Nchini Tanzania, tatizo la utapiamlo kwa
watoto walio chini ya umri wa miaka mitano bado ni kubwa.
Miongoni mwa mikoa yenye idadi kubwa wa
watoto hao ni mkoa wa Shinyanga uliopo kaskazini Magharibi mwa Tanzania, ambapo
asilimia kumi na tano ya watoto wana uzito pungufu huku asilimia 32 wakiwa na
udumavu. Hii ni kwa mujibu Tafiti ya Taifa ya Lishe yani Tanzania National
Nutrition Survery ya mwaka 2018/2019.
Kundi la kina mama lenye watoto
wanaosumbuliwa na tatizo la utapiamlo uliosababishwa na upungufu wa madini
chuma na vitamin A hivyo kuwa na utizo pungufu limekamilisha mafunzo ya wiki
mbili ya mapishi bora yanayojumuisha makundi matano ya vyakula vyenye
virutubishi kwa watoto.
Baadhi ya akina mama kutoka kijiji cha
Wijiteleja kilichopo mkoani Shinyanga kaskazini magharibi mwa Tanzania,
wanaelezea jinsi mafunzo hayo yalivyoongeza uzito wa watoto wao.
Magdalena John Kumalia awali mtoto wake alikuwa
na kilo ambazo sio nzuri, lakini baada ya kumpikia vyakula vyenye virutubishi
hali ilibadilika.
“Mwanangu alikuwa na kilo saba tu, tukaanza
darasa la mapishi, tukaanza kumpikia. Tulikuwa tunapika uji, tunaweka karanga,
maziwa, tukiivisha, tunaepua na kuweka mbogamboga za majani, mpaka leo
tumepima, mwanangu ana kilo tisa,” anasema Magdalena.
Nae Agnes Ngelela anasema mbali na mtoto
wake kuwa na kilo moja alipozaliwa lakini pia aliandamwa kwa magonjwa kama vile
kuharisha na kutapika, lakini sasa magonjwa yote yameisha baada ya kupata lishe
bora.
Christian Ngowi ambae ni mganga mfawidhi wa zahanati ya Mundo
mkoani humo anasema mafunzo hayo yalilenga zaidi kutumia vyakula, mbogamboga na
matunda ambayo upatikanaji wake ni rahisi katika jamii inayozunguka.
“Tuliona katika kundi la mbogamboga, kuna changamoto kubwa ya
upatikanaji wa kundi hili kutokana na hali ya ukame inayozunguka wilaya yetu.
Kwa hiyo, tulishauriana na afisa kilimo na mtendaji wa kijiji na wahudumu wa
afya tukawafundisha kina mama kuwa na bustani za majumbani, kwa hiyo lile kundi
la mbogamboga sasa hivi kina mama wanalipata kwa wingi bila gharama na kupoteza
muda kwa kwenda sokoni,” anasema Dk. Ngowi.
Wakati huo huo, Dk Frank Mtimbwa kutoka Shirika la World Vision
nchini Tanzania ambalo ndilo linalodhamini mradi huu wa mafunzo ya mapishi kwa
kushirikiana na serikali na wadau wengine wa afya, anasema ili kutokomeza
tatizo la utapiamlo katika jamii imewalazimu kuwashirikisha na kina baba.
“Kwa jamii hizi tulizonazo, mwanaume anaweza akalima na mwanamke
na akauza chakula chote na kwenye familia ukasikia kuna njaa, lakini wakati wa
msimu wa kulima, walilima pamoja na walivuna sana. Kwa hiyo, sasa hivi wanafanya
kazi pamoja na mwisho wa siku wanaamua wauze nini na pesa inayopatikana ifanye
nini,” anasema Dk. Mtimbwa.
Mbali na darasa la mapishi, wanakijiji pia wamehamasishwa
kuanzisha bustani za nyumbani ili kurahisisha upatikani wa mbogamboga pamoja na
viazi lishe ambavyo wataalamu wanadai vina asilimia kubwa ya virutubishi kwa
watoto.