Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Mapigano makali yanaendelea kaskazini mwa Gaza wasiwasi ukiongezeka kuhusu watoto wachanga katika hospitali kuu

Mkuu wa WHO anasema "hali ni mbaya na hatari" baada ya kuanzisha tena mawasiliano na waliomo ndani ya Al-Shifa.

Moja kwa moja

Ambia Hirsi, Dinah Gahamanyi and Asha Juma

  1. Marekani yatekeleza mashambulizi ya anga kwenye maeneo ya "Walinzi wa Mapinduzi ya Iran" nchini Syria

    Marekani imesema kuwa imefanya mashambulizi ya anga kwenye vituo viwili vya Iran vilivyoko kusini mashariki mwa Syria, kufuatia mashambulizi ya hivi majuzi dhidi ya wanajeshi wake nchini Syria na Iran.

    Waziri wa Ulinzi wa Marekani Lloyd Austin amesema kuwa mashambulizi hayo yalifanywa dhidi ya maeneo "yanayotumiwa na Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran na makundi yenye uhusiano na Iran."

    Alisema katika taarifa: "Mashambulio hayo yalifanywa dhidi ya kituo cha mafunzo na jumba la kuhifadhi silaha karibu na miji ya Albukamal na Al Mayadin, mtawalia."

    Aliongeza: "Rais hana kipaumbele cha juu zaidi kuliko usalama wa wafanyakazi wa Marekani, na aliamuru kuchukuliwa hatua leo ili kuweka wazi kwamba Marekani itajilinda yenyewe, wafanyakazi wake, na maslahi yake.

    Siku ya Jumatano, Marekani ilianzisha "mashambulizi ya kujilinda" kwa kile ilichosema kuwa ghala la silaha linalotumiwa na Walinzi wa Mapinduzi ya Iran na vikosi vyake shirikishi katika eneo la Maysaloun mashariki mwa Syria.

  2. Daktari wa Al-Shifa anasema 'hakuna mwanamgambo hata mmoja' ndani ya hospitali

    Hakuna "mwanamgambo hata mmoja" ndani ya Al-Shifa, mkuu wa upasuaji wa hospitali hiyo ameiambia BBC.

    Israel hapo awali ilishutumu Hamas kwa kuendesha shughuli zake chini ya ardhi ya eneo la hospitali hiyi kubwa zaidi ya Gaza, jambo ambalo Hamas inakanusha.

    Alipoulizwa kama Hamas ilikuwa inafanya kazi ndani ya Al-Shifa, Dk Marwan Abu Saada aliyataja madai hayo kuwa "uongo mkubwa".

    Katika siku za hivi karibuni eneo la Al-Shifa kaskazini mwa Gaza limekumbwa na mapigano makali, huku Israel ikishutumiwa kushambulia hospitali hiyo moja kwa moja.

    Jeshi la Israel limekiri kuwa linafanya kazi katika eneo la hospitali hiyo, lakini linakanusha kushambulia kituo hicho.

  3. WHO yasema hospitali kuu ya Gaza haiwezi tena kuendesha shughuli zake

    Shirika la afya duniani WHO limesema hospitali ya Al Shifa katika mji wa Gaza haiwezi tena kuendesha shughuli zake.

    Maelfu ya watu wanaripotiwa kukwama ndani ya hospitali hiyo iliyokatiwa umeme kufuatia mashambulizi makali yaliyolenga eneo hilo.

    Mkuu wa WHO Tedros Adhanom Ghebreyesus alisema "milio ya risasi na milipuko ya mara kwa mara" katika eneo karibu na hospitali "imezidisha hali ambayo tayari ni mbaya" na kwamba Al-Shifa "haifanyi kazi kama hospitali tena".

    Jeshi la Israel limekariri kuwa "liko tayari kusaidia" kuwahamisha watoto kadhaa wachanga walio katika mazingira magumu wanaotunzwa kwenye hospitali hiyo hadi hospitali nyingine.

    Mkuu wa upasuaji wa Al-Shifa, Dkt Marwan Abu Saada, ameambia BBC kwamba mtoto wa tatu aliyezaliwa kabla ya wakati amefariki kwa sababu ya ukosefu wa umeme.

    Makumi ya watoto wengine wachanga kwa sasa hawapati huduma wanayohitaji na daktari wa upasuaji alisema "nahofia tutawapoteza watoto hawa wote".

    Akizungumza na BBC hapo awali, rais wa Israel Isaac Herzog alirejelea madai kwamba Hamas ina makao yake makuu chini ya hospitali ya Al-Shifa.

    Hamas inakanusha kutumia hospitali hiyo kwa madhumuni ya kijeshi.

    Dk Abu Saada pia alielezea madai ya Israel kama "uongo mkubwa" na kutoa "mwaliko wa wazi" kwa vikosi vyake vya karibu kuja na kukagua jengo hilo.

    Unaweza pia kusoma:

    • Hezbollah yaonya vita vya kikanda ikiwa mashambulizi Gaza yataendelea
    • Mtoto mmoja huuawa kila baada ya dakika kumi Gaza
    • Nchi ya Amerika Kusini ambayo ina jamii kubwa zaidi ya Wapalestina nje ya Ulimwengu wa Kiarabu na Israeli
    • 'Ninapiga simu kutoka shirika la ujasusi la Israel.Tunarusha bomu, una saa mbili kuondoka’
    • Vita vya Israel na Gaza: Je, uhalifu wa kivita unatekelezwa?, sheria inasemaje?
  4. Hujambo na karibu kwa matangazo ya moja leo Jumatatu 13.11.2023