Mahakama ya Msumbiji imemhukumu mtoto wa kiume wa rais wa zamani na watu wengine kifungo kwa kuhusika katika kashfa ya rushwa ya "tuna bond".
Mwana wa Rais wa zamani Armando Guebuza, Ndambi Guebuza, na wakuu wawili wa zamani wa ujasusi, Gregorio Leao na Antonio do Rosario, kila mmoja alifungwa miaka 12 jela.
Washtakiwa wenzake nane walitiwa hatiani na kuhukumiwa kifungo cha kati ya miaka 10 na 12.
“Uhalifu uliofanywa umeleta matokeo ambayo madhara yake yatadumu kwa vizazi,” Jaji Efigenio Baptista alisema wakati akitoa hukumu hizo.
Jumla ya watu 19 walikuwa wamefunguliwa mashtaka ya ulaghai, ubadhirifu na utakatishaji fedha kwa madai ya majukumu yao katika kashfa kubwa ya kifedha ya Msumbiji.
Wanane wameachiliwa kwa kukosa ushahidi.
Kashfa hiyo ilihusisha nchi hiyo kukopa zaidi ya $2bn ($1.6bn) kutoka kwa benki za kimataifa, nyingi bila kujua au kuidhinishwa na bunge la nchi hiyo, na kusababisha mzozo wa kiuchumi.
Kati ya 2013-2014, kampuni tatu mpya zilizoanzishwa zilichukua $ 2.2bn (£ 1.5bn) ya deni, nyingi bila ujuzi au idhini ya bunge la nchi.
Pamoja na hayo, serikali ya Msumbiji ilisimama kama mdhamini wa mikopo hiyo, ikimaanisha kuwa serikali ingelipa pesa hizo ikiwa mambo yataenda vibaya.
Pesa hizo zilidaiwa kutumika kununua kiwanda kikubwa cha samaki aina ya jodari na meli ya usalama wa baharini, na pia kufadhili mikataba mingine inayohusisha kampuni ambazo jimbo hilo linamiliki hisa.
Mnamo 2016, serikali ilibadilisha baadhi ya deni kwa bondi ya kawaida, iliyotolewa na serikali.
Muda mfupi baadaye, ilikubali kiwango kamili cha ukopaji, na kusababisha mgogoro wa kiuchumi nchini Msumbiji.
Sarafu ya nchi ilipoteza theluthi moja ya thamani yake, mfumuko wa bei uliongezeka na wafadhili wa kigeni wakajiondoa.
Wakaguzi pia waliripotiwa kugundua $500m ya pesa hizo hazikuwepo.
Mikopo hiyo ilitolewa na Credit Suisse na benki ya Urusi VTB, huku mabenki watatu ya zamani ya Credit Suisse wakikiri mashtaka ya Marekani ya utakatishaji fedha juu ya kesi hiyo.
Mwishoni mwa mwaka jana mamlaka ya Uingereza iliitoza benki ya uwekezaji faini ya $178m kutokana na kashfa ya ufisadi wa samaki aina ya jodari.
Benki hiyo pia iliamriwa kufuta deni la $200m "lililochafuliwa na ufisadi" ambalo lilikuwa linadaiwa na Msumbiji.
Faini hiyo ilikuwa sehemu ya maafikiano ya $475m na wadhibiti wa Uingereza, Uswisi na Marekani.