kushambuliwa na risasi, wameiambia BBC namna walivyotoroka

Ramadhani Abdallah aliiambia BBC, risasi ilimpata.

"Tulisikia tu ghafla silaha zinapakiwa wakaanza kutupiga na wengine waliuwawa hapo hapo," majeruhi anasimulia.

''Walikuwa na silaha kubwa za smg kila mtu ana silaha yake ,nikapewa silaha ....nikamwambia afande mimi nna tatizo, nivute tumbaku akaniambia sokota tu uvute na mara kazi ikaanza..." majeruhi mwingine ameiambia BBC.

Jeshi la polisi nchini Tanzania limeanza kuchukua za hatua za kiusalama ili kuwanasa watu wote waliohusika na mauaji ya watu sita mpakani mwa Msumbiji ili kuchukuliwa hatua za kisheria.

Watu sita wameuwawa kusini mwa Tanzania, katika mkoa wa Mtwara, usiku wa jumanne ,Novemba 12, baada ya kuvamiwa na watu wasiojulikana.

Watu hao wasiojulikana wamevamia kijiji cha Ngongo wilaya ya tandahimba mpakani na nchi ya Msumbiji na kuwapiga risasi raia hao wa Tanzania na kujeruhi wengine saba.

Jeshi la polisi nchini Tanzania kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola vimesema kuwa tayari wamechukua hatua za kuhakikisha kwamba watu wote waliohusika na mauaji ya watu sita mkoani Mtwara kusini mwa nchi, wanapatikana na kuchukuliwa hatua za kisheria.

Hali hiyo imefanya vyombo vya ulinzi nchini Tanzania kuapa kushirikiana na wananchi mpaka wauaji kutiwa nguvuni.

Liberatus Sabas ni kamishna wa operesheni na mafunzo ya Jeshi la Polisi, kama alivyokuwa akizungumza na wanachi waliojawa na majozi na hasira.

"Tuko bega na bega na nyinyi, vyombo vyote vya ulinzi na usalama tutawasaka na kuwakamata na hatua kali itachukuliwa, dawa ya moto....wengine wako humu humu ndani"

Unaweza kusoma pia kuhusu:

Kwa upande wake mkurugenzi wa makosa ya jinai Robert Boaz amewataka wananchi kutoa taarifa na pia kuchukua tahadhari wanapokwenda nchi jirani kwa shughuli za kibiashara.

Tukio hili la mauaji ni la pili kutokea, ambalo limefanywa na watu wasio julikana, wanaodaiwa kutokea nchini Msumbiji.