Kampeni za kuelekea uchaguzi kumpata rais ajaye zimeanza nchini
Uganda.
Wagombea 11 akiwemo rais aliyekaa madarakani kwa muda mrefu,
Yoweri Museveni ambaye atawania tena nafasi hiyo katika uchaguzi utakaofanyika
katika kipindi cha miezi miwili.
Masharti makali ya kudhibiti kuenea kwa virusi vya corona
vimewekwa kwenye kampeni, lakini utekelezaji wake umekuwa mgumu.
Rais Museveni
ameanza kampeni katika eneo liitwalo Luweero triangle, eneo ambalo lilikuwa
kitovu cha vita vya msituni vya miaka mitano vilivyomuweka madarakani mwaka
1986.
Mwanamuziki ambaye
sasa ni mwanasiasa Robert Kyagulanyi, maarufu Bobi Wine yuko njiano kuelekea mji
wa West Nile, kuanza kampeni siku ya Jumanne.
Polisi mji wa Mashariki wa Jinja umewatawanya wafuasi wa chama
cha Forum for Democratic Change(FDC) cha mgombea Patrick Amuriat Oboi kwa
kutumia vitoa machozi. Walikusanyika njiani kumshangilia akielekea eneo la
Mashariki kuanza kampeni yake.
Masharti ya afya
wakati huu wa kampeni yanawataka wanasiasa kuepuka mikusanyiko mikubwa kwa kuwa
na mkutano wa watu wasiozidi 70.
Lakini suala hili
limeonekana kuwa gumu kama ilivyoshuhudiwa wakati wa uteuzi juma lililopita,
wakati wafuasi wa karibu wagombea wote walipokusanyika kwa wingi kwenye mitaa
mbalimbali na kwenye vituo vya biashara.
Kinyang’anyiro cha
urais pia kinawahusisha majenerali wawili wa jeshi na mhitimu wa Chuo kikuu
mwenye miaka 24 ambaye hana ajira.
Raia wa Uganda watapiga kura kuchagua rais na wawakilishi tarehe
14 mwezi Januari.