Harusi ya wapenzi wa jinsi moja yazua utata India
Wakati India ikisubiri uamuzi wa Mahakama ya Juu juu ya kuhalalisha ndoa za watu wa jinsia moja, harusi ya hivi majuzi ya wanandoa wa jinsi moja LGBTQ katika jimbo la kaskazini la Punjab imegonga na vichwa vya habari mara kwa mara na kuzua utata.
Dimple, mwenye umri wa miaka 27 - ambaye anajitambulisha kama mwanaume - na Manisha, anayejitambulisha kama mwanamke 21, walioana katika mji wa Bathinda tarehe 18 Septemba kwa baraka za familia zao - jambo ambalo si la kawaida sana katika nchi ya kihafidhina kama India.
Lakini jambo lisilo la kawaida zaidi ni kwamba ndoa yao ilifungwa katika gurdwara - hekalu la Sikh - na bibi na bwana harusi wakifanya matambiko yote ya kitamaduni.
Harusi hiyo imekosolewa na baadhi ya viongozi wa kidini, akiwemo kasisi mkuu wa dini ya Kikalasinga Giani Raghbir Singh ambaye alitangaza kwamba "ndoa za watu wa jinsia moja hazikuwa za asili na ni kinyume na maadili ya Sikh".
Ndoa ya wanawake wawili mbele ya Guru Granth Sahib - maandiko matakatifu ya Sikh - "ilikuwa ukiukwaji mkubwa wa maadili na kidini", alisema, na kuiagiza kamati ya Bathinda gurdwara kumsimamisha kazi kasisi Hardev Singh, aliyeendesha ndoa hiyo, na watatu wengine kutoka kwa majukumu yao hadi ilani nyingine.
Hardev Singh tangu wakati huo ameondolewa kwenye nafasi yake. Katika utetezi wake, alisema kuwa hakuweza kufahamu kuwa bibi na bwana harusi wote walikuwa wa kike kwani mmoja wa wanawake hao alikuwa amevaa kilemba.
Dimple amehoji madai hayo na kusema kuwa walitoa nakala za uthibitisho wa utambulisho wao kwa gurdwara hivyo hakuna sababu ya kuchanganyikiwa.