Rais wa Tanzania, John Magufuli amepokea amesema kuwa amepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya vifo vya watu zaidi ya 60 na wengine 70 kujeruhiwa vibaya baada yakuungua kwa moto baada ya lori lililokuwa na shehena ya mafuta kupata ajali na kisha kulipuka moto Mjini Morogoro.
Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu ya Tanzania, Gerson Msigwa imesema Rais Magufuli ametoa pole kwa familia, ndugu, marafiki na wote waliopoteza jamaa zao katika ajali hiyo na pia amewaombea majeruhi wapone haraka.
Taarifa hiyo pia imekemea vitendo vya wananchi wanaovamia magari yenye milipuko akitaka vikomeshwe mara moja.
Ajali hiyo ilitokea mapema Jumamosi mwendo wa saa mbili asubuhi wakati ambapo lori hilo lililokuwa linatoka Dar es Salaam limepinduka karibu na Kituo Kikuu cha Mabasi cha Msamvu baada ya dereva
wa lori kumkwepa mwendesha pikipiki na kisha mafuta yaliyokuwa yakimwagika kushika moto na kuunguza watu waliokuwa wanayachota.
"Nimeumia sana kusikia idadi kubwa ya Watanzania wenzetu waliopoteza maisha katika ajali hii, natoa pole kwa wote walioguswa na vifo hivi hasa familia za marehemu wote, nawaombea marehemu wapumzike mahali pema peponi na majeruhi wote wapone haraka" amesema Rais Magufuli.